Jumatatu, 13 Machi 2023

HAKIMU MFAWIDHI MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI MTWARA AKABIDHIWA NYENZO

Na Faustine Kapama – Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 13 Machi, 2023 amemkabidhi Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava nyenzo za kufanyia kazi baada ya kuteuliwa kushika wadhifa huo hivi karibuni.

Tukio hilo ambalo lilishuhudiwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma pamoja na viongozi wengine wa Mahakama limefanyika katika Ofisi ya Jaji Mkuu katika jengo la Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam.

Akitoa nasaha na maelekezo baada ya tukio hilo, Jaji Kiongozi alimpongeza Mhe. Mnzava kwa kuaminiwa na kuteuliwa kushika wadhifa huo. Alimkumbusha mambo matatu muhimu ambayo anatakiwa kuyazingatia anapotekeleza majukumu yake.

Mhe. Siyani amemhimiza Hakimu Mfawidhi huyo kusimamia maadili ya Mahakimu na watumishi wa kada nyingine katika Mkoa wake na kuwaunganisha wote ili waweze kutimiza majukumu yao vizuri, hatua itakayomwezesha kupata matokeo.

“Unaposimamia kazi ya msingi ya Mahakama ya kusikiliza na kuamua mashauri lazima kila mtumishi anakuwa mwadilifu. Jamii haitatuamini tukiwa na watumishi wasiowaadilifu hata tunapotoa hukumu zilizosahihi. Kazi yetu ni ya imani ambayo wale tunaowahudumia lazima wawe na imani na sisi,” alieleza.

Hata hivyo, Jaji Kiongozi alimweleza Hakimu Mfawidhi huyo kuwa ili aweze kusimamia maadili lazima aanze yeye mwenyewe kama kiongozi kuwa mwadilifu ndiyo aweze kusimamia wengine, kwani akiyumba atayumbisha jahazi.

“Hatua uliyoifikia leo ni kubwa, ambayo itapunguza uhuru uliokuwa nao, itakunyima fursa ya kufanya mengine ambayo ulikuwa unayafanya kwa uhuru kwa sababu watu watakutazama kwa jicho jingine,” Mhe. Siyani alisema.

Jaji Kiongozi alieleza kuwa anaitazama Mtwara kama Kanda ambayo inahitaji kiongozi ambaye ataunganisha watumishi. Amesema ufuatiliaji ambao umekuwa ukifanyika kwa miaka miwili iliyopita umeonyesha uwepo wa changamoto ya makundi.

“Ili ufanikiwe lazima ufanye kila linalowezekana kuhakikisha una watumishi wa taasisi moja ambayo ni Mahakama ya Tanzania. Ukiyaendeleza na wewe ukawa na kundi la kwako, hautafanikiwa. Kupanda ni jambo gumu, lakini kuanguka ni jambo rahisi. Usikubali kuangushwa,” alisema.

Kadhalika, Mhe. Siyani alimtaka Hakimu Mfawidhi huyo kusimamia majukumu ambayo amepewa, ikiwemo majukumu ya kimahakama yanayohusisha, pamoja na mambo mengine, kusikiliza mashauri na majukumu ya usimamizi na ukaguzi.

“Usiwe Mfawidhi ukaacha kusikiliza mashauri na unaposikiliza mashauri simamia sana kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA). Wewe mwenyewe uwe mfano kwa sababu huko ndiko tunakoelekea, tusisikilize mashauli kizamani,” alisisitiza.

Jaji Kiongozi amemtaka pia kama Hakimu Mfawidhi kuimarisha, kuwa mbunifu na kuonyesha tofauti kati ya Mkoa wake na Mkoa mwingine kwenye matumizi ya TEHAMA kwa sababu hakuna njia ya kurudi nyuma.

Awali, akimkaribisha Jaji Mkuu kukabidhi nyenzo hizo, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma alieleza kuwa Mhe. Mnzava aliajiliwa mwaka 2005 na kufanya kazi katika Mahakama ya  Hakimu Mkazi Mbeya kabla ya kuhamishiwa katika Baraza la Ardhi na Nyumba mwaka 2008.

Ameeleza kuwa mwaka 2020, Mhe. Mnzava alihamia katika Mahakama ya Wilaya Tarime hadi mwezi Mei 2021 alipoteuliwa kuwa Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu na amehudumu katika Mahakama hiyo hadi Februari 2023 alipoteuliwa kuwa Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo fupi ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Silvester Kainda, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hussein Mushi na Mtendaji kutoka Mahakama Kuu, Masjala Kuu, Bi Maria Itala.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (juu na chini) akimkabidhi Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava nyenzo za kufanyia kazi katika hafla iliyofanyika leo tarehe 13 Machi, 2023 jijini Dar es Salaam.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiweka sahihi kwenye moja ya nyenzo hizo.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akiwasilisha nasaha kwa Hakimu Mfawidhi huyo.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma (aliyesimama) akieleza kwa kifupi historia ya Mhe. Mnzava.  Wengine ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani (kulia), Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Silvester Kainda (wa pili kushoto) na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (kushoto).

Viongozi kadhaa waliohudhuria hafla hiyo. Kutoka kulia ni Naibu Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi, Mtendaji kutoka Mahakama Kuu, Masjala Kuu, Bi Maria Itala,  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hussein Mushi na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava akifuatilia kwa makini yaliyokuwa yanajiri kwenye hafla ya kukabidhiwa nyenzo za kufanyia kazi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimpongeza Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava baada ya kumkabidhi nyenzo za kufanyia kazi. 

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akimpongeza Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava baada ya kukabidhiwa nyenzo za kufanyia kazi. 


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava (katikati). Kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ( wa tatu kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava (wa tatu kulia) pamoja na viongozi wengine wa Mahakama.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ( wa nne kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava (wa nne kulia) pamoja na viongozi wengine wa Mahakama.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni