Jumapili, 12 Februari 2023

JAJI MKUU WA TANZANIA ASHIRIKI MBIO ZA SIKU YA SHERIA ZANZIBAR

Na Faustine Kapama-Mahakama, Zanzibar

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 12 Februari, 2023 ameshiriki kikamilifu kwenye mbio za kilometa 10 za Siku ya Sheria zilizoandaliwa na Mahakama Zanzibar kwa lengo la kuchangia waathirika wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Mbio hizo zilizoanzia katika maeneo ya Ngome Kongwe au Forodhani na kumalizikia katika Viwanja vya Mapinduzi Square mjini Unguja zimeongozwa na Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi na kuhudhuriwa na viongozi wengine wa Mahakama na Serikali.

Miongoni mwa viongozi wa Mahakama ya Tanzania walioshiriki mbio hizo ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Barke Sehel, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili Mkuu wa Mahakama, Mhe. Wilbert Chuma.

Kwa upande wa Mahakama Zanzibar waliohudhuria mbio hizo ni Jaji Mkuu, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Majaji kadhaa wa Mahakama Kuu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Bw. Kai Mbaruk na Mrajisi, Bi. Valentina Katema.

Akitoa salamu baada ya kumalizika kwa mbio hizo, Mhe. Prof. Juma aliwaambia washiriki waliofurika katika Viwanja hivyo kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amewasikiliza wananchi katika masuala ya udhalilishaji na ukatili wa kijinsia.

Kadhalika, Jaji Mkuu akawaeleza kuwa Mama Mariam Mwinyi, ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation inayojishughulisha pia katika kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia, ana masikio ya kusikia na anawasiliza wananchi katika maeneo hayo.

“Ninachoweza kusema kinachobaki ni sisi wadau katika mnyororo wa utoaji haki kuhakikisha kwamba tunapambana na hayo yote ambayo viongozi wetu wameyaona,” alisema.

Akimkaribisha Mama Mwinyi kuongea na wananchi katika Viwanja hivyo, Jaji Mkuu wa Zanzibar aliwapongeza viongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kushiriki kwenye mbio hizo. Amesema kiasi cha fedha kitakachokusanywa watakipeleka Zanzibar Maisha Bora Foundation kwa ajili ya kuwasaidia wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Jaji Mkuu huyo akabainisha pia kuwa wamengundua imekuwa vigumu kwa wahanga wa vitendo hivyo kupata fidia baada ya wahusika kutiwa hatiani na kufungwa jela. “Mtu akifungwa miaka 30 jela mara nyingi halipi ile fidia anayoamriwa kutoa kwa mwathirika baada ya kutiwa hatiani. Ndiyo maana katika Siku ya Sheria tumekuja na kauli mbiu hii ili kuwasaidia wahanga hawa,” alisema.

Ameiomba jamii kushiriki kikamilifiu katika kupambana na vitendo hivyo kwa kufika mahakamani kutoa ushahidi ili Mahakama iweze kufanya kazi yake vizuri. Mhe. Abdalla amewakumbusha wananchi kuwa Mahakama inaweza kumtia mtu hatiani kwa makosa hayo iwapo shitaka hilo litathibitishwa bila kuacha shaka yoyote.

Akizungumza na wananchi kupitia hafla hiyo, Mama Mwinyi ameipongeza Mahakama ya Zanzibar kwa kuja na wazo hilo la kuwashirikisha kwenye mbio za Siku ya Sheria kwa lengo la kuwasaidia wahanga wa vitendo vya ukatili wa kijinsia kama ilivyo taasisi yake ya Zanzibar Maisha Bora Foundation.

Mama Mwinyi ameeleza kuwa wamedhamilia kuielimisha jamii ili kupambana na vitendo hivyo vibaya na kuhimiza wananchi kushiriki kikamilifu kuvitokomeza. Amesema kuwa Serikali imechukua hatua kadhaa kupambana na vitendo hivyo, ikiwemo kutunga sheria mbalimbali zinazotoa adhabu kali kwa wanaotiwa hatiani na kuzuia dhamana kwa baadhi ya makosa ya aina hiyo. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitazama saa yake kujua muda aliotumia baada ya kushiriki kikamilifu mbio za kilometa 10 za Siku ya Sheria zilizoandaliwa na Mahakama Zanzibar leo tarehe 12 Februari, 2023. Anayemwangalia ni Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi. Kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akitafakari safari ndefu waliyopita katika mbio hizo na wa pili kulia ni Mke wa Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Mama Zaibab Kombo.
Viongozi wakiongozwa na Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi (katikati picha ya juu na wa kwanza kushoto picha ya chini) wakiingia katika Viwanja vya Mapinduzi Square baada ya kukamilisha mbio hizo. Viongozi wengine ni Mke wa Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Mama Zaibab Kombo (wa pili kulia picha juu na chini), Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ( wa kwanza kushoto picha juu) na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani( wa kwanza kushoto picha chini).

Viongozi (juu na chini) wakijiandaa kupasha misuri baada ya mbio ndefu.

Mazoezi mepensi (picha juu na chini) yakianza taratibu kabla ya kupasha misuri.

Pasha pasha imeanza (picha juu na chini).

Pasha pasha inaendelea kwa kasi (picha juu na mbili chini).


Haya sasa, pasha pasha imekolea (picha juu na chini).

Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi akiwasalimia wananchi waliofurika kwenye Viwanja vya Mapinduzi Square.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa salamu baada ya kushiriki mbio hizo.
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla akizungumza na wananchi katika viwanja hivyo.
Meza Kuu ikiongozwa na Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Zanzibar.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni