Na. Evelina Odemba – Mahakama Morogoro
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe ameahidi kutoa ushirikiano kwa Hifadhi za Taifa (TANAPA) ili kuhakikisha hifadhi za wanyama pori zinalindwa kwa vizazi vilivyopo na vinavyokuja.
Mhe. Ngwembe alitoa ahadi hiyo hivi karibuni alipotembelea Hifadhi ya Taifa ya Nyerere kufuatia mwaliko toka kwa Mkuu wa Hifadhi wa TANAPA, Kanda ya Morogoro ili kuona na kujifunza namna wanavyoendesha shughuli za uhifadhi.
Alisema Mahakama Kanda ya Morogoro itasimamia katika kutenda haki. “Hatutamuonea mtu wala kumfaidisha mtu, sisi tutasimamia katika kutafsiri sheria ili pande zote zipate haki yao inayostahili,” alisema Mhe. Ngwembe.
Jaji Mfawidhi huyo alisema fulsa waliyoipata ya kutembelea hifadhi hiyo imewapa uwezo wa kuona na kujifunza mambo mbalimbali, jambo ambalo litawarahisishia katika utendaji wa kazi.
Aliongeza kuwa TANAPA na Mahakama zina mahusiano mazuri ya muda mrefu ukizingatia viongozi walishawahi kufika katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro kutoa elimu kwa wadau wa Mahakama ili kupunguza makosa ya ujangili.
Naye Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Messe Chaba, ambaye alikuwa miongoni mwa viongozi waliokuwepo kwenye ziara hiyo alisisitiza kuwekwa mipaka kati ya hifadhi na vijiji ili kuondoa migogoro.
Awali, akisoma taarifa fupi ya hifadhi kwa niaba ya Kamishna wa Hifadhi, Afisa Mwandamizi wa Hifadhi Apaikunda Mungure aliishukuru Mahakama kwa hatua inazochukua, ikiwemo kusikiliza kesi na kutolea hukumu kwenye ngazi ya vijiji kwani imekuwa ikipeleka Hakimu mpaka eneo la tukio ili kusikiliza kesi hizo.
“Inapotokea mifugo imekamatwa hifadhini hupelekea
askari wa hifadhi kusitisha majukumu mengine na kuanza kuichunga mpaka maamuzi
yatakapokamilika. Hivyo kitendo cha kuzipa kipaumbele kesi zetu itaturahisishia
uwajibikaji,” alisema.
Wengine walioshiriki ziara hiyo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kanda hiyo, Mhe. Augustina Mmbando, baadhi ya Mahakimu pamoja na wawakilishi kwa kila kada miongoni mwa watumishi wa Mahakama kutoka Kanda ya Morogoro.
Msafara huo wa Mahakama ulipata pia nafasi ya kutembelea mradi wa kufua umeme katika Bwawa la Mwalimu Nyerere na kujionea namna shughuli za ujenzi na ujazaji maji unavyoendelea.
Ukiwa katika bwawa hilo, Msafara huo ulipokea taarifa fupi kutoka kwa Mkandarasi Mkazi Lutengano Mwandambo ambaye alieleza kuwa mradi huo umefikia asilimia 81.8 na shughuli ya ujazaji maji inatarajiwa kukamilika ndani ya misimu miwili au mitatu endapo mvua zitanyesha kwa wastani.
Mkandalasi Mkazi Lutengano Mwandambo (aliyevaa suruali ya bluu) akitoa maelezo kwa msafara wa Mahakama ulipotembelea mradi wa bwawa la kufua umeme la Mwl. Nyerere.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni