Jumamosi, 4 Machi 2023

KUELEKEA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI: WATUMISHI WANAWAKE WA MAHAKAMA MWANZA MJINI WATOA MSAADA

Na Stephen Kapiga-Mahakama Mwanza

Kikundi cha wanawake ambao ni watumishi wa Mahakama zilipo Mwanza mjini (Judicial Women Mwanza) kuanzia Mahakama Kuu mpaka Mahakama za Mwanzo jana tarehe 3 Machi, 2023 kilitembelea Kituo cha Kulelea Watoto waliotelekezwa cha Forever Angels na kutoa msaada wa pesa na vifaa mbalimbali.

Watumishi hao ambao waliambatana na Mlezi wao, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza, Mhe. Monica Ndyekobora walifanya tendo hilo la huruma ikiwa ni siku chache kuelekea Siku ya Wanawake inayosherekewa dunia kila siku ya tarehe 8 Machi.

Akiwakaribisha watumishi hao katika Kituo hicho kilichopo maeneo ya Bwiru Wilaya ya Ilemela mkoani hapa, Mkuregenzi Msaidizi wa Forever Angels, Bi. Leonola Sanga alisema kuwa Kituo hicho tangu kilipoanzishwa mwaka 2006 mwezi Agosti kikiwa na mtoto mmoja kimelea jumla ya watoto 420.

Amesema kwa sasa wapo watoto 20 wanaolelewa. “Kituo hiki hasa kinashughulika na watoto kuanzia umri wa mwaka 0 hadi miaka mitano na mara nyingi huwa tunapokea watoto waliotelekezwa au kutupwa na wazazi wao,” alisema Bi. Sanga.

Alieleza kuwa katika kushirikiana na idara ya ustawi wa jamii wamekuwa wakitoa taarifa ya kila mwezi kuhusiana na maendeleo ya watoto wanaopokelewa katika Kituo hicho kuwezesha idara hiyo kufanya uchunguzi kwa lengo la kuwatafuta wazazi au ndugu zao.

“Pindi wazazi au ndungu wanapokosekana watoto hao huwa huru kuweza kufanyiwa utaratibu wa kuathiriwa (adoption) kwa wale waliokidhi sifa za kisheria kuweza kufanya hivyo na mtoto anapozidi miaka mitano huwa tunampeleka katika vituo vingine kwa ajili ya kuendelea na masomo, kwani hapa tuna elimu ya awali tu,” Bi. Sanga alisema.

Kituo hicho kinaendeshwa kwa kutegemea msaada wa kutoka kwa wafadhili nje ya Tanzania, hususani katika nchi ya Uingereza, ambapo wafadhili hao hutoa gharama za kulipa mishahara ya wafanyakazi na mahitaji mengine.

Akiutambulisha umoja huo wa watumishi wa Mahakama, Mwenyekiti wa Kikundi cha Judicial Women Mwanza, Bi. Irene Malamsha aliwapongeza wanachama wote kwa kujitolea sehemu ya kipato chao na kuweza kurudisha kwa jamii kwa njia ya msaada katika Kituo hicho.

“Niwapongeze wote kwa hiki ambacho tumefanikiwa kukusanya na kuleta kwa jamii na hasa hawa watoto ambao wametelekezwa na wazazi wao, kwani si hawa watoto ndio waliopenda kuishi katika vituo hivi. Ni jukumu letu kama mama kuweza kusaidia watoto kwa kurudisha kiasi tupacho katika kipato chetu kwa njia hii,” alisema.

Kikundi hicho kimefanikiwa kutoa msaada wa vifaa mbalimbali, ikiwemo sukari, mchele, mafuta ya ngozi na mafuta ya kupika na vifaa vingine vyenye jumla ya kiasi cha shillingi za Kitanzania 500,000/=.

Kikundi cha wanawake ambao ni watumishi wa Mahakama zilipo Mwanza mjini (Judicial Women Mwanza) kikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Kituo cha Kulelea Watoto cha Forever Angels.

Mlezi wa Kikundi hicho, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza, Mhe. Monica Ndyekobora akitoa neno la shukrani.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni