Jumanne, 23 Mei 2023

RAIS SAMIA KUONGEZA JOPO LINGINE LA MAJAJI WA MAHAKAMA WA RUFANI

Na Tiganya Vincent-Mahakama, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameahidi kuongeza jopo jingine la Majaji wa Mahakama ya Rufaa ili kuendelea kupunguza mrundikano wa mashauri.

Ametoa kauli hiyo leo tarehe 23 Mei 2023 wakati wa hafla fupi ya kuwaapisha Majaji sita wa Mahakama ya Rufani iliyofanyika Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma kufuatia uteuzi alioufanya hivi karibuni.

Mhe. Dkt.Samia alisema lengo ni kufikisha Majopo ya Majaji wa Mahakama ya Rufani 10 badala ya tisa (9), hatua hiyo itasaidia kuharikisha utoaji haki kwa wananchi katika ngazi ya Mahakama ya Rufani.

"Napenda kukupongeze Jaji Mkuu wa Tanzania kwa kupata timu mpya ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na kila nitakapokuwa nikiteua nitaongeza idadi ya wanawake ili kufikia wastani wa hamsini kwa hamsini," alisisitiza.

Aliongeza kuwa sanjari ya kuongeza Jopo la Majaji wa Mahakama ya Rufani pia ataongeza Majaji wa Mahakama Kuu wapya kwa lengo la kuhakikisha utoaji wa haki kwa wananchi unafanyika kwa wakati.

Naye Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alisema uteuzi na uapisho alioufanya Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan umeweka historia kwa ongezeko la idadi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani.

Alisema kuwa kabla ya Rais Samia kuingia madarakani, Majaji wa Rufani walikuwa hawazidi 16 na alipoingia aliongeza na kufikia 25 na uapisho mpya umefanya wafikie Majaji wa 31 hapa nchini.

Mhe. Prof. Juma alisema hatua hiyo umesaidia Mahakama ya Rufani kuongeza Majopo ya Majaji wa Mahakama ya Rufani kutoka saba hadi kufikisha Majopo tisa ambapo kwa wastani kila Jopo hukaa Majaji watatu, au watano, au saba kutokana  na shauri husika linalosikilizwa.

Alisema faida ambayo Mahakama imeipata kutokana na uteuzi huo ni kupungua kwa mzigo wa mashauri ambao kila jopo lilikuwa likiubeba ambapo kwa wastani yalikuwa mashauri 805 na sasa yatafikia 626.

Aidha, Jaji Mkuu aliwataka Majaji kubadili mtazamo ikiwemo kuangalia matumizi ya usuluhushi kwa baadhi ya mashauri, ikiwemo ya biashara. Amesema hatua hiyo itapunguza mrundiko wa mashauri ambayo yangeweza kumalizika kwa mazungumzo.

Naye Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson alisema wako tayari kufanya marekebisho kwenye maeneo ambayo ni kikwazo katika utoaji wa haki ili wananchi wapate haki kwa wakati.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (juu na chini) akisisitiza jambo alipokuwa anazungumza baada ya kuwaapisha Majaji wapya sita wa Mahakama ya Rufani Ikulu Chamwino Jijini Dodoma leo tarehe 23 Mei, 2023.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim Majaliwa akitoa salamu katika hafla hiyo.
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Tulia Ackson akieleza jambo.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisisitiza jambo alipokuwa anazungumza kwenye hafla ya uapisho huo.
Sehemu ya viongozi wa Mahakama (juu na chini) waliohudhuria uapisho huo.

Ndugu na jamaa wakifuatilia matukio mbalimbali.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (wa tano kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya, viongozi wa Mahakama, ndugu na jamaa baada ya uapisho huo (picha juu na chini).
Picha na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni