Alhamisi, 14 Septemba 2023

HAKIMU MFAWIDHI NJOMBE ASISITIZA UMALIZAJI MASHAURI KWA WAKATI

Na Abdallah Salum-Mahakama, Njombe

Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama amewahimiza Mahakimu katika Mahakama za Wilaya mkoani hapa kuendelea na mpango mkakati wa kumaliza kwa wakati mashauri yanayokaribia kuwa mlundikano kwa kuvuka mwaka toka yaanze kusikikizwa.

Mhe. Chamshama alitoa wito huo hivi karibuni kwenye kikao na kusisitiza ifikapo tarehe 31 Desemba, 2023, Mahakama za Wilaya za Mkoa wa Njombe ziwe zimemaliza aina hiyo ya mashauri. “Hakikisheni kesi inayoanza kufunguliwa ndiyo inayoanza kuisha, lengo kuu hapa ni kuondokana na mlundikando,” alisema.

Kadhalika, Hakimu Mfawidhi aliwasihi watumishi wa Mahakama katika Mkoa huo kuwa na ubunifu ambao utasaidia utekelezaji wa majukumu ya kimahakama na kuongeza ufanisi. Akahimiza pia kwenda na mabadiliko ya teknolojia na kutumia mifumo iliyopo, kama JSD2 na ofisi mtandao (e-office) ili kurahisisha utendaji.

“Mtumishi yoyote ambaye anaubunifu wa nini kifanyike kwenye utendaji kazi wa Mahakama kwa hapa Njombe asisite kuusema au kutoa wazo ambalo litasaidia katika utekelezaji wa misingi ya kimahakama ili kutoa haki kwa wakati na kwa kila mwananchi,” alisema.

 Mhe. Chamshama pia aliwataka watumishi katika eneo lake kujua haki zao za msingi, ikiwemo stahiki za likizo na maslahi kwa upana zaidi ili kuondokana na malalamiko ya kiutumishi ya mara kwa mara.

Akizungumza katika Mkutano huo, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Bw. Yusuph Msawanga aliwahasa watumishi wa Mahakama hiyo kufanya kazi kwa bidii na weledi na kujituma katika kazi ili kukidhi mahitaji na matarajio ya mwananchi.

Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama (kushoto) akitoa mada kwa watumishi. Kulia ni Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Bw. Yusuph Msawanga.
Mtumishi Aneth Mfikwa kutoka Mahakama ya Mwanzo Makambako akichangia hoja. 
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Njombe Mjini, Mhe. Barnaba Mwangi.
Afisa Bajeti wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, akishauri jambo. 

Baadhi ya watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya Njombe wakiwa kwenye kikao.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni