Jumatano, 31 Mei 2023

MAJAJI MBEYA WAJITOSA KWENYE MAZOEZI

Na Mwinga Mpoli- Mahakama Kuu, Mbeya

Mahakama Mkoa wa Mbeya imezindua programu maalum itakayowashirikisha watumishi wa kada zote, wakiwemo Majaji kushiriki katika mazoezi ya viungo ili kujenga afya bora na ushupavu, hatua itakayosaidia kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Programu hiyo ilizinduliwa hivi karibuni ambapo Majaji, viongozi waamdamizi na watumshi kwa ujumla walishiriki kwenye mazoezi ya michezo mbalimbali, ikiwemo kukimbia, mpira wa miguu na mpira wa pete.

Akizungumza katika ufunguzi wa mazoezi hayo, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. James Karayemaha aliwapongeza watumishi kwa kushiriki kwa wingi kwani mazoezi ni afya.

“Kwa hakika, mazoezi ni afya na hii inaongeza ari na nguvu hata katika utendaji wetu wa kazi, hivyo kutufanya tuweze kuepuka magonjwa yasiyo ya kuambukiza,” alisisitiza Mhe. Karayemaha.

Naye Mtendaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Bw. Teoford Ndomba alisema atahakikisha vifaa vyote vinavyohitajika vinapatikana kwa wakati ili kuwapa watumishi nguvu ya mazoezi. Alisema atahakikisha  mwalimu wa mazoezi anapatikana.

Kwa upande wao, watumishi wa Mahakama walionyesha kufurahia programu hiyo ya mazoezi na kuahidi kushiriki bila kukosa kwa kuzingatia ratiba endelevu itakayotolewa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda Mbeya, Mhe. Dastan Ndunguru akiongoza mazoezi.
Sehemu ya watumishi wa Mahakama katika mazoezi wakiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa (kushoto) wakishiriki kwenye mazoezi. Katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu katika Kanda hiyo, Mhe. David Ngunyale.
Watumishi (juu na chini) wakiwa katika mazoezi.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni