Jumanne, 28 Februari 2023

JAJI MUGETA ATETA NA WATUMISHI WA MAHAKAMA KUU IRINGA

Na. Lusako Mwang’onda- Mahakama Kuu Iringa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Ilvin Mugeta amewaasa watumishi wa Mahakama Kuu kwenye Kanda hiyo kuacha kufanya kazi kwa mazoea, bali watekeleze majukumu yao kwa weledi na umakini wa hali ya juu.

Mhe. Mugeta alitoa wito huo hivi karibuni katika kikao cha pamoja alichokifanya na watumishi hao. Aliwaeleza kuwa tegemeo la wana Iringa na Watanzania kwa ujumla katika kuitafuta haki liko kwenye chombo cha Mahakama, hivyo kila mtumishi ahakikishe anawajibika ipasavyo ili kutimiza matarajio ya wananchi.

Ameonya kuwa hatamvumilia mtu yoyote mzembe na mvivu kwenye kufanya kazi katika kipindi chake atakachohudumu katika Kanda ya Iringa. Amesema ni wajibu wa kila mtumishi wa Mahakama kutekeleza kwa umakini na waledi yale yote yampasayo kuyatekeleza kwa mujibu wa Kanuni za Utumishi.

Jaji Mfawidhi huyo alisema Kanuni za Utumishi zinamtaka kila mtumishi wa umma kuwa kazini asubuhi na mapema, yaani saa 1:30 na kutoka alasiri, yaani saa 9:30, hivyo hategemei kuona mtumishi yoyote hazingatii muongozo huo.

Alitumia nafasi hiyo kujitambulisha kwao baada ya kuhamishiwa katika Kanda ya Iringa akitokea katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke mkoa wa Dar es Salaam.

Naye, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanazania katika Kanda hiyo, Mhe. Angaza Mwipopo, akizungumza katika mkutano huo alisisitiza upendo baina ya watumishi.

Alisema ni muhimu kwa watumishi kupendana wao kwa wao na kuwapenda viongozi wao na viongozi nao kuwapenda wanaowaongoza. Jaji Mwipopo alikazia kuwa sehemu yoyote yenye upendo na isiyo na mfarakano huwa na mafanikio katika kazi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Ilvin Mugeta akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu hivi karibuni. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kanda hiyo, Mhe. Angaza Mwipopo na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu kutoka Kanda ya Iringa, Mhe. Maximillian Malewo.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Iringa (juu na chini) ikimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Ilvin Mugeta (hayupo kwenye picha).
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA, Mahakama-Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni