Jumamosi, 4 Machi 2023

MWENYEKITI TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA AWAAPISHA MAKAMISHNA WATATU WAPYA

·Awakumbusha Makamishna wa Tume kubuni utaratibu wa kufuatilia utendaji kazi

Na Faustine Kapama – Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama leo tarehe 4 Machi, 2023 amewaapisha Makamishna wapya wa Tume hiyo walioteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Hafla hiyo ya uapisho imefanyika katika ofisi ndogo za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zilizopo jijini Dar es Salaam. Makamishna hao wapya ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, Wakili Msomi Tom Nyanduga na Wakili Msomi Docas Mutabuzi.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, ambaye ni Kamishna wa Tume, Mhe. Mustapher Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, ambaye ni Katibu wa Tume, Prof. Elisante Ole Gabriel, Makatibu Wasaidizi wa Tume, Bi Enziel Mtei na Bi Alisia Mbuya na watumishi wengine wa Tume hiyo.

Kulikuwepo pia na Makamishna wawili ambao wamemaliza utumishi wao, Wakili Msomi Kalolo Bundala na Msomi Genoveva Kato. Kutoka Mahakama ya Tanzania alikuwemo Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma na Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji, Bw. Erasmus Uisso.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Prof. Juma alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuiwezesha Tume ya Utumishi wa Mahakama.

“Baada ya kipindi cha miaka mitatu kukamilika tulikuwa na hofu, pengine ingechukua muda mrefu kabla ya nafasi kujazwa, lakini aliteua Makamishna watatu ambao wamewezesha mwendelezo wa kufanya kazi za Tume bila kupumzika. Tunamshukuru sana kwa kutupa Makamishna wenye historia (zilizotukuka),” alisema.

Aliwapongeza Makamishna hao wapya kwa kukubali utezi huo kwa kuzingatia kazi wanayoenda kuifanya siyo nyepesi. Kadhalika aliwapongeza Makamishna wanaomaliza muda wao wa kuhudumu katika Tume kwa kazi nzuri waliyofanya.

“Mnaweza kuona mchango wenu kwa kuangalia yale mafanikio tuliyofanya, idadi ya Majaji tuliyopendekeza kwa Rais na idadi ambayo ameikubali kuonyesha kwamba hatua za awali za mapendekezo zilifanyika vizuri. Nakumbuka hata idadi ya Mahakimu katika kipindi chenu ilikuwa kubwa sana. Kwa mwaka 2020/2021 tumeajiri takribani Mahakimu 200 au 300 na kuna masuala ya maadili mengi ambayo mmeyashughulikia,” alisema.

Mwenyekiti wa Tume alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha Makamishna wapya kuwa wao ni wawakilishi wa wananchi katika Tume, hivyo hawatakuwa wanazungumzia maslahi yao binafsi wanapotekeleza majukumu waliyopewa bali wazingatie maslahi ya wananchi kwa ujumla.

Amesema kuwa watumishi wa Mahakama ni tofauti na wabunge au wanasiasa ambao kila baada ya miaka mitano hurudi kwa wananchi kuomba ridhaa upya ya kuwatumikia.

“Sisi kama Mahakama Katiba inatulinda, hiyo nafasi ya wananchi kuangalia utendaji kazi wetu hawana. Kazi yetu muhimu kama Tume ni kuangalia utumishi na utoaji wa huduma unaotolewa na Majaji na Mahakimu kwa niaba ya wananchi,” amesema.

Jaji Mkuu amesema kwa kuwa wananchi hawana nafasi ya kuwaita watumishi wa Mahakama kama watakuwa wamekiuka masharti, Makamishna hao wapya wa Tume hawana budi kutumia hiyo nafasi vizuri katika kuibua maeneo mengine ya kuboresha utumishi wa Mahakama.

Alieleza kuwa kila mwaka Tume huajiri watumishi wapya na kupandisha vyeo, lakini haijapata nafasi ya kupata taarifa za utendaji, ikiwemo kuchukua hatua kwa mtu aliyepewa ujaji, uhakimu, au usajili anapokuwa ameshindwa au kiwango chake cha utendaji kimeshuka.

“Kwa sasa tumejikita zaidi kwenye utovu wa maadili, lakini hatujaangalia kwenye utoaji wa huduma. Haya ni maeneo ambayo tunapaswa kuanza kufikiria tuwe na utaratibu wa kuangalia utendaji wa mara kwa mara kwa kila mmoja, siyo tu suala la mashauri, lakini pia mambo mengine yanayogusa haki kwa ujumla,” alisema.

Kwa upande wao, Makamishna hao wapya kwa nyakati tofauti tofauti walimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uteuzi walioupata, hivyo wameahidi kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo vyao.

Nao, Makamishna waliomaliza muda wao wameshukuru kwa kuaminiwa kuitumikia Tume hiyo. Kadhalika, wamewapongeza Makamishna wapya na kuwahakikishia ushirikiano kutoka kwao ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu. Mmoja wa Makamishina hao alitumia nafasi hiyo kuiomba Tume kuangalia uwezekano wa kutenga nafasi kadhaa za utumishi kwa ajili wa watu wenye mahitaji maalumu kama sera ya Serikali inavyoeleza.

Tume ya Utumishi wa Mahakama inaundwa na wajumbe ambao Jaji Mkuu wa Tanzania, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzani na wajumbe wawili wanaoteuliwa na Rais. Mtendaji Mkuu wa Mahakama huingia kama Katibu wa Tume hiyo.   

Majukumu ya Tume yameelezwa kwenye Ibara ya 113 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikisomwa pamoja na kifungu cha 29 cha Sheria ya Uendeshaji wa Mahakama Na. 4 ya mwaka 2011.

Imeundwa na Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Aidha, Tume hii ni chombo cha kikatiba kilichopewa jukumu la kusimamia uendeshaji wa Mahakama ya Tanzania. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama akimwapisha Kamishna wa Tume hiyo, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika katika hafla iliyofanyika leo tarehe 4 Machi, 2023 jijini Dar es Salaam. 
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama akimwapisha Kamishna wa Tume hiyo, Wakili Msomi Tom Nyanduga
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama akimwapisha Kamishna wa Tume hiyo, Wakili Msomi Docas Mutabuzi
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (juu na chini) akizungumza katika hafla hiyo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, ambaye ni Katibu wa Tume, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa utambulisho wa viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo. Kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, ambaye ni Kamishna wa Tume, Mhe. Mustapher Siyani.
Makatibu Wasaidizi wa Tume, Bi Enziel Mtei (kushoto) na Bi Alisia Mbuya.
Makamishna wapya. Kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, Wakili Msomi Msomi Tom Nyanduga na Wakili Msomi Docas Mutabuzi.
Makamishna waliomaliza utumishi wao, Wakili Msomi Kalolo Bundala (kulia) na Msomi Genoveva Kato.
Viongozi wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria hafla hiyo. Kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma na Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji, Bw. Erasmus Uisso (kulia).
Sehemu ya watumishi wa Tume (juu na picha mbili chini) waliohudhuria hafla hiyo.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makamishna wapya na viongozi wengine wa Mahakama ya Tanzania.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makamishna waliomaliza muda wao wa utumishi.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makamishna wapya na  Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Tume.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni