Jumamosi, 4 Machi 2023

KAMATI YA KANUNI YA JAJI MKUU YAFURAHISHWA NA MABORESHO YA MIUNDOMBINU

Na. Arapha Rusheke- Mahakama, Dodoma

Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania hivi karibuni ilitembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma, jengo la Makao Makuu ya Mahakama pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Majaji jijini hapa na kufurahishwa na miundombimu hiyo inayowekezwa na Mahakama ya Tanzania.

Katika ziara hiyo, Kamati hiyo ilifurahishwa pia na mabadiliko na maboresho yanayofanywa na Mahakama ya Tanzania, hususani eneo la miundombinu katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Rehema Mkuye alifurahi kujionea majengo hayo ya kisasa, hususani jengo la Makao Makuu ya Mahakama ambalo tayari limeanza kutoa baadhi ya huduma za kimahakama.

Wajumbe wa Kamati walioshiriki ziara hiyo ni Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiwemo Mhe.  Mkuye (Mwenyekiti), Mhe. Mwanaisha Kwariko (mjumbe), Mhe. Lugano Mwandambo (mjumbe) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (mjumbe).

Wajumbe wengine waliokuwepo ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma na Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimaliwatu, Bi. Agness Kavishe, ambaye ni mwakilishi. Aidha, ugeni huo uliambatana na Jaji mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Edward Rutakangwa, na Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Bw. Yamiko Malekano.

Kamati hiyo iliambatana na wajumbe wa Sekretarieti akiwemo Mhe. Kifungu Kariho (Katibu Mwenza), Mhe. Hawa Mnguruta (Mjumbe) na Mhe. Daudi Kinywafu (Mjumbe). Wajumbe hao walipokelewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe.  Rehema Mkuye ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania akitia saini kitabu cha wageni katika Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama walipotembelea jengo la Makao Makuu ya Mahakama lililopo Jijini Dodoma. Picha chini akifurahia jambo.

Wajumbe wa Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania wakipokelewa katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma walipowasili katika ziara yao.
Wajumbe wa Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania wakifafanuliwa jambo na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kushoto) pindi wajumbe hao walipotembelea jengo la Makao Makuu ya Mahakama lililopo jijini Dodoma.
Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania, wageni na wenyeji walioshiriki ziara hiyo wakiwa katika Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Wajumbe wa Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakamaya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel pindi walipotembelea jengo la Makao Makuu ya Mahakama lililopo jijini Dodoma.
Wajumbe wa Kamati ya Kanuni ya Jaji Mkuu wa Tanzania na wageni wengine wakiwa katika mradi wa ujenzi wa makazi ya Majaji unaoendelea kutekelezwa katika eneo la Iyumbu Jijini Dodoma (picha juu na chini wakipatiwa maelekezo kuhusiana na mradi huo).

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni