Jumanne, 30 Mei 2023

JAJI DKT. NDIKA AZINDUA TOLEO LA TATU MFUMO WA KUTUNZA MAAMUZI

Na. Innocent Kansha-Mahakama

Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. Dkt. Gerald Ndika jana tarehe 29 Mei, 2023 amezindua Tovuti toleo la tatu la mfumo maalumu wa kutunza maamuzi ya kimahakama ujulikanao kama TanzLII wenye kauli mbiu isemayo ufikiaji na upatikanaji bure wa Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania kwa njia ya Mtandao “TanzLII - Access Court Decisions and Laws of Tanzania for Free”.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke Mkoa wa Dar es Salaam na kuhudhuriwa na machampioni wa mfumo huo, wakiwemo Majaji wa Mahakama wa Mahakama ya Rufani na wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Makatibu wa Sheria wa Majaji na Wakutubi, Mhe. Dkt. Ndika alisema kuwa ni fursa muhimu kuzindua mfumo huo mpya unaofanya kazi kwa takribani miaka tano sasa kwa ufanisi mkubwa.

“Natambua kuwa mfumo huu tunaouzindua leo ulioboreshwa wenye muonekano mpya ni toleo la tatu wenye uwezo wa kufanya kazi nyingi zaidi ikilinganishwa na ule wa awali na sasa tutaanza kutumia toleo hili la mfumo unaotumia lugha mbili kwa maana ya Kiswahili na Kiingereza hapo awali tulikuwa tukitumia mfumo wa kiingereza pekee”, alisema Mhe. Dkt. Ndika

Mhe. Dkt. Ndika aliongeza kuwa, mfumo huo sasa unamuonekano wa kuvutia sana, unaweza pia kupatikana kupitia simu janja ya kiganjani tofauti na ule mfumo ulipita ilikuwa sio rahisi kwa watumiaji kutumia kupitia simu ya mkononi.

“Mfumo huu mpya ni rafiki kwa mtumiaji unatoa fursa kwa mtu yeyote kuyafikia maamuzi ya kimahakama kwa njia nyepesi na unatoa matokeo sahihi zaidi kwa mtumiaji yaani mtafiti anayetafuta taarifa fulani za kimaamuzi ama kisheria, unatoa matokea sahihi na kwa haraka binafsi nimeshautumia”, alifafanua Jaji Dkt. Ndika.

Jaji Dkt. Ndika alitanabaisha kuwa, mfumo huo unasifa ya kipekee, unatumia kiungo maalum “hyperlink” unayomwezesha mtafiti kufanya kazi kutoka dirisha moja hadi jingine wakati wa utafiti kwa njia rahisi zaidi. Tofauti na mfumo uliopita haukuwa na kiunganishi hicho.

“Kupitia mfumo huu mpya utasaidia kutunganisha na kuboresha mahusiano ya Mahakama za kikanda kama vile Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariaki na Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kwenye eneo la maamuzi na sheria mbalimbali zilizotungwa”, aliongeza Mhe. Dkt. Ndika

Aidha, mfumo huo hautaishia kwa wataalum wa sheria na watafiti bali unalenga hasa kumnufaisha mwananchi wa kawaidi ambaye atataka kupata nakala ya maamuzi ama sheria iliyokwisha pakiwa kwenye mfumo huo bila kutumia gharama, muda na kumuondolea usumbufu.

Awali, akisoma histori fupi ya maendeleo ya matumizi ya mfumo wa TanzLII kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza alisema, ushirikianao na mahusiano mema baina ya Mahakama ya Tanzania na Chuo Kikuu cha Cape Town Afrika ya Kusini yamekuwa na tija kwa kuimarisha matumizi ya mfumo huo wa kutunza maamuzi ya kimahakama TanzLII na kutengeneza namna bora ya ufikiaji na upatikanaji bure wa Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania kwa njia ya Mtandao.

Mhe. Kahyoza alisema kuwa, kwa kipindi chote Mahakama imeendelea kuchukua utaalam na uzoefu wa namna bora ya kuendesha na kuratibu maendeleo endelevu ya mfumo wa TanzLII hadi sasa unapoziduliwa mfumo huo wa toleo la tatu.

“Natambua jitihada za wadau wote SafLII, AfricnLII, Chuo Kikuu cha Cape Town Afrika ya Kusini na Mahakama ya Tanzania licha ya changamoto tumeendelea kushirikiana na tumeweza kuimarisha mfumo huu wa kutunza maamuzi yaani TanzLII”, alisema Jaji Kahyoza

Mhe. Kahyoza aliondeza kuwa, mfumo huo unawawezesha Majaji, Mahakimu, wanafunzi wa sheria wanataaluma ya sheria, mawakili na wananchi wa kawaida ufikiaji na upatikanaji bure wa maamuzi, sheria na kanuni za Tanzania kwa njia ya mtandao na kuifanya kuwa njia ya ufuatiliaji na usimamizi kwa viongozi wa Mahakama na uora wa mfumo umethibitisha kuwa kiungo muhimu kwa utawala wa sheria nchini.

Sambamba na uzinduzi wa mfumo TanzLII, Mahakama ya Tanzania imeingia makubaliano ya ushirikiano na Chuo Kikuu cha Cape Town Afrika ya Kusini wenye lengo kuendeleza juhudi za kuboresha mfumo maalumu wa kutunza maamuzi ya kimahakama TanzLII na kutengeneza namna bora ya ufikiaji na upatikanaji bure wa Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania kwa njia ya Mtandao “TanzLII - Access Court Decisions and Laws of Tanzania for Free”.

Makubaliano hayo yamesainiwa jana tarehe 29 Mei, 2023 Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Temeke jijini Dar es salaam kati ya Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Martin Chuma kwa upande wa Mahakama ya Tanzania pamoja na Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva. Huku utiwaji saini huo ukishudiwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Gerald Ndika.

Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Gerald Ndika, jana tarehe 29 Mei, 2029 amezindua toleo la tatu la tovuti mpya ya mfumo wa kutunza maamuzi ya kimahakama wenye lengo la kuboresha ufikiaji na upatikanaji bure wa Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania kwa njia ya Mtandao “TanzLII - Access Court Decisions and Laws of Tanzania for Free”,  katika hafla iliyofanyika Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Temeke jijini Dar es salaam. 


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara na Championi wa mfumo wa TanzLII Mhe. John Kahyoza (wa kwanza kulia) akitoa historia fupi ya mfumo huo wakati wa uzinduzi wa toleo la Tatu la mfumo huo, kushoto ni Kaimu Mkuu wa huduma za Maktaba ya Tanzania, Mhe. Kifungu Mrisho.


Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na wa Mahakama Kuu (walioketi mstari wa mbele) waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa tovuti ya kutunza maamuzi TanzLII toleo la Tatu sambamba na utiaji saini makubaliano ya ushirikiano wa lengo la kuboresha ufikiaji na upatikanaji bure wa Maamuzi, Sheria na Kanuni za Tanzania kwa njia ya Mtandao “TanzLII - Access Court Decisions and Laws of Tanzania for Free”, wakimsikiliza Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (hayupo pichani) akitoa historia fupi ya mchakato wa uanzishwaji wa mfumo wa kutunza maamuzi TanzLII wakati wa hafla hiyo.


Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Gerald Ndika (wa nne kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Majaji walishiriki hafla hiyo, wengine ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe. Jacobs Mwambegele (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma Mhe. Dkt. Adam Mambi (wa tatu kulia), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (wa kwanza kulia), Kaimu Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Temeke (IJC) Mhe. Asina Omari (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa Mhe. Said Kalunde (wa kwanza skushoto) pamoja na Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva (wa nne kushoto) akiwa na Meneja Mradi wa sheria Africa Bi. Morina Chindia (wa tatu kushoto).
 
Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Gerald Ndika (wa sita kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya machampioni wa mfumo wa kutunza maamuzi ya kimahaka TanzLII wengine katika picho hiyo ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Martin Chuma (wa tano kulia) na Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva (wa saba kushoto)   walishiriki hafla hiyo.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Martin Chuma (kulia)kwa upande wa Mahakama ya Tanzania akitia saini makubaliano ya ushirikiano ya kuimarisha mfumo wa kutunza maamuzi ya kimahakama pamoja na Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva (kushoto). Huku utiwaji saini huo ukishudiwa na  Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Gerald Ndika, jana tarehe 29 Mei, 2029 katika hafla iliyofanyika Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Temeke jijini Dar es salaam. 


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Martin Chuma (kulia) na Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva (kushoto) kutoka Chuo Kikuu cha Cape Town Afrika ya kusini, akionyesha hati zililzosainiwa za kukubali mashirikiano hayo.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Martin Chuma (kulia) akibalisha hati za makubaliano mara baada ya kutia saini na Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva (kushoto) kutoka Chuo Kikuu cha Cape Town Afrika ya kusini, nyuma yao ni Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Kamishina wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt. Gerald Ndika aliyeshuhudia utiaji wa saini makubaliano hayo.


Mkurugenzi wa AfricanLII Bi. Mariya Badeva ( kushoto) akiwa na Meneja Mradi wa sheria Africa Bi. Morina Chindia (Kulia) wakifuatilia shughuli hiyo.

(Picha na Innocent Kansha-Mahakama)
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni