Jumatano, 3 Mei 2023

ZIARA ZA JAJI MFAWIDHI DIVISHENI YA KAZI ZAANZA KULIPA

·Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi watoa vitabu kuimarisha Maktaba

Na Faustine Kapama na Mwanaidi Msekwa-Mahakama Kuu, Kazi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina leo tarehe 3 Mei, 2023 amepokea vitabu vyenye muunganiko wa sheria kutoka ofisi za Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa ajili ya kuimarisha tovuti ya Divisheni hiyo na Maktaba Mtandao ya Mahakama ya Tanzania.

Tukio la kupokea vitabu hivyo limeshuhudhiwa na Majaji wengine katika Divisheni hiyo, Mhe. Katarina Mteule, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu na Mhe. Biswalo Mganga, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kuratibu Masuala ya Tovuti, Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Said Ding’ohi, Naibu Msajili, Mhe. Enock Kassian, Mtendaji, Bw. Samson Mashalla na watumishi wengine.

Vitabu hivyo vimekabidhiwa na Afisa Sheria Mwandamizi wa WCF, Bw. Deo Victor ikiwa ni siku chache tangu Jaji Mfawidhi alipomtembelea Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo, Dkt. John Mduma ofisini kwake Kijitonyama Mkoa wa Dar es Salaam kwa ajili ya kujitambulisha na kubadilishana uzoefu.

Akiongea baada ya kukabidhiwa vitabu hivyo, Mhe. Dkt. Mlyambina amewashukuru WCF kwa mchango wao huo ambao hautatumiwa na Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi pekee bali pia Mahakama ya Tanzania kwa ujumla pamoja na wadau wake.

“Nakala hizi zitaingizwa kwenye tovuti ya Divisheni yetu na Maktaba Mtandao ya Mahakama ili kuwezesha watu wengi zaidi, hata katika Mahakama Kuu, Kanda zote nchini ambao wanashughulikia migogoro ya kazi, kuzitumia kupitia Maktaba Mtandao (e-Library),” amesema.

Aidha, Jaji Mfawidhi amemshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na uongozi wote wa Mahakama kwa kutekeleza Mpango Mkakati wa Mahakama (2021 – 2025) hususani nguzo ya tatu katika kushirikiana na wadau kufanikisha utoaji wa haki.

“Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi ni miongoni mwa wadau wetu, kinachofanyika hapa leo na matokeo ya upatikanaji wa sheria hizi tulizopewa vina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Mpango Mkakati huo, hususani katika nguzo ya Pili ambayo inahimiza upatikanaji wa haki kwa wakati,” amesema.

Mhe. Dkt. Mlyambina amesema kuwa WCF kama wadau wameonyesha utayari wa kushirikiana na Mahakama katika mambo mengi, ikiwemo kudhamini na kutoa  elimu juu ya sheria na shughuli zao zenye uhusiano na migogoro ya kazi, ununuzi wa vifaa vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya Maktaba kama vile Komputa na vifaa vingine vya kielectroniki.

Amemshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa WCF na Menejimenti yote kwa majitoleo hayo ambayo yatakuwa na faida kubwa kwa Mahakama katika kusimamia haki kazi. Jaji Mfawidhi amewaomba kuendelea kufanya hivyo ili Masjala zote za Mahakama Kuu na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi waweze kupata nakala za sheria hizo.

Akipokea shukrani hizo, Afisa Sheria Mwandamizi wa WCF alimshukuru Jaji Mfawidhi kwa uamuzi wake wa kuwatembelea. Amesema ndani ya muda mfupi ujao watatoa mafunzo kwa watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na baadhi ya wadau kuhusu sheria na masuala mbalimbali yanayohusu fidia kwa wafanyakazi.

Bw. Victor amesema hatua hiyo itawawezesha watumishi hao kuwa na wigo mpana wa uelewa wa sheria hizo na utekelezaji wake katika utatuzi wa migogoro ya kikazi inayoletwa mbele  yao.

Kadhalika ameahidi kutoa nakala za vitabu hivyo vya kutosha kwa Majaji wote wa Kanda za Mahakama Kuu ya Tanzania nchi nzima ambao wanashughulika na utatuzi wa migogoro ya kazi.

Wakati huo huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina leo tarehe 3 Mei, 2023 ametembelewa ofisini kwake na Wakili Msomi Isaack Zake na kufanya naye mazungumzo mafupi.

Katika mazungumzo yao, Wakili Zake kutoka Kampuni ya Uwakili ya Zake Advocates ameahidi kutoa vitabu 150 vyenye maudhui ya kisheria vitakavyosaidia Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu kuamua mashauri mbalimbali ya kazi yanayoletwa mbele yao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (juu na chini) akipokea vitabu kutoka kwa Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor katika hafla iliyofanyika leo tarehe 3 Mei, 2023 katika ukumbi wa Mahakama hiyo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akizungumza na watumishi wakati wa hafla hiyo.
Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor akizungumza baada ya kukabidhi vitabu hivyo.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi wakiwa katika hafla ya kukabidhi vitabu hivyo.
Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Said Ding’ohi (katikati) na Naibu Msajili kutoka Divisheni hiyo, Mhe. Enock Kassian (kushoto), wakipokea vitabu kutoka kwa Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (kulia) akisalimiana na Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor alipowasili ofisini kwake.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) akizungumza na Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor (kulia) na Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Said Ding’ohi (kushoto).
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na mgeni wake, Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor (wa tatu kulia) na viongozi wakuu wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na mgeni wake, Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor (wa nne kulia), viongozi wakuu wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na Makatibu wa Kamati ya Elimu ya Ndani, Mhe. Jane Masua (wa kwanza kulia) na Bi Jane Nyange (wa pili kushoto).
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati). Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu  ya Tanzania, Mhe. Katarina Mteule, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Biswalo Mganga, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kuratibu Masuala ya Tovuti (wa kwanza kushoto, Afisa Sheria Mwandamizi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Deo Victor (wa pili kulia) na Katibu wa Kamati ya Elimu, Mhe. Jane Masua (wa kwanza kulia).

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na wadau waliohudhuria makabidhiano ya vitabu hivyo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na maafisa Teknolojia Habari na Mawasiliano (TEHAMA).
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi (juu na chini).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (kushoto) akipokea sehemu ya vitabu vyenye maudhui ya kisheria ambayo Wakili Msomi Isaack Zake ameahidi kutoa kwa ajili ya Majaji wote wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni