Jumatano, 30 Agosti 2023

UJUMBE BENKI YA DUNIA WAKUTANA NA MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA

Na Faustine Kapama na Magreth  Kinabo-Mahakama

Ujumbe wa Benki ya Dunia leo tarehe 30 Agosti, 2023 umekutana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ofisini kwake jijini Dar es Salaam na kufanya naye mazungumzo mafupi yenye lengo la kuendeleza ushirikiano uliopo kati ya Mahakama na Benki hiyo.

Akizungumza baada ya kuupokea ujumbe huo ulioongozwa na Kiongozi wa Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama ya Tanzania kutoka Benki ya Dunia, Bi. Christine Owuor, Mtendaji Mkuu alielezea maendeleo makubwa yaliyofikiwa na Mahakama ya Tanzania katika kutekeleza jukumu lake la kutoa haki kwa wananchi na kuimarisha miundombinu mbalimbali, ikiwemo majengo.

Ameuhakikishia ujumbe huo kuwa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Mahakama ya Tanzania chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia inaendelea vizuri, siyo tu katika majengo yenyewe, lakini pia matokeo chanya yanayoonekana kutokana na huduma bora zinazotolewa.

Prof. Ole Gabriel alitoa mfano wa ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki, ikiwemo kile cha Masuala ya Familia Temeke ambacho mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa kiasi cha kufikiria watumishi wa Mahakama kuanza kutoa huduma kwa masaa 24.

Ameuambia ujumbe huo wa Benki ya Dunia kuwa kila kitu kwa sasa kinaenda vizuri katika mstakabali mzima wa uendelezaji wa miundombinu mbalimbali na hakuna changamoto kubwa ambayo wanaweza kuielezea kukwamisha utekelezaji wa miradi inayoendelea.

“Ninavyojua, kila kitu kiko chini ya udhibiti wetu wa ndani, daima kumekuwa na usaidizi na uungwaji mkono tangu mwanzo. Kwangu hilo ndilo la muhimu zaidi. Daima mambo huelekea kwenye mwelekeo sahihi kama kuna ushirikiano. Kwa unyenyekevu mkubwa, naomba tuendelee na kasi hii hii,” alisema.

Mtendaji Mkuu, kwa niaba ya Jaji Mkuu, alitoa shukrani zake kwa namna timu kutoka Banki ya Dunia inavyoshirikiana na Mahakama katika kuhakikisha mipango yote inatekelezwa kikamilifu.

Prof. Ole Gabriel aliwaalika Benki ya Dunia kushiriki katika Mkutano mkubwa wa Majaji Wakuu kutoka nchi zote za Bara la Afrika unaotarajia kufanyika Tanzania kwa mara ya kwanza jijini Arusha mwishoni mwa mwezi Octoba, 2023.

Kiongozi wa jumbe huo alitumia nafasi hiyo kumtambulisha Mtaalamu Kiongozi wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bi. Donna Andrews ambaye anaungana na timu hiyo kufuatilia utekelezaji wa miradi mbalimbali inayofadhiliwa na Benki hiyo hapa nchini.

Bi. Donna alieleza kuwa ingawa bado ni mgeni lakini ameshasikia maendeleo mazuri ya miradi mbalimbali inayotekelezwa na Mahakama nchini na kwamba inaeleweka kumekuwepo na mafanikio makubwa.

Alielezea pia furaha yake kwa kukutana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama na kufanyakazi pamoja na timu hiyo ya Benki ya Dunia na aliahidi kuendeleza ushirikiano ulipo kati ya pande mbili.

Tukio hilo la utambulisho lilihudhuriwa pia na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha na Mtalaam wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bw. Benjamin Mtesigwa. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akiongea na wageni wake kutoka Benki ya Dunia. Katikati ni Mtaalamu Kiongozi wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bi. Donna Andrews na kulia ni Kiongozi wa Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama ya Tanzania kutoka Benki ya Dunia, Bi. Christine.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa na wageni wake ofisini jijini Dar es Salaam. Picha chini Kiongozi wa Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama ya Tanzania kutoka Benki ya Dunia, Bi. Christine Owuor (kulia) akisisitiza jambo.

Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (kushoto) na Mtalaam wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bw. Benjamin Mtesigwa wakifuatilia mazungumzo hayo. 



Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe huo kutoka Benki ya Dunia. Kutoka kushoto ni Kiongozi wa Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama ya Tanzania kutoka Benki ya Dunia, Bi. Christine Owuor, Mtaalamu Kiongozi wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bi. Donna Andrews na Mtalaam wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bw. Benjamin Mtesigwa. 
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiagana na mmoja wa wageni wake, Mtaalamu Kiongozi wa Utawala kutoka Benki ya Dunia, Bi. Donna Andrews. Picha chini wageni hao wakibadilishana mawazo na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (wa pili kushoto) baada ya kukutana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama.

(Picha na Magreth Kinabo-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni