Jumatatu, 6 Februari 2023

MASHAURI 13 YA MAUAJI KATAVI KUSHUGHULIKIWA NDANI YA MWEZI MMOJA

Na. James Kapele – Mahakama, Katavi

Ikiwa zimepita siku tano toka kilele cha Siku ya Sheria kuadhimishwa nchini, Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga imeanza vikao maalumu vya kusikiliza mashauri (sessions) ambapo imepanga kushughulikia mashauri ya mauaji 13 mkoani hapa kwa muda wa siku 31.

Vikao hivyo vinavyoongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Thadeo Mwenempazi vimeanza leo tarehe 6 Februari, 2023 na vinatarajiwa kuhitimishwa tarehe 7 Machi, 2023. Kati ya mashauri hayo 13, nane yatasikilizwa na kutolewa uamuzi na mengine matano yanawahusisha washitakiwa ambao watasomewa mashitaka yao kwa mara ya kwanza.

Awali, Mhe. Mwenempazi alikagua gwaride liloandaliwa na kikosi cha kutuliza ghasia cha Jeshi la Polisi mkoani Katavi kuashiria kuanza kwa usikilizwaji wa mashauri hayo kwa mwaka 2023.

Akiongea na waandishi wa Habari waliohudhuria uzinduzi wa Vikao hivyo katika Viwanja vya Mahakama, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Maira Kasonde amesema kuwa mpango huo wa kuanza kusikiliza mashauri hayo kwa haraka ni kuhakikisha msongamano wa mahabusu unapungua hasa kwa watuhumiwa ambao tayari mashauri yao yameshafikia kwenye hatua ya kusikilizwa.

 Amesema jumla ya vikao vitatu vya kusikiliza mashauri vipepangwa kwa mwaka huu kwa lengo mahususi hilo hilo la kupunguza msongamano wa mahabusu gerezani pamoja na kutoa haki kwa wakati.

“Tumepanga jumla ya mashauri nane ya mauaji ya kusikilizwa kuanzia leo tarehe 6 Februari, 2023 mpaka tarehe 7 mwezi ujao kwa lengo la kupunguza msongamano wa mahabusu gerezani. Kwa mwaka huu tumepanga jumla ya vikao vitatu ili utimiza adhima hiyo.” alisema Mhe. Kasonde.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Thadeo Mwenempazi (mwenye joho jekundu) akikagua gwaride lililoandaliwa na kikosi cha kuliza ghasia kutoka Jeshi la Polisi mkoani Katavi.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama mkoani Katavi, akiwemo Mtendaji wa Mahakama Mkoa wa Katavi, Bw. Allan Mwela (wa pili kulia), ikifuatilia gwaride la uzinduzi wa vikao hivyo.
Sehemu ya kikosi cha kutuliza ghasia mkoani Katavi kikiwa tayari kwa ukagazi.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Thadeo Mwenempazi akipokea salamu za ukaguzi wa gwaride kutoka kwa kiongozi wa kikosi hicho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni