Jumatatu, 1 Mei 2023

WATUMISHI MAHAKAMA DAR ES SALAAM WASHIRIKI MAADHIMISHO MEI MOSI 2023

Na Faustine Kapama-Mahakama, Dar es Salaam

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam, leo tarehe1Mei, 2023 wameungana na Watanzania wengine kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi, inayojulikana kama Mei Mosi, inayosherekewa kote duniani.

Maadhimisho hayo ambayo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Mwanahamisi Munkunda, yamefanyika katika Uwanja vya Uhuru katika Mkoa wa Dar es Salaam na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi.

Pilikapilika za maadhimisho hayo zilianza mapema asubuhi ambapo watumishi wa Mahakama waliojitokeza kwa wingi waliungana na wananchi wengine katika eneo la Mnazi Mmoja na baadaye kushiriki kwenye maandamano hadi kwenye Uwanja wa Uhuru.

Maandamano hayo yaliyoongozwa na Bendi ya Jeshi la Magereza yalipita katika barabara ya Nyerere, Keko na baadaye Uwanja wa Uhuru na kupokelewa na Mkuu wa Wilaya ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Amos Makala.

Mbali na watumishi kupita mbele ya mgeni rasmi kwenye maandamano hayo, magari ya Mahakama nayo yalikuwa miongoni mwa magari kutoka taasisi na mashirika mbalimbali ambayo yalipita mbele yake, likiwemo gari la Mahakama Inayotembea, ‘Mobile Court’, ambalo lilikuwa kivutio kikubwa kwa wananchi.

Baada ya maandamano hayo, ratiba ya maadhimisho hayo iliendelea, ikiwemo viongozi mbalimbali wa Chama cha Wafanyakazi (TUCTA) na Serikali ya Mkoa walipata nafasi ya kutoa salamu.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mhe. Munkunda amewapongeza wafanyakaizi wote kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye maadhimisho hayo ambayo kwa mwaka huu wa 2023 yamebeba kauli mbiu inayosema, “Mshahara Bora na Ajira za Staha ni Nguzo kwa Maendeleo ya Wafanyakazi, Wakati ni Sasa.”


 

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam (juu na chini) wakipita mbele ya jukwa kuu, likiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Mwanahamisi Munkunda katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, Mei Mosi, leo tarehe 1 Mei, 2023 kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Sehemu nyingine ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam (juu na picha mbili chini) ikipita mbele ya jukwa kuu, likiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Mwanahamisi Munkunda katika maadhimisho hayo.

Jukwa kuu, likiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Mwanahamisi Munkunda likiwapungia mkono watumishi wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam walipokuwa wanapita mbele yake katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ya Tanzania nao hawakubaki nyuma kushiriki kwenye maadhimisho hayo.

Sehemu ya magari ya  Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Dar-es-Salaam ikipita ndani ya  Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kwenye maadhimisho ya Mei Mosi. Chini ni mwonekano wa karibu wa Mahakama Inayotembea, ambayo ilikuwa kivutio kikubwa kwa wananchi walijitokeza kwa wingi.

Safari kuelekea katika maeneo ya Mnazi Mmoja ndiyo inaanza kushiriki katika maandamano ya kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani.
Sehemu ya magari ya  Mahakama ya Tanzania yakiwa yamefurika watumishi yakiwasili katika maeneo ya Mnazi Mmoja kabla ya kuanza maandamano hayo.
Maandamano yameanzia sasa.
Maandamano yamekolea....

Bendi ya Jeshi la Magereza ikiongoza maandamano hayo kukatisha mitaa mbalimbali hadi Uwanja wa Uhuru.

Wananchi wakiimba wimbo wa mshikamano katika Uwanja wa Uhuru baada ya maandamano.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni