Na. Aidan Robert-Mahakama, Kigoma.
Mahakama ya Tanzania Kanda
ya Kigoma hivi karibuni ilifanya kikao cha Kamati ya Uongozi kujadili mambo
mbalimbali ya kiutendaji na kiutawala, ikiwemo kuweka mikakati madhubuti kuhakikisha
huduma za haki zinatolewa kwa wananchi kwa wakati.
Akizungumza wakati
anafungua kikao hicho cha kwanza kwa mwaka 2023, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Lameck Mlacha aliwataka wajumbe wa Kamati hiyo kuweka
mikakati itakayosaidia kuongeza kasi ya umalizaji wa mashauri na kurahisisha
shughuli za kiutawala.
Jaji Mfawidhi huyo amesisitiza
kuwa usuluhishi utumike ipasavyo kama njia mbadala ya kutatua migogoro, hasa
ile yenye asili ya madai na kuhimiza kasi ya matumizi ya Mahakama Mtandao katika
kuratibu shughuli mbalimbali za kiutawala ili kurahisha utendaji na kuongeza
ufanisi.
“Mtakumbuka tarehe 1
Februari, 2023 wakati natoa hotuba yangu katika maadhimisho ya Siku ya Sheria
niliujulisha umma kwamba kwa mwaka 2022, Kanda nzima iliweza kumaliza kwa njia
ya usuluhishi mashauri 256 kati ya 5,366
yaliyosajiliwa, sawa na asilimia 4.8,” alisema.
Hivyo alisisitiza kwa
mwaka 2023 lazima Kanda hiyo iwekeze zaidi katika eneo hilo pamoja na kuongeza
wigo wa kutoa elimu kwa njia mbalimbali kupitia vipindi vya Radio ili wananchi
wengi wajue umuhimu na faida za utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhuishi.
Naye Jaji wa Mahakama Kuu
kutoka Kanda hiyo, Mhe. Stephen Magoiga, akizungumza katika kikao hicho aliwataka
wajumbe kwenda kusimamia vigezo vya ukaguzi wa Mahakama na Magereza, hususani
suala la ujazaji sahihi wa rejesta na uzingatiaji wa taratibu zote katika
usikilizaji wa mashauri.
Aliwahimiza kufanyia kazi
changamoto na mapungufu yaliyobainishwa katika ukaguzi wa Mahakama na Magereza katika
kipindi cha robo mwaka kati ya Oktoba hadi Disemba, 2022.
Mambo mbalimbali yalijadiliwa
na kuwekewa mikakati ya utekelezaji katika kikao hicho kilichofanyika katika
Ukumbi wa Mahakama Kuu Kigoma na kuwashirikisha wajumbe kutoka Makao Makuu ya
Kanda, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya sita.
Miongoni mwa masuala hayo
ni ongezeko la kasi ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)
katika kusajili, usikilizaji na usimamizi wa shughuli za mashauri na kiutawala.
Masuala mengine ni
tathmini ya utekelezaji wa bajeti kwa robo mwaka ya Oktoba hadi Disemba, 2022, mapitio
ya taarifa ya Mkaguzi wa Ndani na tathmini ya uendeshaji wa maadhimisho ya Wiki
ya Sheria mwaka 2023.
Wajumbe wa Kamati ya Uongozi wa Mahakama Kanda ya Kigoma wakiendelea na kikao.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni