Jumatano, 8 Machi 2023

MSAJILI MKUU AWAPA ‘NONDO ZA MAANA’ MAAFISA TEHAMA

·Msajili Mahakama Kuu naye awakumusha wasijisahau leo siku ya wanawake duniani

Na Faustine Kapama`– Mahakama, Morogoro

Mafunzo kuhusu mfumo mpya wa kielekroniki (e-complaint) wa kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko (mrejesho) kutoka kwa wananchi yanayofanyika mjini hapa yemeingia siku ya tatu kwa kujumuisha kundi la maafisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wa Mahakama ya Tanzania.

Kundi hili leo tarehe 8 Machi, 2023 lilianza kukutana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, ambaye ‘amewasuka’ kwenye maeneo mawili, ikiwemo kuzingatia maadili na kutoa huduma bora kwa mteja wanapotekeleza majukumu yao katika muktadha mzima wa utoaji haki.

Akiwasilisha mada kuhusu maadili, Mhe. Chuma amewaambia washiriki hao wa mafunzo kuwa maadili ni msingi, taratibu au kanuni ambazo kundi la watu au jamii fulani imejiwekea, kukubalika na kuzingatiwa na kila mtu au jamii husika ili kujenga jamii yenye tabia na mwenendo mwema.

“Hata mahakamani kuna taratibu ambazo kila mtumishi anatakiwa kuzizingatia ili kulinda taswira ya Mahakama. Hatutegemei kumwona mtumishi kufanya mambo ambayo yanakiuka maadili, ikiwemo kuvaa nguo zisizofaa kama za kubana, kuacha wazi maungo ya mwili, kuvaa mlegezo, suruali fupi au pedo na kuvaa viatu virefu vya rangi mchanganyiko,” alisema.

Msajili Mkuu aliwahimiza watumishi hao kuzingatia sheria, kanuni, miongozo na mazoea katika utekelezaji wa jukumu la utoaji haki kwa wananchi. Amesema kwa kufanya hivyo wataongeza tija au ubora wa huduma na kujenga au kuongeza imani ya Mahakama kwa umma.

“Tukitekeleza vema jukumu la utoaji haki kwa kila mmoja wetu kwa nafasi aliyonayo kutalinda taswira ya Mahakama, kutajenga na kuimarisha au kukuza mahusiano miongoni mwa wananchi, hivyo kuleta amani na utengamano kwa taifa, jambo ambalo hupelekea kukuza uchumi endelevu,” alisema.

Mhe. Chuma aliwakumbusha watumishi hao kuwatumikia wananchi ambao ni wateja muhimu kwa Mahakama kwa wakati na bila ubaguzi wa aina yoyote. “Tutumie lugha nzuri siyo tu kwa watumishi wenzetu ambao pia ni wateja wetu lakini pia kwa wananchi, bila wao sisi hatutakuwa na haki ya kuendelea kukaa mahakamani,” alisisitiza.

Naye Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt, kabla ya kuwasilisha mada yake kuhusu “Jinsia katika Muktadha wa Mahakama” alianza kwa kuwaomba washiriki wote kujipigia makofi kwa kusherekea siku ya wanawake duniani.

Aliwaeleza maafisa TEHAMA hao kuwa kuzungumzia jinsia au usawa wa kijinsia hakuna maana ya mwanamke au mwanaume au mwanamke kupewa upendeleo kama viti maalumu ili naye awe sawa na mwanaume.

Mhe. Sarwatt aliwaeleza kuwa jinsia ni hali ya kijamii inayomfanya mtu afahamike katika hali aliyonayo na kutokana na majukumu yake katika jamii na ndiyo inayomfanya kuwa hivyo na kupata fursa au haki ambayo ni sawa na mwingine.

“Mfano wewe afisa TEHAMA ukiweka mitambo yako vizuri na kumwezesha mwananchi ambaye yupo mbali kutoa ushahidi utakuwa umempa fursa sawa kama vile angefanya hivyo ana kwa ana, hii ndiyo usawa wa kijinsia ninaoueleza,” alisema.

Kadhalika, Msajili huyo amewakumbusha washiriki hao wa mafunzo kuwa katika kutekeleza jukumu lake la kikatiba kwa mujibu wa Ibara ya 107A ya Katiba, Mahakama ya Tanzania imekuwa ikizingatia kwa muda wote usawa wa kijinsia.

Alieleza kuwa Mahakama imekuwa ikifanya hivyo ili kuhakikisha kuna usawa kamili katika nyanja zote za maisha na imekuwa ikisisitiza kutenda haki bila kuwa na upendeleo kwa kila mtu kulingana na maadili yanayokubalika au mwenendo wa haki.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma akisisitiza jambo alipokuwa anawasilisha mada kuhusu mfumo mpya wa kielekroniki (e-complaint) wa kutoa na kupokea maoni, maulizo na malalamiko (mrejesho) kutoka kwa wananchi yanayotolewa kwa maafisa TEHAMA mjini Morogoro.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt akizungumza wakati anawasilisha mada kwenye mafunzo hayo.

Naibu Msajili kutoka Idara ya Usimamizi na Ukaguzi wa Shughuli za Kimahakama na Maadili, Mhe. Kinabo Minja akitoa utambulisho wa viongozi kwa washiriki wa mafunzo hayo.

Sehemu ya wajumbe wa sekretarieti wanaoratibu mafunzo hayo.
Sehemu ya maafisa TEHAMA (juu na picha mbili chini) wanaoshiriki kwenye mafunzo.




Sehemu ya maafisa TEHAMA wanawake wanaoshiriki kwenye mafunzo hayo.
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wanawake katika mafunzo hayo.
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (juu na chini) akiwa katika picha ya pamoja na wanawake kwa mitindo ya kusimama tofauti tofauti wanaoshiriki katika mafunzo.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni