Jumamosi, 29 Aprili 2023

JAJI MFAWIDHI SUMBAWANGA AONGOZA KIKAO CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI

Na Mayanga Someke-Mahakama, Sumbawanga

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Amir Mruma jana tarehe 28 April, 2023 aliongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo, kujadili mambo mbalimbali yanayohusu wafanyakazi wa Mahakama kutoka Mikoa ya Katavi na Rukwa.

Kadhalika, kikao hicho kililenga kuangalia hoja za wafanyakazi na maazimio kuelekea Baraza Kuu la Wafanyakazi Taifa. Mhe. Mruma aliwaambia wajumbe kuwa Mabaraza hayo yanaundwa kwa mujibu wa sheria na kwa kufuata misingi halali.

 ‘’Hoja za wafanyakazi zijadiliwe na kutolewa majibu yake na wafanyakazi wapate mrejesho kupitia Baraza hili na tufanye maazimio kwa pamoja ili tuwe na kauli moja sisi sote kama wafanyakazi,’’alisema Mhe. Mruma alipokuwa anafungua kikao hicho.

Jaji Mfawidhi alipendekeza kuwa watumishi wasio maofisa wa Mahakama (Non-Judicial Officers) wapate sare itakayoendana na maadili ya Mahakama, hivyo mwaka wa fedha 2023/2024 itengwe bajeti kwa ajili ya kuwanunulia watumishi hao, hasa wale wanaoingia mahakamani ili kuwa na sare itakayowatambulisha kwa wateja.

“Nasisitiza tutenge bajeti kwa ajili ya sare kwa watumishi wanaongia mahakamani na pia tusimame imara kuzungumzia mazuri ya Mhimili wetu wa Mahakama kuanzia Mhudumu mpaka nafasi ya Jaji na sio kuiongelea Mahakama kama idara,’’aliongeza.

Jaji Mfawidhi aliwashukuru wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi na kuwaahidi kuendeleza ushirikiano na TUGHE ili kuweka uwiano was pale panapotokea jambo linalowahusu wafanyakazi.

Baada ya ufunguzi wa kikao, Katibu wa TUGHE, Bw. Ayub Nyarobi alianza kusoma agenda mbalimbali za kikao ambapo kwa kauli moja walizipitisha bila mabadiliko na kumalizia kusoma muhtasari wa kikao cha Baraza kilichopita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Amir Mruma akizungumza wakati anafungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi. 

Viongozi wa Mahakama Kanda ya Sumbawanga wakifuatilia ufunguzi wa kikao hicho. Kuanzia kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Bw. Emmanuel Munda, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Maira Kasonde, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi, Mhe, Gway Sumayi na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Sumbawanga, Mhe. Kisasila Malangwa.

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Kanda ya Sumabwanga kutoka Mikoa ya Katavi na Rukwa wakiwa kwenye kikao hicho.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni