Jumanne, 7 Machi 2023

MSAJILI MKUU AKUMBUSHIA MAADILI MAHAKAMANI

Na Faustine Kapama`– Mahakama, Morogoro

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma amewakumbusha Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama katika Kanda zote nchini kuzingatia maadili wanapotekeleza majukumu yao ili kulinda taswira ya Mahakama.

Mhe. Chuma ametoa wito huo leo tarehe 7 Machi, 2023 alipokuwa anawasilisha mada kwenye mafunzo yanayofanyika mjini hapa kuhusu mfumo mpya wa kielekroniki (e-complaint) wa kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko (mrejesho) kutoka kwa wananchi. 

“Hatutegemei kuona Naibu Msajili au Mtendaji amevaa suruali ya mlegezo na anatembea kama amefunga tofali nyuma. Huu sio utamaduni wetu ambao tumejiwekea mahakamani,” alisisitiza.

Amesema kuwa Mahakama inategemea kuona mtumishi anayaishi maadili akiwa kazini au nje ya mazingira yake ya kazi ili kuongeza imani ya wananchi kwa Mahakama, kuimarisha amani na maelewano katika jamii na kuiwezesha Mahakama kutekeleza jukumu lake la kikatiba kikamilifu.

Kadhalika, Mhe. Chuma amewakumbusha viongozi hao kuchunga ndimi zao kulingana na nafasi walizonayo katika jamii. “Unajua ukizungumza kitu kwa jamii watapigia mstari kile ulichokisema kuwa alichozungumza ni Hakimu au Mtendaji wa Mahakama.

“Kuna watu hapa wanapenda kucheza muziki, lakini unachezaje. Kuna vitu ambavyo unatamani kuvifanya, lakini mazingira hayakuruhusu. Kwa hiyo, tunatakiwa kuwa waangalifu sana.”

Amesema kuwa Mahakama inategemea kuona mtumishi mwenye maadili akitekeleza majukumu yake kwa kuzingatia misingi ya taaluma yake, mtu anaye heshimu wenzake, anayetunza siri na kuheshimu viongozi au mamlaka.

“Hapa napo kuna tatizo, wengine hawawezi kujisimamia, kila kitu ni kutii tu hata kwa jambo ambalo hatakiwi kufanya hivyo kwa sababu ya uoga. Hata majumbani kwetu kuna utii na kuheshimiana. Hivyo tusome kwa makini kanuni za mwenendo mzuri wa utumishi ili zituongoze vizuri,” alisema.

Alitumia fursa hiyo kutaja baadhi ya faida za kuzingatia maadili kwa watumishi, ikiwemo kuongeza uwajibikaji na ufanisi, uaminifu katika mahusiano, mshikamano katika kazi na kuongeza imani kwa umma. 

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma  (juu na chini) akisisitiza jambo alipokuwa anawasilisha mada kuhusu maadili kwenye mafunzo kuhusu mfumo mpya wa kielekroniki (e-complaint) wa kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko (mrejesho) kutoka kwa wananchi. 

Washiriki wa mafunzo hayo (juu na chini) wakimsikiliza Msajili Mkuu, Mhe. Wilbert Chuma

Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo hayo (juu na picha mbili chini) ikimsikiliza Msajili Mkuu, Mhe. Wilbert Chuma



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni