Jumatano, 30 Agosti 2023

MAHAKAMA MBEYA YAWANOA WATENDAJI WA KATA KUHUSU DHAMANA

Na Mwinga Mpoli-Mahakama Kuu, Mbeya

Mahakama Mkoa wa Mbeya hivi karibuni iliendesha zoezi la utoaji elimu kwa  Watendaji wa Kata kuhusu mambo muhimu wanayopaswa kuzingatia wanapoandaa barua kwa ajili ya washitakiwa kupata dhamana mahakamani.

Zoezi hilo lilifanyika katika ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Mbeya likihusisha Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, baadhi ya Mahakimu, Mawakili wa Serikali pamoja na Watendaji wa Kata wa jiji la Mbeya.

Akiongea katika ufunguzi wa zoezi hilo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba aliwahimiza Watendaji hao kuzingatia taratibu za utoaji wa barua za dhamana ili wasiingie kwenye matatizo.

Aliwaomba kuwa na uthibitisho wa mali zinazowekwa dhamana na wadhamini wawe wanatoka kwenye maeneo yao ya kiutawala ili kurahisisha upatikanaji woa pindi washtakiwa wanapotoroka au wanaporuka dhamana.

“Tujitahidi kutoa barua za dhamana kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni,” alisisitiza Mhe. Tedy.

Naye Wakili wa Serikali Lodgud Eliamani alisisitiza dhamana ni haki ya kila mtu, hivyo Watendaji wasishiriki katika kuzuia barua za dhamana. Alitumia nafasi hiyo kuwaelimisha juu ya makosa yenye dhamana na yasiyo na dhamana.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Watendaji hao, Bw. Jumapili Mwasenga, kwa niaba ya wenzake, alishukuru kwa elimu waliyopata kwani imewawezesha kufahamu na kujua nini kinapaswa kufanyika.

Aliomba yaandaliwe mafunzo ambayo watapata muda wa kutosha pamoja na wenyeviti wa mitaa wao ili nao waelewe mambo yanayotakiwa kufanyika.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba akieleza jambo kwa washiriki.
Wakili wa Serikali Lodgud Eliamani akitoa elimu.
Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Paul Rupia akiwaeleza washiriki vitu gani vinatakiwa kuwepo kwenye barua ya dhamana.
Mwenyekiti wa Watendaji wa Kata Mbeya, Bw. Jumapili Mwasenga akitoa shukurani.
Baadhi ya Watendaji wa Kata na washiriki wengine wa zoezi hilo (juu na chini).

 (Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni