Jumatatu, 6 Machi 2023

JAJI MFAWIDHI MOROGORO AHIMIZA UTENDAJI BORA MAHAKAMANI

·Anyoshea kidole gumba mfumo mpya wa kupokea maoni, malalamiko

Na Faustine Kapama`– Mahakama, Morogoro

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe amewahimiza watumishi wote katika Kanda zote za Mahakama nchini kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uaminifu wa hali ya juu ili kuondoa viashilia vya rushwa na malalamiko ya kiutendaji yanatotolewa na wananchi.

Mhe. Ngwembe ametoa wito huo leo tarehe 6 Machi, 2023 alipokuwa anafungua mafunzo ya kushughulikia malalamiko kwa njia ya mfumo wa kielekroniki (e- complaint) ambayo yamewaleta pamoja Naibu Wasajili na Watendaji kutoka Kanda zote za Mahakama yanayofanyika katika Ukumbi wa Magadu mjini Morogoro.

Mafunzo hayo yanatolewa baada ya Mahakama ya Tanzania kuanzisha mfumo mpya wa kisasa wa kielektroniki uitwao “Sema na Mahakama” utakaotumika katika kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko (mrejesho) kutoka kwa wananchi.  Mfumo huu unatarajiwa kurahisisha njia za uwasilishaji wa maoni kuongeza uwazi katika kushughulikia maoni, malalamiko na kuweza kukusanya taarifa sahihi kutoka kwa wadau wa Mahakama, wakiwemo wananchi.

“Mahakama kilikuwa ni chombo cha kulalamikiwa kila mwaka. Sasa, kutokana na mapinduzi makubwa yanayoendea kufanyika, tunataka Mahakama iwe chombo cha kupongezwa na siyo kulalamikiwa na kusutwa. Nataka Kanda zote za Mahakama Tanzania tusisikie lalamiko lolote la rushwa. Ili tuondokane na hili lazima tujikite pia kwenye uelimishaji wa wananchi,” alisema.

Alitolea mfano wa Kanda yake ya Mororogo ambapo baada ya kufanya utafiti wa kina hivi karibuni imebainika malalamiko ya vitendo vya rushwa yanayopokelewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rusha (TAKUKURU) ni yale yanayohusu uelewa mdogo wa wananchi wa masuala ya kisheria.

“Nilimwita Mkuu wa TAKUKURU hapa Morogoro, nikakaa naye ofisini, nikamwambia aseme usafi wa Mahakama katika Kanda nzima ya Morogoro ukoje. Nilimwambia aseme ukweli, asinifiche kitu chochote. Aliniambia kwa sasa hajapokea lalamiko lolote za rushwa, isipokuwa tuhuma ambazo zilichunguzwa na kubainika zinahusu uelewa mdogo kwenye masuala ya kisheria,” alisema.

Mhe. Ngwembe alisema sasa anauhakika Mahakama ya Tanzania itafikia asilimia 80% au zaidi kujenga imani ya wananchi kwa Mahakama ifikapo mwishoni mwa mwaka 2025, kufuatia hatua mbalimbali zilizochukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa katika kushughulikia changamoto zinazowakabili.

Ametaja hatua zilizokwisha chukuliwa na Mahakama ni pamoja na kuanzisha mfumo huo maalumu wa kushughulikia maoni, maulizo na malalamiko ya wananchi, hivyo malalamiko mengi waliyokuwa wanayasikia huko nyuma yatakuwa historia.

Jaji Mfawidhi huyo amebainisha pia kuwa sambamba na kuwepo mfumo huo maalumu, watekelezaji muhimu wake ni hao Naibu Wasajili na Watendaji ambao wamekusanyika kupata mafunzo hayo ili mfumo uliopo uweze kutekelezwa ipasavyo katika Kanda zao. 

“Ni imani yangu kuwa kupitia mafunzo haya mtapata ujuzi wa usimamizi wa mfumo huu ili uwawezeshe kushughulikia maoni, maulizo na malalamiko ya wananchi kielektroniki. Tunatarajia kuwa baada ya mafunzo haya mtakwenda kuwafundisha maafisa malalamiko walio katika Kanda zenu na kwa ujuzi mtakaoupata, mtasimamia na kuhakikisha kuwa maoni, maulizo na malalamiko yanawasilishwa na kushughulikiwa kwa wakati kupitia mfumo huu,” alisema.

Mhe. Ngwembe alisisitiza kwamba lengo la kufikia asilimia 80% ya kuridhika kwa wananchi na huduma zinazozitolewa na Mahakama haliwezi kufikiwa kwakuwa na mfumo mzuri wa kutoa na kupokea mrejesho pekee, bali kuwa na maafisa wenye weledi na kujituma katika kutekeleza wajibu wao.

Hivyo anatarajia matumizi ya mfumo huo utamilikiwa na kutumiwa ipasavyo na watendaji hao wenyewe na watawasimamia maafisa malalamiko waliochini yao ili kuhakikisha wanaufahamu vyema na wanautumia ipasavyo.

“Simamieni utekelezaji wake ili kuona kila maoni au malalamiko yaliyowasilishwa yanashughulikiwa kwa wakati kwa mujibu wa Mkataba wa Mteja ambao Mahakama tumejiwekea. Ninyi mkawe chachu ya kuutangaza mfumo huu kwa umma na namna unavyofanya kazi ili waweze kuujua na kuutumia kikamilifu,” alisema.

Akiwasilisha neno la shukrani baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo, Naibu Msajili kutoka Idara ya Usimamizi na Ukaguzi wa Shughuli za Kimahakama na Maadili, Mhe. Kinabo Minja alieleza kuwa tafiti zilizofanyika mwaka 2015 zilionyesha kiwango cha wananchi kuridhika na huduma zinazotolewa na Mahakama kilikuwa asilimia 61.

Alisema baada ya kuchambua na kuingiza masuala mbalimbali yaliyoonekana kuwa na changamoto kwenya Mpango Mkakati wa Mahakama na baadaye kufanyiwa kazi kikamilifu, kiwango cha wananchi kuridhishwa na huduma za kimahakama kilipanda hadi asilimia 78 kwa mwaka 2019.

“Lengo kwa sasa ni kuhakikisha tunaendelea kuboresha huduma zetu, tunawajibika kwa wananchi, ni jukumu letu kuhakikisha wananchi wanaridhika na huduma tunazozitoa. Tumeshaangalia yale waliyotulalamikia na yale ambayo tunahitaji kuyafanya. Sasa, utafiti mwingine unafanyika, tunaamini kiwango kitaongezeaka na malengo yetu ni kufikia asilimia 80,” alisema.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (juu na chini) akizungumza wakati anafungua mafunzo ya kushughulikia malalamiko kwa njia ya mfumo wa kielekroniki (e- complaint) kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama nchini yaliyoanza leo tarehe 6 Machi, 2023.


Naibu Msajili kutoka Idara ya Usimamizi na Ukaguzi wa Shughuli za Kimahakama na Maadili, Mhe. Kinabo Minja akieleza jambo baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo.
Sehemu ya Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama (juu na chini) wakifuatilia ufunguzi wa mafunzo hayo.

Sehemu nyingine ya Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama (juu na chini) wakifuatilia ufunguzi wa mafunzo hayo.

Sehemu ya tatu ya Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama (juu na chini) wakifuatilia ufunguzi wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati). Wengine ni Naibu Msajili kutoka Idara ya Usimamizi na Ukaguzi wa Shughuli za Kimahakama na Maadili, Mhe. Kinabo Minja (kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Morogoro, Mhe. Augustina Mmbando.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti ya mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wanawake wa mafunzo.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Watendaji wanaoshiriki kwenye mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili wanaoshiriki kwenye mafunzo hayo.



















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni