Jumatatu, 20 Machi 2023

MAHAKAMA SPORTS YANG’ARA KWENYE BONANZA

·Yaizabua TEMESA bao nne, yakwea nafasi ya kwanza

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu imeng’ara katika Bonanza lililoshirikisha timu tatu, zikiwemo Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) na Wakili FC baada ya kuibuka vinara kwa kuzoa pointi nne na mabao matano.

Katika Bonaza hilo lililofanyika kwenye Viwanja vya Shule ya Sheria kwa Vitendo (Law School) Dar es Salaam, timu ya Wakili FC ilishika nafasi ya pili baada ya kupata pointi nne na magori manne, huku TEMESA ikiburuza mkia kwa kupata pointi moja na magori mawili.

Kulikuwepo na mechi tatu zilizoshirikisha timu hizo ambapo mechi ya kwanza ilikuwa kati ya Wakili FC na TEMESA na Wakili FC kuibuka washindi kwa mabao 3:1. Mechi ya pili ilikuwa kati ya Mahakama na Wakili FC ambapo timu hizo zilitoka suluhu kwa kufungana 1:1, huku goli la Mahakama likifungwa na Robert Tende.

Mechi ya tatu ilikuwa kati ya TEMESA na Mahakama ambapo Mahakama iliwazabua TEMESA bao 4:1, magoli ya Mahakama yakifungwa na Kariho Mrisho (2), goli la tatu likipachikwa na Martin Mpanduzi, kabla ya Chilemba Hassan kutikisa nyavu kwa kufunga goli la nne.

Mbali na kutangazwa mabingwa katika Bonanza hilo, Mahakama Sports ilizawadiwa kombe na kutoa mchezaji bora, ambaye ni Kariho Mrisho, Wakili FC nayo ilipata zawadi ya kombe la mshindi wa pili, huku TEMESA ikiambulia kutangazwa kama timu yenye nidhamu.

Akizungumza baadaye, Katibu wa Mahakama Sports Taifa Donald Tende amesema Bonanza hilo liliandaliwa na viongozi wawakilishi wa timu ya Mahakama, Kanda ya Dar es Salaam, lengo likiwa kuboresha afya na kuimarisha ujirani mwema, hatua ambayo ni utekelezaji wa nguzo ya tatu ya Mpango Mkakati wa Mahakama katika kushirikiana na wadau.

Tende, kwa niaba ya uongozi wa Kanda ya Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Jamal Mkumba na Katibu Chilemba Hassan, alisema pia kuwa wamelichukulia Bonanza hilo kama maandalizi ya Mahakama Sports katika ushiriki na mashindano ya Mei Mosi yanayotarajiwa kuanza tarehe 14 Aprili, 2023 mkoani Morogoro.

“Kila Mkoa una uongozi wakilishi ambao uliteuliwa na viongozi wa Mahakama Sports Taifa ili kusaidiana katika kusimamia michezo na kufanya mazoezi ili kuboresha afya mahala pakazi. Kwa hiyo kila Mkoa wamekuwa wakifanya mazoezi na kushiriki mabonanza mbalimbali ya ndani na nje,” amesema.

Sehemu ya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu ikishangilia baada ya kukabidhiwa kombe.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu kabla ya mchezo.

Mwalimu wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu , Spear Mbwembe (juu) akiongea na wachezaji (chini) wakati wa mapumziko. 

Mgeni Rasmi katika Bonanza hilo Rajab Mwaliko (juu) akizungumza na wachezaji (chini).



Timu ya TEMESA.
Timu ya Mahakama Sports.

Timu ya Wakili FC.

Orodha ya Makombe yaliyokabidhiwa kwa washindi mbalimbali.
Mchezaji bora wa Bonanza Kariho Mrisho akikabidhiwa kombe lake.


Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende (kushoto) akimpongeza Nahodha wa Timu ya Mpira wa Miguu, Gisbert Chentro, baada ya kuibuka mabingwa wa Bonanza hili.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni