Ijumaa, 3 Machi 2023

NEMC WATEMBELEA ENEO LA UJENZI WA KITUO JUMUISHI MKOANI PWANI

Na Eunice Lugiana-Mahakama, Kibaha

Maafisa Mazingira kutoka Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Makao Makuu jijini Dar es Salaam leo tarehe 3 Machi, 2023 wametembelea eneo linatotarajiwa kujengwa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki katika Mkoa wa Pwani ili kufanya tathmini ya athali za mazingira.

Mmoja wa Maafisa hao, Bw. Helmes Cosmas amesema kuwa taarifa kamili ya tathmini yao wataitoa siku chache zijazo kabla ya ujenzi wa Kituo hicho kuanza. Kituo hicho kinatarajiwa kujengwa katika Kata ya Tumbi, Mtaa wa Mkoani A katika Wilaya ya Kibaha.

Kabla ya kutembelea eneo hilo, maafisa hao walimtembelea Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha, Mhandisi Msham Munde ofisini kwake kwa ajili ya utambulisho uliofanywa na Afisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Bi. Malkia Nondo.

Katika mazungumzo yake na maafisa hao, Mhandisi Munde alisema kuwa ujenzi wa Kituo hicho katika Mkoa wa Pwani utasaidia kupunguza usumbufu wa wananchi kwenda kufuata huduma za Mahakama Kuu katika Mkoa wa Dar es salaam.

Wakiwa katika eneo litakalojengwa Kituo hicho, maafisa hao wa NEMC walikutana na Mtendaji wa Mtaa wa Mkoani A, Bw. Adamson Mwandalima, ambaye ameomba ujenzi utakaofanywa uzingatie mazingira rafiki ya miundombinu inayowajali watu wenye mahitaji maalumu.

Ameshauri jengo la Kituo hicho lijumuishe pia huduma muhimu kama stationaries, kantini na sehemu za kupumzikia wakati wananchi wanasubiri mashauri yao kuitwa mahakamani.

Kadhalika, Bw. Mwandamila ameomba pindi ujenzi utakapoanza, kazi zisizohitaji taaluma ziwashirikishe vijana wanaotoka katika Mtaa huo ili wafaidike na mradi mkubwa unaojengwa mtaani kwao.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha, Mhandisi Msham Munde (katikati) akiongea na mmoja wa maafisa kutoka Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Bw. Helmes Cosmas (kushoto) na Afisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibaha, Bi. Malkia Nondo (kulia) walipokutana ofisini kwake leo tarehe 3 Machi, 2023.
Eneo ambalo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kitajengwa katika Kata ya Tumbi, Mtaa wa Mkoani A, barabara ya Uhamiaji.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni