Jumanne, 2 Mei 2023

MAHAKAMA GEITA YAADHIMISHA MEI MOSI KWA KUTOA MSAADA KWA WAGONJWA.

Na Charles Ngusa - Mahakama Geita.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita na Wilaya zake wameshiriki maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani kwa kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo kutoa misaada kwa wodi ya watoto wenye changamoto ya ugojwa wa utapiamlo kwa kutoa sukari, mafuta ya kula na kupikia, maziwa ya unga pamoja na sabuni ikawa ni mchango wao kwa jamii wanayoihudumia.

Wakiungana na taasisi nyingine za kiserikali na binafsi mkoani Geita kuadhimisha kilele cha siku hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Chama cha Mapinduzi-Kalangalala jana tarehe mosi Mei, 2023 Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya zake ikiwemo Geita, Chato, Bukombe, Mbogwe na Nyangh’wale wote walijumuika pamoja.

Akizungumza kwa niaba ya Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita, Muuguzi Kiongozi katika wodi ya watoto wenye utapiamlo Bi. Generoza Wanna alisema, changamoto hii kwa kiasi kikubwa inatokana na ukosefu wa elimu kwa wazazi ya namna nzuri ya kotoa lishe bora kwa watoto jambo ambalo hupelekea watoto walio wengi kupewa chakula cha aina moja tu.

“Nawashukuru watumishi wa Mahakama kwa kuwakumbuka watoto hao, kwani wadau walio wengi wamekuwa wakiwakumbuka wahitaji wengine bila kuwakumbuka hawa watoto wenye utapiamlo na kwamba mahitaji yao yamekuwa na gharama kubwa sana, ndiyo maana matibabu haya hutolewa bure kwani ni vigumu kwa raia wa kawaida kuyamudu hivyo anawashukuru kwa upendo wenu mkuu’’, Muuguzi Wanna.

Naye, mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Martin Shigela akitoa hotuba yake kwa wafanyakazi, amesisitiza suala la mahusiano kazini (socialization) baina ya waajiri na wafanyakazi kwani inasaidia kujenga mahusianao mema miongoni mwao.

Mhe. Shigela akaongeza kuwa, uboreshaji wa mishahara unapaswa kuendana na uzalishaji katika taasisi husika kama ilivyo kwa serikali ukuaji wa uchumi unaoendana na uzalishaji mali ndiyo tija ya uboreshaji wa maslahi ya wafanyakazi ikiwemo mishahara yao.  

Kadhalika, Mkuu wa Mkoa huyo, amewashauri waajiri kujenga utamaduni wa kubaini na kuzitambau changamoto zinazowakabili wafanyakazi ikiwemo kuwatembelea na kufahamu maeneo wanayofanyia kazi, vilevile uchumi na bajeti zenu zinaporuhusu muwawezeshe wafanyakazi wenu motisha kama vile usafiri na makazi bora.

Aidha, akisoma risala ya wafanyakazi wa Mkoa wa Geita kwa niaba ya vyama vya wafanyakazi wote, katibu wa TAMICO Mkoa wa Geita Bw. Obedi Mwakapango alisema kuwa, lazima Serikali ijikite katika kuimarisha fursa za ajira ambazo ni za kujiajiri na kuajiriwa lakini pia ziwe za staha kwa sekta zote.

Katibu huyo, aliendelea kwa kuwakumbusha waajiri wazingatie haki na maslahi ya wafanyakazi wote ikiwemo mishahara bora yenye kuendana na nguvu ambazo wafanyakazi wanazitoa pamoja na kuzingatia upandishwaji wa madaraja kwa watumishi wenye sifa. Sambamba na hilo watumishi pia wameiomba serikali kuangalia upya suala la kikokotoo kwani linaonekana kuwa kandamizi kwa wafanyakazi.

Kwa upande wao watumishi wa Mahakama hawakubaki nyuma katika kuzungumzia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Mahakamani. Katika maandamano hayo watumishi hao walishika bango lenye ujumbe uliosomeka,MAHAKAMA SASA INAFIKIKA KWA URAHISI KUPITIA TEHAMA”.

ujumbe huo ulilenga kutoa elimu na kuwakumbusha wadau umuhimu wa matumizi ya TEHAMA Mahakamani kama njia rahisi ya kupata huduma za kimahakama tofauti na ilivyokuwa hapo awali ambapo wadau walipaswa kufika Mahakamani ili kuweza kupata huduma zitolewazo. tofauti na sasa mteja anaweza kupata huduma ya Kimahakama bila kulazimika kufika Mahakamani mfano, kujua tarehe ya shauri, kufungua shauri na kusikiliza shauri kwa njia ya mtandao na huduma nyingine lukuki.

Watumishi wa Mahakama Mkoa wa Geita wakiwa kwenye matembezi ya kuadhimisha siku ya wafanyakazi Dunia wakiwa wamebebe Bango lenye ujumbe unaosomeka Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Mahakamani. MAHAKAMA SASA INAFIKIKA KWA URAHISI KUPITIA TEHAMA.

Sehemu ya Watumishi  wa Mahakama mkoani Geita wakiwasili katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita kuwasilisha ukarimu wao katika wodi ya watoto wenye utapiamlo.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama mkoani Geita wakiwa kwenye picha ya pamoja wakijiandaa kuanza maandamano kuelekea katika viwanja vya CCM-Kalangalala kushiriki maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Duniani.



Mgeni rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Martin Shigela akitoa hotuba wakati wa maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Dunia, yaliyofanyika kimkoa katika viwanja vya CCM - Kalangalala-Geita Mjini.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni