Jumanne, 30 Mei 2023

WATUMISHI MAHAKAMA YA KAZI WAPATA ELIMU KUHUSU AFYA YA AKILI

Na Mwanaidi Msekwa-Mahakama Kazi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina hivi karibuni alishiriki katika zoezi la utoaji elimu kuhusu Afya ya Akili lililoongozwa na Msaikolojia kutoka Sally International Hospital, Bi. Eva Msaki.

Mafunzo hayo yalihudhuriwa na washiriki 32, wakiwemo Majaji, viongozi na watumishi wa Mahakama hiyo ambayo yalifanyika katika Ukumbi wa Mikutano. Bi Msaki alifafanua kwa kina maana ya afya ya akili, visababishi na sababu zinazopelekea mtu kupata ugonjwa wa akili.

Katika mada yake, Msaikolojia huyo aliweza kutaja tabia na mtindo wa maisha utakaomwezesha mtumishi kuepukana na ugonjwa huo, ikiwemo kuzingatia ulaji wa mlo kamili na kufanya mazoezi mara kwa mara. Pia alisisitiza kuwa mazingira na jamii inayomzunguka mtu ni kisababishi kikubwa cha kupata ugonjwa wa akili.

Vile vile, Bi. Msaki alieleza njia za kukabiliana na ugonjwa wa afya ya akili, huku aliruhusu watumishi kuuliza maswali mbalimbali ambayo yalijibiwa vema.

Akichangia mada hiyo, Mhe. Dkt. Mlyambina aliwaeleza watumishi kujitambua na kujua kwamba wote wana akili, hivyo inawapasa kujiamini katika kutekeza majukumu yao.

Akizungumza wakati wa kuahirisha mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Biswalo Mganga alimshukuru Bi. Msaki kwa kutoa mada hiyo nzuri na aliwasisitiza watumishi kufuatilia elimu hiyo.

Alimuomba Mtaalamu huyo kurudi tena na kutoa mada hiyo kwa undani ili kuwawezesha wafanyakazi kupata maarifa ya namna ya kuwahudumia wadau.

Utoaji wa elimu hiyo ni mwendelezo wa mafunzo yanayoendelea kutolewa kwa wadau na watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi yakisimamiwa na Kamati ya Elimu ya Ndani.

Katika hatua nyingine, aliyekuwa Mtendaji katika Divisheni hiyo, Bw. Samson Mashalla alitumia nafasi hiyo kuwaaga watumishi baada ya kuhamishiwa katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke. Amewashukuru watumishi hao kwa ushirikiano waliompa katika kipindi chote alipokuwa akihudumu kwenye Mahakama hiyo.

Msaikolojia kutoka Sally International Hospital, Bi. Eva Msaki (juu na chini) akitoa elimu ya afya ya akili.

Viongozi na watumishi wakifuatilia darasa.

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Biswalo Mganga (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na aliyekuwa Mtendaji wa Mahakama hivyo, Bw. Samson Mashalla (kulia), Bi Eva Msaki (kushoto) na watumishi wengine.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni