Alhamisi, 31 Agosti 2023

JAJI MZUNA, MAKANI WAAGWA KITAALUMA BAADA YA KUSTAAFU

·Waacha alama ya kutukuka mahakamani

·Kasi ya Jaji Makani kuamua mashauri mfano wa kuigwa

Na Faustine Kapama-Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani leo tarehe 31 Agosti, 2023 ameongoza Majaji na watumishi wa Mahakama kuwaaga kitaaluma Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Moses Mzuna na Mhe. Victoria Makani, ambao wamestaafu katika utumishi wa umma.

Hafla ya kuwaaga Majaji hao imefanyika kwenye ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama, wakiwemo Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni, Bi. Mary Shirima, Naibu Wasajili, Watendaji, ndugu na jamaa wa wastaafu hao.

Zoezi la kuwaaga viongozi hao lilianza kwa mashauri mawili Namba 2, 2023 na Namba 3, 2023 yaliyokuwa yanawahusu Mhe. Mzuna na Mhe. Makani, mtawalia, kuunganishwa pamoja kabla ya kuruhusu Mawakili kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) kuwasilisha hoja zao.

Akiwasilisha hoja zake, Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Bw. Camilius Ruhinda alieleza kuwa katika kipindi cha miaka 33 ambacho Jaji Mzuna amefanya kazi akiwa Hakimu, Msajili na baadae Jaji, aliweza kutoa maamuzi mbalimbali ambayo yamekuwa na mchango mkubwa katika jukumu la utoaji haki nchini.

“Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inatambua mchango mkubwa wa Mhe. Mzuna katika kutenda haki kupitia maisha yake ambayo yanadhihirika hususan katika hukumu mbalimbali alizowahi kutoa. Ni wazi kuwa hatuwezi kuandika mambo mengi kwa kuwa wasaa hautoshi; ila inatosha kusema kuwa tumefanya naye kazi na tutaendelea kuenzi maisha yake katika kutetea haki ambayo ni msingi mkuu katika utekelezaji wa sheria,” alisema.

Kwa upande wa Mhe. Makani, Wakili wa Serikali alisema kuwa katika utumishi wake akiwa Jaji aliweza kutoa maamuzi mbalimbali ambayo yalionyesha umuhimu wa kufuata sheria katika kutatua migogoro. Alisema kuwa maamuzi mengi aliyotoa yanahimiza kuwa makini katika kufuata utaratibu uliowekwa kisheria ili haki iweze kutendeka.

“Tunakupongeza kwa kusimamia sheria na kutoa maamuzi ambayo kwa nafasi kubwa tumeendelea kuyatumia katika mashauri mengine. Tutaendelea kujifunza kutoka kwako hususan usimamiaji wa sheria. Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inakutakia heri na baraka katika maisha yako,” alisema.

Makamu Rais wa TLS, Bi. Aisha Sinda, akiwasilisha hoja kwa niaba ya Rais wa Chama hicho, alieleza kuwa moja ya kigezo kikubwa katika upatikanaji wa haki ni uwepo wa watendaji mahiri katika Mahakama, hasa Majaji.

Alisema TLS inafarijika pale ambapo wanachama wao ambao pia ni maafisa wa Mahakama, wanapofanya kazi na Mhimili ambao unaundwa na watendaji waadilifu, wanaosimamia misingi ya haki pasipo kuyumbishwa na wenye kujali taratibu za kazi kama ilivyokua kwa Majaji Mzuna na Makani.

“Kwa niaba ya baraza la uongozi wa TLS tunawakaribisha sana Majaji hawa wastaafu tena katika chama chetu cha wanasheria, imekuwa ni kawaida sasa kwa Majaji wastaafu kurejea kufanya shughuli za uwakili. Tunapenda kuwafahamisha kuwa chama kitakuwa tayari kuwapa ushirikiano wa kutosha katika ngazi zote,” alisema.

Baada ya hoja hizo kuwasilishwa, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu, Mhe. Latifa Mansoor, alimwelezea Mhe. Mzuna kuwa amefanya kazi nzuri katika Mahakama ya Tanzania na kuchangia katika utawala wa haki kwa ujumla, hali ambayo ilijidhihirisha mara kadhaa wakati wa kuamua mashauri mbalimbali yaliyoletwa mbele yake.

Alieleza kuwa katika utawala wa haki, Jaji Mzuna alikuwa imara katika kusimamia sheria na haki ambapo haki ilionekana inatendeka ipasavyo kwa kuwa aliheshimu na kuzingatia misingi ya haki asilia.

Mhe. Mansoor alisema hukumu zilizotolewa na Jaji Mzuna ziliamuliwa bila upendeleo, zilizingatia hoja nzuri na msingi zilizopelekea mashauri kuamriwa kwa wakati na katika jukumu la kutenda haki alikuwa anajali makundi yenye mahitaji maalum, wakiwemo wajane.

“Tutamkumbuka sana  Jaji Mzuna kutokana  na mchango wake katika maisha ya kitaaluma na ya ushiriki wake katika kudumisha utamaduni wa  Mahakama ya Tanzania. Yeye ni mmoja wa waliojitoa  kwa kazi yao na kuhakikisha kuwa haki inatolewa kwa wakati,” alisema.

Naye Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda alimwelezea Jaji Makani kama mtumishi wa umma aliyetekeleza majukumu yake kikamilifu na kwa ufanisi mkubwa, ikiwemo kusikiliza mashauri na kutoa maamuzi kwa wakati.

Takwimu zinaonesha kwamba kwa kipindi chote cha kuanzia mwaka 2019 Mei hadi siku yake ya mwisho ya utumishi wa umma tarehe 4 Mei, 2023, ikiwa ni muda ambao alitumikia Divisheni ya Ardhi, Jaji Makani aliweza kusikiliza na kuamua jumla ya mashauri 861,” alisema.

Mhe. Luvanda alieleza kupata nafasi ya kuongea na watumishi waliofanya kazi na Jaji Makani ambapo Majaji wameonesha kuwa kuondoka kwake imekuwa haraka ukilinganisha na uwezo au umahiri wake.

“Wengi wametamani angebaki kwa muda zaidi ili aendelee kuandaa maandiko muhimu kwa mashauri yanayoendelea kufunguliwa, kwani kwa mashauri aliyosikiliza alifanikiwa kuonesha umahiri mkubwa na msimamo chanya zaidi kulingana na matakwa ya kisheria,” alisema.

Baada ya maelezo hayo, Jaji Kiongozi alitoa amri kadhaa za kuhitimisha mashauri hayo na kuwashukuru wote waliohudhuria hafla hiyo ya kitaaluma ya kuwaaga Majaji hao wa Mahakama Kuu, ambao wamestaafu rasmi katika utumishi wa umma.

 “Kwa niaba yangu na kwa niaba ya (Majaji wengine wa Mahakama Kuu) ambao kwa pamoja tumesikiliza mwenendo wa mashauri haya maalumu ya kuenzi kazi za kitaaluma, sasa natamka kuwa Majaji Wastaafu, Mhe. Moses Mzuna na Mhe. Victoria Makani wameagwa kitaaluma na kwamba wamestaafu rasmi utumishi wa umma,” amesema.

Jaji Mzuna alianza safari yake ya utumishi katika Mahakama ya Tanzania  tarehe 31 Machi, 1990 alipoajiriwa kama Hakimu Mkazi. Amehudumu katika nyadhifa mbalimbali kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania tarehe 26 Juni, 2009.

Kwa upande wake, Jaji Makani amehudumu katika nafasi mbalimbali katika fani ya sheria kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania mwaka 2015.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akiendesha mashauri katika hafla ya kuwaaga kitaaluma, Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Moses Mzuna na Mhe. Victoria Makani, ambao wamestaafu katika utumishi wa umma. Hafla hiyo imefanyika leo tarehe 31 Agosti, 2023 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dar es Salaam.
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (aliyesimama picha juu na chini) akianzisha mchakato wa kuanza kusikilizwa mashauri katika hafla ya kuwaaga kitaaluma  Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Moses Mzuna na Mhe. Victoria Makani.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu, Mhe. Latifa Mansoor, akimwelezea Mhe. Moses Mzuna.
 Mhe. Moses Mzuna.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda akimwelezea Mhe. Victoria Makani.
 Mhe. Victoria Makani.
 Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Bw. Camilus Luhinda akiwasilisha hoja zake.
Makamu Rais wa  Chama cha Mawakili Tanganyika, Bi. Aisha Sinda akieleza jambo katika hafla hiyo.
Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, wakiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati mstari wa mbele) wakisimama baada ya kusikiliza mashauri hayo. Picha chini, Majaji hao wakiinama kuonyesha heshima ya tukio hilo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni