Jumamosi, 29 Aprili 2023

MAHAKAMA MSHINDI WA NNE MASHINDANO YA MEI MOSI

·Timu za Mpira wa Miguu, Kamba na Riadha zachomoza

Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

Timu ya mpira wa miguu na timu ya kamba wanaume toka Mahakama Sports Klabu zimeibuka mshindi wa nne katika mashindano ya kuwania kombe la Mei Mosi yanayoendelea mkoani hapa.

Michezo hiyo ilifanyika jana tarehe 28 Aprili, 2023 katika uwanja wa Jamhuri ambapo kwa upande wa mpira wa miguu Mahakama ilicheza na Tanesco na kupata goli moja (1) huku Tanesco ikiondoka na goli mbili (2) na kwa upande wa Kamba, Mahakama ilivutana na Ikulu.

Michezo hii yote ilishuhudiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ambaye alitoa pongezi zake za dhati kwa washiriki wote na kusema kuwa hakika wamefanya kazi nzuri na wameiwakilisha vyema Mahakama ya Tanzania upande wa michezo na hata katika nidhamu.

Mara baada ya michezo kumalizika Mtendaji Mkuu alipata wasaa wa kuzungumza na wachezaji wote wanaoiwakilisha Mahakama katika mashindano hayo. Alisema alifika kuwaunga mkono kwa niaba ya uongozi wa juu wa Mahakama ukiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Alisisitiza kuwa katika michezo kuna vingi vya kujifunza zaidi ya kuwa washindi pekee, kwani kupitia mchezo huo alioushuhudia ameona vipaji vingi na kazi kubwa ambayo wanamichezo hao wameifanya uwanjani.

Prof. Ole Gabriel aliwataka wanamichezo hao kutokata tamaa kwa kuwa hawakufanikiwa kupata nafasi ya kwanza kama walivyokusudia. “Nilitaka kuondoka ila nikaona nisubiri kwani mtu asiposhinda ndio anahitaji kutiwa moyo zaidi kuliko hata angeshinda, kikubwa nawaomba kutokata tamaa, mimi Mtendaji Mkuu wa Mahakama sijakata tamaa sasa nyie mtakataje tamaa?” aliuliza.

Sambamba na hilo, Mtendaji Mkuu alivutiwa na namna michezo ilivyoweka ushirikiano baina ya kada tofauti tofauti ndani ya Mhimili wa Mahakama na kueleza, “Nimeona Hakimu anafunga magoli na anapasiwa mpira na RMA, golikipa nae ni Hakimu ni jambo zuri, naamini mashindano yajayo tutafanya vizuri zaidi,” alisema. Alimwomba Kocha Spear Mbwembe asikate tamaa na kuahidi kuwa watajitahidi kuboresha kwa kuwezesha wanamichezo kupata wasaa mzuri wa kukaa kambini kwa mazoezi na hata kuwezesha wanamichezo wengi kushiriki kadri ambavyo bajeti itaruhusu.

Awali, kabla ya kuanza kwa mechi hizo za kuwania mshindi wa nne, wanamichezo wa Mahakama walipata fulsa ya kutembelewa na Mkurugenzi wa Utawala na Raslimali Watu, Bi. Beatrice Patric katika kambi waliyofikia na kuzungumza nao machache. Bi. Patrick aliwaambia wanamichezo hao kuwa michezo inajenga urafiki na kuleta umoja na afya, hivyo hatua waliyofikia ni nzuri na Mahakama iko pamoja nao.

Naye Mwenyekiti wa Mahakama Sports Klabu Wilson Dede alihitimisha kwa kusema kuwa mwisho wa mashindano haya ndio mwanzo wa kujipanga kwa ajili ya michezo ijayo.

Alieleza kuwa wao kama viongozi wamepanga kukaa kikao kujadili kama wanamichezo ili kuboresha katika mashindano yajayo waweze kufanya vizuri zaidi.

Mashindano ya kuwania kombe la mei mosi yanategemewa kumalizika leo tarehe 29 Aprili, 2023. Katika michezo mingine, Mahakama imeibuka mshindi wa pili kwenye bao, mshindi wa nne karata na mshindi wa nne riadha.

Kumalizika kwa mashindano haya ni mwanzo wa maandalizi ya michezo inayofuata ya SHIMIWI ambayo inatarajiwa kufanyika mkoani Iringa kwa mwaka wa 2023.

Kikosi cha timu ya Kamba (ME) toka Mahakama kikivutana na Kamba (ME) toka Ikulu (hawapo pichani) huku wakishuhudiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyevaa traki suti ya bluu).

Mtendaji Mkuu wa Mahakama wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyevaa nguo ya bluu) akiwasili katika uwanja wa Jamuhuri Morogoro na kupokelewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala Stephen Magoha na Mwenyekiti wa Mahakama Sports Klabu Wilson Dede (aliyempa mkono) ili kushuhudia timu za Mahakama zilizokuwa zinacheza kuwania mshindi wa nne.

Timu ya mpira wa miguu toka Mahakama Sports Klabu wakiwa katika picha ya pamoja na kocha wao Spear Mbwembe.

Mkurugenzi Utawala na Raslimali Watu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patric akiwa katika picha ya pamoja na wachezaji wa timu ya mpira wa pete toka Mahakama Sports Klabu.

Mkurugenzi wa Utawala na Raslimali Watu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patric akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Mahakama Sports Klabu alipotembelea kambi ya wanamichezo hao mkoani Morogoro.

Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala Stephen Magoha akisalimiana na kikosi cha timu ya mpira wa miguu toka Mahakama sports klabu kabla ya kuanza kwa mechi dhidi ya Tanesco.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyevaa nguo ya bluu) akionesha jambo wakati mchezo dhidi ya Mahakama na Tanesco ukiendelea. Kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala Stephen Magoha na kulia ni Mwenyekiti wa Mahakama Sports Klabu Wilson Dede.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiteta jambo na Nahodha wa timu ya mpira wa miguu Seleman Magawa mara baada ya mechi kumalizika.
Picha ya pamoja kikosi cha mpira wa miguu toka Mahakama wakiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisalimiana na timu ya Kamba (ME) toka Mahakama kabla ya mchezo wao dhidi ya Ikulu.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni