Jumatatu, 13 Februari 2023

JAJI MKUU WA TANZANIA ASHIRIKI MAADHIMISHO SIKU YA SHERIA ZANZIBAR

·Ahimiza mabadiliko kifikra kuongeza ufanisi, uwazi, ubora wa huduma za utoaji haki

Na Faustine Kapama-Mahakama, Zanzibar

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 13 Februari, 2023 ameungana na wananchi wa Zanzibar, akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kuadhimisha Siku ya Sheria visiwani humo na kuhimiza mabadiliko ya kifikra kuelekea haki mtandao ili kuongeza ufanisi, uwazi na ubora wakati wa kutoa huduma za haki. 

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo yaliyofanyika katika Viwanja vya Mahakama Kuu Zanzibar, Mhe. Prof. Juma amesema kuwa kauli mbiu ya Siku ya Sheria inayohusu “Haki Mtandao kwa Kukuza Uchumi na Ustawi wa Jamii” ni ahadi ambayo Jaji Mkuu wa Zanzibar anaitoa kwa Rais, wananchi na wadau wote wa sekta ya sheria Zanzibar kuwa wamejipanga kufanya mabadiliko katika utoaji wa haki.

“Kama tunavyoelewa, ahadi siku zote ni deni na ninaamini kupitia maadhimisho haya tutapata sisi faida ya ufanisi, uwazi na ubora ambao siyo tu utasaidia utoaji wa haki lakini pia utasaidia uchumi na jamii ya watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ujumla,” amesema.

Jaji Mkuu amebainisha kuwa kwa kawaida mageuzi makubwa kama yanayoahidiwa huleta mabadiliko siyo kutokana na uwezeshaji ambao Rais wa Zanzibar ameahidi kwamba ataiwezesha Mahakama ili ifikie ahadi hiyo, lakini yanahitajika mabadiliko ya kifikra, kimtanzamo na namna huduma za haki zinavyotolewa.

“Tunapozungumzia mabadiliko ya kifikra ni ile ‘business process’, tumezoea ule utaratibu wa kawaida wa kimahakama, shauri linaanzia hatua fulani na kupitia milolongo mingi, lakini mabadiliko ya fikra, ile ‘business process’ ya Mahakama tunatakiwa kuiangalia upya. Kwa hiyo, katika utoaji wa haki tunahitaji kutoka katika zile fikra za kizamani na kuja katika fikra mpya,” Mhe. Prof. Juma alisisitiza.

Aliwakumbusha wananchi maneno aliyosema Rais Mwinyi mwaka jana katika uzinduzi wa Wiki ya Sheria Dodoma ambapo aliwafahamisha azma ya Serikali yake ya kujenga uchumi wa bluu na kueleza kuwa ili kufanikiwa lazima kuwepo mfumo wa kisheria na kimahakama ambao unaendana na uchumi huo.

“Kwa hiyo, maana yake ni kwamba ahadi mnayotoa leo yeye tayari yupo tayari kufanikisha, itabaki sisi na fikra zetu ili mfumo wetu wa sheria uweze kutoa huduma katika huo uchumi wa bluu,” aliwaeleza wananchi waliohudhuria maadhimisho hayo.

Baada ya kuwasilisha salamu hizo, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla alimkaribisha Rais Mwinyi kuzindua Bendera na Nembo ya Mahakama ya Zanzibar. Kadhalika, Jaji Mkuu huyo alimkabidhi Rais Mwinyi ripoti ya utendaji ya Mahakama ya Zanzibar kwa mwaka 2022 kabla ya kumkaribisha kuongea na wananchi.

 Akiongea na taifa kupitia maadhimisho hayo, Mhe. Dkt. Mwinyi amepongeza ushirikiano uliopo kati ya Mahakama ya Tanzania na Mahakama Zanzibar. Amesema kitendo ya Jaji Mkuu wa Tanzania na ujumbe wake kufika Zanzibar na kuhudhuria maadhimisho hayo ni dalili tosha za kuimarika kwa ushirikiano huo.

Kadhalika, Rais Mwinyi ameipongeza Mahakama ya Zanzibar kwa kuja na kauli mbiu hiyo ambayo inaenda sambamba na Dira ya Maendeleo ya Taifa kuhusu Serikali Mtandao. Amesema kuwa umefika wakati wa kufanya mageuzi makubwa katika mfumo wa utoaji haki nchini kwa vile utaratibu wa kuendesha mashauri kwa kutumia makaratasi umepitwa na muda.

Amesema anatambua kuwa haki mtandao lazima iende sambamba na uwepo wa mambo mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa majengo ya kisasa kwa taasisi za haki, hususani Mahakama, uwepo wa nyenzo za TEHAMA, kuwajengea uwezo watumishi kuhusiana na matumizi ya teknolojia na kuwajengea uwezo mkubwa maafisa TEHAMA ili waweze kuanzisha na kusimamia mifumo pamoja na usalama wa miundombinu hiyo.

“Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza juhudi ambazo zimeanzishwa za kuimarisha taasisi zetu za haki ili ziweze kufanya kazi zake kwa ufanisi. Serikali pia itahakikisha kwamba inatenga fedha za kutosha kwa ajili ya kuboresha miundombinu muhimu ya taasisi hizo ili iende sambamba na mifumo ya haki mtandao ambayo tunaendelea kuianzisha,” alisema.

Rais Mwinyi amebainisha kuwa matumizi ya TEHAMA yanafaida nyingi katika shughuli za utoaji haki, ikiwemo usikilizaji na uamuzi wa mashauri kwa haraka, upatikanaji wa takwimu sahihi za mashauri kwa taasisi za sheria na ufuatiliaji bora na usimamizi mzuri wa mashauri.

Amesema kupitia haki mtandao hakutakuwa na ulazima kwa Majaji wa Mahakama Kuu kusafiri kwenda Pemba kusikiliza mashauri, kwani mashauri hayo yataweza kusikilizwa na kuamriwa kwa mfumo wa TEHAMA, shahidi hatalazimika kufika kwenye jengo la Mahakama kutoa ushahidi, bali inaweza kuandaliwa mifumo na kuweza kutoa ushahidi wake hata kwa kutumia simu yake ya mkononi.

“Kwa utaratibu huo mienendo ya kesi itapatikana kwa haraka kwa wahitaji. Zaidi ya hayo watumishi wa taasisi za haki wataweza kufanya mikutano yao, kubadilishana uzoefu hata kushiriki mafunzo kwa njia ya mtandao bila kulazimika kusafiri au kuondoka kwenye ofisi zao. Hayo yakifanyika tutaokoa fedha nyingi ambazo Serikali hutumia kugharamia shughuli hizo, badala yake fedha hizo zitaelekezwa kwenye shughuli nyingine za maendeleao ya nchi,” Rais Mwinyi amesema.

Kwa upande wa Mawakili na wananchi, Mhe. Dkt. Mwinyi amesema nao watanufaika kwani wataweza kufungua mashauri na kufuatilia uendeshaji wa mashauri yao wakiwa nyumbani, vijijini ama ofisini na kwa njia hiyo wataweza kuutumia muda mwingi ambao hutumika kwenye taasisi za sheria kuweza kufanya kazi zingine za kuinua vipato vyao.

“Kwa muhtasari, haki mtandao ina mchango mkubwa wa kuimarisha uwazi, uwajibikaji, utawala bora, ukusanyaji mzuri wa mapato na kuimarisha uchumi wa nchi. Aidha itasaidia kukuza imani ya wananchi na wawekezaji wa nje na wale wa ndani kwa vyombo vya sheria,” amesema.

Awali, akimkaribisha Rais Mwinyi kuongea na wananchi, Jaji Mkuu wa Zanzibar alisema kuwa wamechagua kauli mbiu hiyo kwa vile haki mtandao siyo suala linalohusu Mahakama pekee, bali pia kila mdau anayejihusisha katika mnyororo wa utoaji haki nchini.

Amesema Mahakama Zanzibar inatambua juhudi za Serikali za kuanzisha mifumo mbalimbali ambayo imerahisisha utendaji wa kazi, hivyo wanaunga mkono juhudi hizo kwa kuanzisha mifumo mbalimbali, ukiwemo ule wa kusajili Mawakili kwa njia ya mtandao na mfumo wa kupandisha hukumu katika ZanzLii.

Jaji Mkuu amebainisha kuwa matumizi ya TEHAMA yataondoa usumbufu wa wananchi wakati wa kutafuta haki zao mahakamani, ikiwemo jinsi ya kufungua mashauri kwa njia ya mtandao na kupata hukumu kwa wakati, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri na kuongeza uwazi, hivyo kuimarisha imani kwa Mahakama.

Maadhimisho hayo yalianza majira ya saa 2.30 asubuhi kwa wageni waalikwa na wananchi kuwasili katika viwanja vya Mahakama Kuu Tunguu.

Mhe. Prof. Juma akiongozwa na mwenyeji wake, Jaji Mkuu wa Zanzibar, aliwasili katika viwanja hivyo majira ya saa 3.15 asubuhi akiwa ameongozana na viongozi wengine wa Mahakama ya Tanzania na wale kutoka Zanzibar. 

Rais Mwinyi ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo aliwasili katika viwanja hivyo saa 3.40 na kwenda moja kwa moja kwenye jukwaa kuu na kukaribishwa na viongozi mbalimbali wa Serikali na Mahakama. 

Baadaye Nyimbo za Taifa, Zanzibar na Jumuiya ya Afrika Mashariki zilipigwa kabla ya viongozi wa dini kuiweka shughuli hiyo mikononi mwa Mola.

Baada ya utenzi maalumu uliokuwa umeandaliwa kusherehesha maadhimisho hayo kuimbwa, viongozi mbalimbali walipewa nafasi ya kuwasilisha salamu, wakiwemo Rais wa Chama cha Mawakili Zanzibar, Mkurugenzi wa Mashtaka visiwani humo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa Zanzibar.

Viongozi wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria maadhimisho hayo ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.  Mustapher Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sylvester Kainda. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisisitiza jambo akipokuwa anazungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar yaliyofanyika leo tarehe 13 Februari, 2023.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akizungumza na taifa kupitia maadhimisho hayo.
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla akiwasilisha salamu za Mahakama kwenye maadhimisho ya Siku ya Sheria visiwani humo.



Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (kushoto), Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma pamoja na majaji wengine wakiwasili katika viwanja vya Mahakama Kuu Zanzibar kwa ajili ya maadhimisho ya Siku ya Sheria.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (wa kwanza kulia) akiwasili kwenye viwanja hivyo.
Jukwaa Kuu likiongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati) likiimba nyimbo za taifa.

Majaji wa Mahakama Kuu Zanzibar wakiwa kwenye maadhimisho hayo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akipandisha Bendera ya Mahakama Zanzibar baada ya kuizindua. Chini ni picha ya Nembo ya Mahakama ya Zanzibar aliyoizindua.

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (kushoto) akimkabidhi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi zawadi maalumu iliyoandaliwa na Mahakama kwa ajili yake.
Viongozi wa Mahakama waliohudhuria maadhimisho hayo. Kutoka kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sylvester Kainda na Mtendaji wa Mahakama Zanzibar, Bw Kai Mbaruk. 
Sehemu nyingine ya watumishi wa Mahakama ya Tanzania pamoja na wananchi wengine (juu na picha mbili chini) wakifuatilia matukio mbalimbali kwenye maadhimisho hayo. 



Jukwaa Kuu likiongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati waliokaa) likiwa katika picha ya pamoja na maafisa waandamizi wa Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Zanzibar. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni