Alhamisi, 2 Februari 2023

WITO WANANCHI KUJIEPUSHA NA MAWAKILI WANAOKWAMISHA USULUHISHI

Na Mwandishi wetu-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania tarehe 1 Februari, 2023 iliazimisha Siku ya Sheria kuashiria mwanzo mpya wa shughuli za kimahakama. Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na wananchi nchini kote, huku ujumbe mkuu ukiwahimiza wananchi kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi kwanza badala ya kukimbilia mahakamani na kujiepusha na Mawakili vishoka.

Mwandishi wetu Stephen Kapiga kutoka Mahakama Mwanza anaripoti kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe Dkt Ntemi Kilekamajenga amewaasa wananchi wa Mikoa ya Mwanza na Geita kuepuka Mawakili wasio na sifa, yaani vishoka kwani ndio wamekuwa chanzo cha mrundikano ya migogoro isiyofika mwisho mahakamani.

“Nawaomba sana wananchi muweze kuwaepuka Mawakili vishoka kwani wao ndio wamekuwa wakisuka zaidi migogoro ili kuona kuwa Mahakama inashindwa kumaliza migogoro hiyo. Ni muhimu sasa kuanza kutumia Mawakili wanaotambulika,” alisema.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Jaji Kilekamajenga alisema kuwa amekaa na kuzungumza na Mawakili wote wa Mkoa wa Mwanza kuhusu umuhimu wa kauli mbiu ya Siku ya Sheria, hivyo kuwataka kabla ya kukimbilia kuleta kesi mahakamani waaze kutatua mgogoro kwa njia ya usuluhishi.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika Mkoa wa Mwanza, Wakili Lenin Njau aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kauli mbiu hiyo kwani imeamsha uelewa wa umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

“TLS Mkoa wa Mwanza tumejipanga kwani tunajua umuhimu huu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi ndio maana kwa mwaka 2019 tulianzisha kituo cha kimataifa cha utatuzi wa migogoro ya kimataifa na kituo hiki kimekuwa kikiendesha mafunzo kwa Mawakili ili kuweza kuwa mahiri katika utatumizi wa migogoro,” alisema.

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali Mkoa wa Mwanza Mamti Sehewa alisema utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi unaokoa muda wa wadau, hivo kuweza kujikita kwenye shughuli zingine za kiuchumi na kukuza uchumi wao.

Akiongea katika hafla hiyo, mgeni mwalika ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Mhe. Hassan Masala aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza aliishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuja na kauli mbiu hiyo kwani itachangia kudumisha amani na mshikamano kwa wananchi kwani katika usuluhishi huwa hakuna anayeshindwa au kushinda bali wote huwa ni washindi.

Maadhimisho hayo yalitanguliwa na burudani mbali mbali kutoka katika vikundi vya kwaya, band na maigizo ambayo kwa ujumla yaliwavutia watu wote walihudhuria.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe Dkt Ntemi Kilekamajenga akikagua gwaride lililoandaliwa na Jeshi la Polisi kwa heshima yake katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini.
Sehemu ya viongozi wa Mahakama wakiwemo Majaji wakifuatilia mwenendo wa gwaride hilo.

Wakili wa Serikali Mkoa wa Mwanza Mamti Sehewa akizungumza katika hafla hiyo. Chinio ni Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika Mkoa wa Mwanza, Wakili Lenin Njau.


Naye Evelina Odemba wa Mahakama Morogoro anaripoti kuwa
Mahakama Kanda ya Morogoro imeadhimisha Siku ya Sheria kwa kutoa takwimu ya idadi kubwa ya maelfu ya wananchi waliofikiwa na elimu ya sheria kwa kipindi cha Wiki ya Sheria.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe alisema kuwa wamefanikiwa kuwafikia wananchi 51,000 katika Wilaya zote za Morogoro.

Idadi hiyo inajumlisha wanawake 27,730 na wanaume 23,858 na kwa upande wa Morogoro mjini jumla ya wananchi elfu 9, 178 wamefikiwa, ikiwa ni ongezeko la watu 2,490 kutoka mwaka 2022 ambapo wananchi 6,731 ndio waliofikiwa.

Kazi hii imefanywa na Mhakama kwa ushirikiano mkubwa toka kwa wadau. Idadi hii haijajumuisha Morogoro Mjini,” alisema.

Aidha, Jaji Ngwembe alisema kuwa kazi ya kutoa maamuzi inawataka Majaji na Mahakimu wawe na uadilifu usio tia shaka kwani Mahakama ndio chombo pekee kilichokathimiwa majukumu ya kutoa haki nchini, hivyo aliomba viongozi wa dini waendelee kuiombea Mahakama.

Naye Mgeni Maalum,ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Fatma Mwassa alisema ni ukweli usiopingika kuwa viongozi wa Mahakama wanashirikiana vizuri na Mihimili mingine hususani Mhimili wa Serikali, huku akiamini utekelezaji wa kauli mbiu yam waka huu 2023 utapunguza mzigo mkubwa wa kesi mahakamani.

Akitoa salamu toka kwa Chama Cha Mawakili wa Kujitegemea (TLS), Wakili  Azizi Mahenge alishukuru kwa ushirikiano mkubwa wanaoupata kutoka mahakamani na kumpongeza Jaji Mfawidhi kwa kuasisi programu ya msaada wa kisheriakwa wananchi.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akihutubia wakati wa hafla ya Siku ya Sheria iliyofanyika katika uwanja wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (aliyesimama juu ya jukwaa) akiwa tayari kwenda kukagua gwaride la heshima lililoandaliwa siku ya kilele cha Wiki ya Sheria.
Sehemu ya waliohudhulia katika hafla ya uzinduzi wa wiki ya sheria.

Kwaya ya Mahakama (Moro VIP Lounge) ikitumbuiza.

Kwa upande wake, Richard Matasha kutoka Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara anaripoti kuwa maadhimisho ya Siku ya Sheria yameadhimishwa katika viwanja vya Mahakama Kuu, ambapo shughuli hiyo ilitanguliwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Zainab Mruke kukagua gwaride lililokuwa limeandaliwa na kikosi cha Jeshi la Polisi.

Baada ya gwaride hilo, Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara, Mhe. Amiri Msumi aliwakaribisha wawakilishi kutoka dini mbalimbali ili kukabidhi shughuli nzima mikononi mwa Mungu. Utambulisho ukafuata wa jukwaa kuu pamoja na wageni mbalimbali mashuhuri.

Kisha Naibu Msajili akaikaribisha kwaya ya Mahakama Kanda ya Mtwara kutumbuiza kwa muziki mwanana uliokonga nyoyo za kila aliyehudhuria. Baada ya hapo salamu kutoka kwa viongozi mbalimbali zilifuata ambao kwa ujumla walisistiza umuhimu wa kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Ikafuata hotuba ya Jaji Mfawidhi ambaye naye alisisitiza kuhusu kauli mbiu ya mwaka 2023. Alitumia fursa hiyo kuwaaga rasmi watumishi wa Mahakama Kanda ya Mtwara baada ya kuhamishiwa kituo kingine cha kazi.

Kabla ya kuhitimisha maadhimisho hayo, Naibu Msajili aliikaribisha kwaya ya Mahakama kwa mara nyingine kuwasilisha shairi la kipekee lililotungwa na Jaji wa Mahakama Kuu kutoka Kanda hiyo, Mhe. Dkt. Eliamani Laitaika. Hakika shairi hilo liliteka hisia za hadhira kutokana na utamu wa tenzi na ujumbe wake.


 

Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara wakiwa katika picha ya pamoja, wakiwemo Jaji Mfawidhi, Mhe. Zainab Muruke (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Mhe Dkt. Eliamani Laltaika (kulia) na kushoto ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara.

Gwaride la Jeshi la Polisi Mtwara.
Naibu Msajili, Mhe. Amiri Msumi akieleza jambo meza kuu.

Wanafunzi wa Chuo cha Ufundi VETA ni moja kati ya wale walioshirika sherehe hiyo.

Naye Paul Pascal kutoka Mahakama Kuu Moshi anaripoti kuwa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi imeadhimisha Siku ya Sheria nchini mwaka 2023 katika viwanja vya Mahakama Kuu Moshi, ambapo mgeni rasmi alikuwa Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Juliana Massabo ambaye ametanabaisha kuwa kauli mbiu ya kwa mwaka 2023 sio utashi wakutungwa bali ni takwa la kikatiba ya Jamuhuri ya Muungani wa Tanzania ya mwaka 1977 kupitia Ibara ya 107A (2) (d).

Alisema Ibara hiyo inatamka bayana kuwa “katika kutoa uamuzi wa mashauri ya madai na jinai kwa kuzingatia sheria, Mahakama zitafuata kanuni zifuatazo yaani kukuza na kuendeleza usuluhishi baina  ya wanaohusika katika migogoro”.

Sambamba na kuonyesha kuwa utatuzi wa migogoro ni suala la kikatiba Jaji Mfawidhi huyo aliwaeleza wananchi baadhi ya sheria zilizotungwa kwa weledi kuwezesha usuluhishi wa migogoro katika taifa, zikiwemo Sheria ya Mwenendo wa Madai Sura ya 33, Sheria ya Taasisi za Kazi na.7/2004 (The Labour Institution Act), Sheria ya Mahakama za usuluhishi wa migogoro ya ardhi sura 216, Sheria ya Ndoa Sura ya 29 na Sheria ya Bima na 10/2009 sura ya 394.

Alibainisha faida kuu za utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, ikiwemo upatikanaji wa haki kwa wakati kwa kuondokana na milolongo ya kisheria katika shauri, upatikanaji wa haki kwa gharama nafuu kutokana na kutokuwepo kwa gharama za uendeshaji wa shauri, kudumisha umoja na mshikamano katika jamii ambapo njia hiyo huondoa uhasabana baina ya wadaawa na kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani kwa kuwa mengi yatamalizika kwa maridhiano.

Naye Mwakilishi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bi. Tamali Mndeme katika hotuba yake alisema kauli mbiu yam waka huu wa 2023 ya Siku ya Sheria ina maana kubwa katika kukuza uchumi wa nchi kama ikitumika kimamilifu kwenye kutatua migogoro mbalimbali.

Kwa upande wake Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Chapta ya Kilimanjaro, Wakili David Shilatu katika hotuba yake alibainisha kuwa dhima ya usuluhishi imekuja wakati sahihi, hivyo akaomba juhudi zifanyike kuwaelimisha wananchi faida za utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Akiwasilisha salamu za Mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Nurdin Babu alimueleza Jaji Mfawidhi kuwa Kamati ya Ulinzi na Usalama  ya Mkoa iko tayari kutoa ushirikiano utakaohitajika katika utekelezaji wa kauli mbiu ya mwaka 2023.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Juliana Massabo akikagua gwaride la Jeshi la Polisi lililoandaliwa kwa heshima yake.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Juliana Massabo akizungumza na wananchi katika maadhimisho ya Siku ya Sheria.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Nurdin Babu akiwasilisha salamu za Mkoa.
Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) Chapta ya Kilimanjaro, Wakili David Shilatu akizungumza kwenye maadhimisho hayo.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama, Kanda ya Moshi wakiwa kwenye maadhimisho hayo.

Kutoka Mahakama Katavi, James Kapele anaripoti kuwa Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Mwananvua Mrindoka ambaye alikuwa mgeni maalum katika maadhimisho ya Siku ya Sheria amefurahishwa na kauli mbiu ya mwaka huu wa 2023 ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza mrundikano wa mashauri mahakamani.

Akiwasilisha hotuba yake, Mhe. Mrindoka amewasihi wadau wote wa haki mkoani hapa kuitumia kauli mbiu hiyo kwa ufasaha kwa kuwa mashauri mengi yatamalizwa kwa usuluhishi isipokuwa yale tu ambayo sheria za nchi haziruhusu kusikilizwa kwa njia hiyo.

“Utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi tena kwa wakati utazisaidia Mahakama zetu kumaliza kabisa tatizo la mlundikano wa mashauri. Hii inatokana na ukweli kwamba wadaawa wengine hupenda mashauri yao kusikizwa kuanzia mwanzo mpaka mwisho hata kama sheria zetu zinaruhusu migogoro hiyo kutatuliwa kwa njia ya usuluhishi,” alisema.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe. Gway Sumaye amesisitiza umuhimu wa kauli mbiu hiyo kuwa imekuja kwa wakati sahihi kwa kuwa sheria nchini zinaruhusu utatuzi wa migogooro kwa njia ya usuluhishi.

“Katika nchi yetu, mfumo wa utatuzi wa migogoro kwa upatanishi upo kwenye sharia zetu, lakini bado nwananchi hawajui na hautumiki ipasavyo hasa kwa  migogoro iliyopo mahakamani. Katika Mahakama zetu miongoni mwa kesi zinazochukua muda mrefu ni mashauri ya madai na sababu moja wapo ni kutojua sheria na manufaa yake,” alisema.

Awali wakisoma hotuba zao, Mwenyekiti wa Maraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Mpanda, Mkuu wa Ofisi ya Mashtaka Mkoa wa Katavi na Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Tanganyika kwa ujumla wao wameipongeza Mahakama kwa kauli mbiu hiyo na kuonyesha utayari wa kuitekeleza kwa vitendo wakishirikiana na wadau wengine katika kada ya sheria.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe. Mwanamvua Mrindoka akitoa salamu za mkoa katika hafla ya kilele siku ya Sheria.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe. Gway Sumaye akiwasilisha hotuba yake katika siku ya kilele cha wiki ya sheria Mkoani Katavi.
Sehemu ya wadau na wageni mbalimmbali waliohudhuria hafla hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Katavi,Bw. Allan Mwela akitoa utambulisho wa wageni mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni