Na Faustine Kapama-Mahakama
Mahakama ya Tanzania imekamilisha
ujenzi wa mfumo wa kunukuu na kutafsiri mienendo na hukumu, hatua inayokwenda kuongeza
kasi na uwazi wakati wa usikilizaji wa
mashauri na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama.
Hayo yamebainishwa na
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma katika hotuba yake aliyoitoa
kwenye maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika kitaifa katika Viwanja vya
Chinangali jijini Dodoma hivi karibuni.
Mhe. Prof. Juma ameeleza
kwenye hotuba hiyo kuwa Mahakama ya Tanzania imekuwa ikitafuta mfumo (software)
unaotumia akili bandia (Artificial Intelligence) kutafsiri mienendo ya mashauri
na hukumu za Mahakama kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili na kutoka Kiswahili kwenda
Kiingereza.
“Tuligundua kuwa
Mahakama ya Juu ya India tayari ilikuwa inatumia
software hiyo kutafsiri lugha kubwa tisa za India na kubaini kuwa India
walipata ujuzi huo kutoka Italia, nchi yenye utaalamu na uzoefu mkubwa wa
kutengeneza programu au softaware za kutafsiri na kuweka sauti katika maandishi
(translation and transcription),” ameeleza.
Jaji Mkuu amesema kuwa
wataalamu wa Mahakama ya Tanzania, Mahakama Kuu
Zanzibar, wakishirikiana na wale wa Serikali Mtandao (eGA) walikwenda Italia
kutafuta na kufanikiwa kutengeza mfumo na kuufundisha lugha ya Kiswahili kwa
lafudhi na sauti mbalimbali za Kitanzania. Ameeleza mfumo huo umejengwa kwa
pamoja kati ya Mahakama ya Tanzania na Mkandarasi Almawave S.P.A wa Italia kwa
kutumia fedha za ndani.
“Utakapoanza kutumika
mfumo huu utawaondolea Majaji na Mahakimu jukumu zito la kunukuu na kutafsiri
mienendo ya mashauri, hivyo kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri, uwazi na
kuimarisha imani ya wananchi kwa Mahakama. Tanzania pia itapata mrahaba wa
asilimia 20 kwa mauzo yoyote ya mfumo huu kwa mtu mwingine,” Jaji Mkuu amesema.
Alitumia fursa hiyo kutambua
uwezeshwaji mkubwa kwa Mahakama uliofanywa na Serikali inayoongozwa na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye kwa mwaka
2022 aliendelea kuiongezea nguvu kazi Mahakama kwa kuteua Majaji 22 wa Mahakama
Kuu.
Mhe. Prof. Juma ameeleza
kuwa uteuzi huo uliofanyika tarehe 6 Agosti, 2022 uliongeza idadi ya Majaji wa
Mahakama Kuu kutoka 78 hadi 100 na hivyo kupunguza mzigo wa mashauri kwa ngazi
hiyo kutoka mashauri 340 hadi 265 kwa wakati huo.
Amebainisha pia kuwa kwa
mwaka 2022, watumishi 292 wapya waliajiriwa, wakiwemo Mahakimu Wakazi 48, ongezeko
lambalo limesaidia pia Mahakama kutimiza mpango wake wa kusogeza huduma zake
karibu na wananchi kwa kuanzishwa kwa huduma ya Mahakama Kuu katika Mkoa wa
Manyara na huduma za Mahakama katika Wilaya 12 kufuatia kukamilika kwa mradi wa
majengo ya Mahakama za Wilaya.
“Uwezeshaji mkubwa
ulifanyika katika miundombinu ya majengo. Katika kipindi cha mwaka jana 2022
Mahakama ya Tanzania imefanikiwa kukamilisha ujenzi wa majengo mapya 32
yakijumuisha majengo 24 ya Mahakama za Wilaya na matano ya Mahakama za Mwanzo. Aidha,
majengo mengine matatu ya Mahakama yamefanyiwa ukarabati mkubwa,” alisema.
Jaji Mkuu ameeleza pia
kuwa ili kuendelea kusogeza huduma karibu na wananchi, kupitia mradi wa
maboresho 2020/21- 2024/25, Mahakama inatarajia kufikisha huduma ya Mahakama
Kuu katika mikoa nane isiyo na huduma hiyo ambayo ni Singida, Pwani, Songwe,
Katavi, Geita, Njombe, Simiyu na Lindi.
Aidha, alisema, Mahakama
inatarajia kujenga Mahakama za Mwanzo 60 na Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki 10,
kikiwemo Kituo kimoja kitakachojengwa huko Pemba na kupitia fedha za ndani kutajengwa
jumla ya majengo 24, kati ya hayo 14 ni ya Mahakama za Wilaya na 10 ni ya
Mahakama za Mwanzo.
Mhe. Prof. Juma kipekee amemshukuru
Rais Samia pamoja na Serikali yote anayoiongoza kwa kuridhia na kufanikisha
Serikali kuingia katika makubaliano na Benki ya Dunia mwishoni mwa Februari
2022 ya kuongeza fedha na muda wa utekelezaji wa mradi huo wa maboresho.
“Kukamilika kwa majengo
hayo kutaongeza pia mahitaji ya watumishi. Ni matumaini yangu kwamba Serikali
itaendelea kuiwezesha Mahakama kwa kutoa vibali vya ajira ili kusaidia wananchi
kupata huduma za Mahakama karibu na maeneo yao kwa gharama nafuu na kwa wakati,”
amesema.
Watanzania waliadhimisha
Siku ya Sheria tarehe 1 Februari, 2023 kama ishara ya kuanza mwaka mpya wa
shughuli za kimahakama kote nchini. Maadhimisho ya kitaifa yalifanyika jijini
Dodoma, ambayo ni Makao Makuu ya nchi na mgeni rasmi akiwa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Sehemu nyingine ya wananchi, watumishi na Mawakili (juu na mbili chini) ikiwa katika Viwanja vya Chinangali wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni