Alhamisi, 4 Mei 2023

SHIRIKA LA KAZI DUNIANI, MAHAKAMA KUU KAZI MAMBO SAFI

·Mwakilishi atua mahakamani na mzigo wa vitabu vya sheria

Na Faustine Kapama-Mahakama, Dar es Salaam

Mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) na Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi jana terehe 3 Mei, 2023 yameendelea kujidhihirisha baada ya mwakilishi kutoka shirika hilo kukabidhi vitabu kwa ajili ya kuimarisha tovuti ya Divisheni hiyo na Maktaba ya Mahakama ya Tanzania.

Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano na Usimamizi wa Habari wa ILO Ofisi ya Dar es Salaam, Bi. Nasikiwa Berya, akiwa na makasha ya vitabu hivyo aliwasili mahakamani hapo saa saba mchana na kupokelewa na mwenyeji wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina.

Mara baada ya kutia sahihi kwenye kitabu cha wageni, Mhe. Dkt. Mlyambina aliongozana na mgeni wake kwenye ukumbi uliokuwa umeandaliwa kwa ajili ya makabidhiano ya vitabu hivyo, tukio lililoshuhudiwa na Majaji wote wa Divisheni, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo, Mhe. Katarina Mteule na Mhe. Biswalo Mganga.

Wengine waliohudhuria tukio hilo ni Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Said Ding’ohi, Naibu Msajili, Mhe. Enock Cassian, Mtendaji, Bw. Samson Mashalla, watumishi kutoka Divisheni hiyo wakiwemo viongozi wa Kamati ya Elimu ya Ndani na mwakilishi kutoka Maktaba ya Mahakama, Bw Salum Tawani.

Akizungumza baada ya makabidhiano hayo, Mhe. Dkt. Mlyambina alisema kuwa tukio hilo ni hatua muhimu katika kutafuta haki ndani ya maeneo yao na kulipongeza Shirika hilo kwa msaada huo waliotoa na kujitolea kwa ajili ya kuendeleza hitaji la kazi zenye staha na haki ya kijamii duniani kote.

"Kujitolea kwa ILO katika kuimalisha viwango vya kazi na kukuza haki na usawa za ajira kumeleta mafanikio makubwa kwenye maisha ya wafanyikazi kote ulimwenguni na maendeleo ya jamii yenye utaratibu. Tunashukuru sana kwa ushirikiano na usaidizi wao katika kuimarisha uwezo wa Mahakama yetu ya Kazi,” alisema.

Jaji Mfawidhi alieleza kuwa mchango huo wa vitabu unawakilisha utajiri wa maarifa na ujuzi katika uwanja wa sheria za kazi. Alisema vitabu hivyo vitatumika kama nyenzo muhimu kwa Majaji, Wasaidizi wa Kisheria wa Majaji, Wataalamu wa Sheria na Watumishi wa Mahakama ili kuwawezesha kuongeza uelewa wao wa sheria za kazi, viwango vya kimataifa vya kazi na sheria za kesi husika.

"Hii bila shaka itachangia katika utoaji wa haki kwa ufanisi katika Divisheni yetu ya Kazi. Vitabu hivi vitachangia jukumu muhimu katika kujenga uwezo na ukuzaji wa taaluma ndani ya mfumo wa Mahakama. Kwa kupanua upatikanaji wetu wa fasihi ya kisheria, ILO imetuwezesha kukuza utamaduni wa kuendelea kujifunza na kuimarisha ujuzi,” alisema.

Alieleza pia kuwa kitendo cha Shirika hilo kuiwezesha Mahakama ya Kazi rasilimali zinazohitajika kunasisitiza umuhimu wa sheria za kazi kama njia ya kulinda haki za wafanyakazi, kukuza uhusiano mzuri na kuchangia maendeleo ya taifa.

Hivyo, alitoa shukurani zake za dhati kwa watumishi katika Shirika hilo waliojitolea na kufanya kazi bila kuchoka ili kufanikisha mchango huo, akiwemo Mkurugenzi wa ILO wa Afrika Mashariki, Ofisi ya Dar es Salaam anayemaliza muda wake, Mhe. Wellingston Chibebe.

Naye Bi. Berya, akizungumza baada ya kukabidhi vitabu hivyo, alishukuru uongozi kwa kuendelea kuimarisha mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Mahakama hiyo na ILO na kuahidi kuendeleza ushirikiano kati ya pande zote mbili.

Tukio la kukabidhi vitabu hivyo limekuja muda mchache baada ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kukabidhi vitabu vingine vinavyohusu sheria za kazi na fidia katika Divisheni hiyo.

Matukio hayo yote mawili ni matunda yanayotokana na ziara alizozifanya hivi karibuni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina kwenye taasisi hizo ili kuendeleza uhusiano na kubadilishana uzoefu namna ya kutua migogoro ya kazi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina.(kushoto) akimkaribisha ofisini kwake Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano na Usimamizi wa Habari wa ILO Ofisi ya Dar es Salaam, Bi. Nasikiwa Berya baada ya kuwasili katika Mahakama hiyo jana terehe 3 Mei, 2023 kukabidhi vitabu mbalimbali vya masuala ya sheria za kazi.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina.(katikati) akiwa na mgeni wake, Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano na Usimamizi wa Habari wa ILO Ofisi ya Dar es Salaam, Bi. Nasikiwa Berya. Kushoto ni Mtendaji wa Mahakama hiyo, Bw. Samson Mashalla.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina.(kushoto) akipokea moja ya vitabu kutoka kwa Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano na Usimamizi wa Habari wa ILO Ofisi ya Dar es Salaam, Bi. Nasikiwa Berya. Picha chini, Bi. Berya akikabidhi aina nyingine za vitabu hivyo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina.(juu na chini) akiongea na watumishi baada ya makabidhiano ya vitabu hivyo.



Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano na Usimamizi wa Habari wa ILO Ofisi ya Dar es Salaam, Bi. Nasikiwa Berya akizungumza baada ya kukabidhi vitabu hivyo.


Majaji wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi wakishuhudia makabidhiano ya vitabu hivyo. Kutoka kulia ni  Mhe. Dkt. Modesta Opiyo, Mhe. Katarina Mteule na Mhe. Biswalo Mganga.

Viongozi wengine wa Mahakama wakifuatilia mambo mbalimbali ya tukio la kukabidhi vitabu. Kutoka kushoto kwa mgeni wa ILO ni Naibu Msajili Mfawidhi, Mhe. Said Ding’ohi, Naibu Msajili, Mhe. Enock Cassian, Mtendaji, Bw. Samson Mashalla.

Watumishi wa Mahakama (juu na chini) wakifuatilia makabidhiano ya vitabu hivyo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati). Wengine ni Majaji wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo (wa pili kushoto), Mhe. Katarina Mteule (wa kwanza kushoto) na Mhe. Biswalo Mganga (wa kwanza kulia). Kushoto kwa Jaji Mfawidhi ni Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano na Usimamizi wa Habari wa ILO Ofisi ya Dar es Salaam, Bi. Nasikiwa Berya.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi waliohudhuria makabidhiano ya vitabu hivyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni