Jumatano, 24 Mei 2023

SHIRIKA LA UMOJA WA MATAIFA LAENDESHA MAFUNZO KUHUSU SHERIA YA BAHARI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama

Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuzuia Dawa za Kulevya na Uhalifu ((UNODC) linaendesha mafunzo maalum kwa watumishi wa Mahakaka ya Tanzania, hususan Majaji na Mahakimu kuwaongezea uelewa kuhusu Sheria ya Bahari na Hukumu.

Mafunzo hayo ya siku tano ambayo yanafanyika katika Hoteli ya Protea Mkoa wa Dar es Salaam yalifunguliwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo.

Akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo, Mhe. Dkt. Opiyo alitoa shukrani zake za dhati kea UNDC kwa msaada wao kufanikisha mafunzo hayo.

“Natambua juhudi kubwa za Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Jaji Dkt. Paul Kihwelo, ambaye ameiongoza timu ya Chuo hicho katika kuandaa mafunzo haya. Kujitolea kwake na utaalamu wake umekuwa muhimu, tunashukuru sana kwa michango yake, "alisema.

Jaji huyo alieleza pia kuwa wamekuwa na bahati ya kuwa na Jaji Maurice Kamga, Jaji wa Mahakama ya Kimataifa ya Sheria ya Bahari, ambaye amekuwa mwanachama mashuhuri wa Mahakama hiyo tangu tarehe 1 Oktoba, 2020.

 “Uwepo wake hapa unasisitiza umuhimu wa mafunzo haya na umuhimu wa masuala tutakayojadili. Tuna hamu ya kujifunza kutokana na ujuzi na uzoefu wake mkubwa katika nyanja hiyo,” alisema.

Jaji Opiyo alibainisha kuwa katika mtazamo wa Tanzania, Sheria ya Bahari inahusu mfumo wa kisheria unaosimamia haki na wajibu wa nchi katika matumizi na usimamizi wa bahari ya dunia na rasilimali zake.

Alisema Tanzania, ikiwa ni nchi ya pwani  inafungwa na Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Sheria ya Bahari (UNCLOS), ambao ni makubaliano ya msingi ya kimataifa yanayosimamia masuala ya bahari.

Tanzania, kama mataifa mengine ya pwani, ina haki na mamlaka fulani juu ya eneo lake la maji, ambayo yanaenea hadi maili 12 kutoka kwa msingi wake. Ndani ya ukanda huu, Tanzania ina mamlaka kamili, ikiwa ni pamoja na haki ya kudhibiti na kunyonya rasilimali zilizo hai na zisizo hai.

Jaji Opiyo alisema pia kuwa zaidi ya eneo lake la maji, Tanzania ina eneo la kipekee la kiuchumi (EEZ) ambalo linaenea hadi maili 200 kutoka katika msingi wake.

"Katika EEZ, Tanzania ina haki huru ya kuchunguza, kunyonya, kuhifadhi na kusimamia maliasili, hai na isiyo hai, katika safu ya maji na juu au chini ya bahari," alisema.

Jaji Opiyo alieleza zaidi kuwa Tanzania pia inastahili kupata haki katika upanuzi wa chini ya maji wa ardhi yake. Alisema kuwa eneo hilo linaenea zaidi ya EEZ katika hali fulani, kwa kuzingatia jiolojia ya bahari.

“Tanzania, kama mshirika wa UNCLOS, inatekeleza kanuni za ulinzi wa mazingira ya baharini, usimamizi endelevu wa uvuvi na uhifadhi wa viumbe hai vya baharini. Nchi ina jukumu la kuzuia na kudhibiti uchafuzi wa mazingira katika maji yake, "alisema.

Jaji Opiyo pia alieleza kuwa Tanzania ikiwa ni nchi ya mwambao wa Afrika Mashariki, inakabiliwa na matukio ya uhalifu mbalimbali wa baharini, ukiwemo uharamia, uvuvi haramu, biashara ya dawa za kulevya, biashara haramu ya binadamu na biashara haramu.

"Ni muhimu kutambua kwamba Tanzania, kama nchi nyingine nyingi, inachukulia kwa uzito uhalifu huu wa baharini na inashirikiana na washirika wa kimataifa, kama vile mashirika ya kikanda, nchi jirani, na vyombo vya sheria vya kimataifa, kupambana na vitendo hivi haramu na kudumisha usalama wa baharini." alisema.

Hii ni mara ya pili chini ya mradi wa Global Maritime Crime Programme (GMCP), kwa Shirika hilo kufadhili mafunzo ya aina hiyo kwa Majaji na Mahakimu wa Tanzania.

  Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo (kulia) akiwa na  Jaji wa Mahakama ya Kimataifa ya Sheria ya Bahari, Mhe. Maurice Kamga.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania (wa kwanza hadi wa tatu kutoka kushoto) wanaohudhuria mafunzo hayo.

Mchanganyiko wa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakimu wanaohudhuria mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja. Katikati ni Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo. Kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na  kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Kimataifa ya Sheria ya Bahari, Mhe. Maurice Kamga.


Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Majaji wanaohudhuria mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu wanaohudhuria mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wote wa mafunzo hayo.
Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na sekretarieti inayoratibu mafunzo hayo.



















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni