Jumatano, 27 Septemba 2023

IRINGA YAZIZIMA MAHAKAMA SPORTS IKITINGA KIBABE KWENYE MASHINDANO SHIMIWI

·Yazua gumzo kila kona

·Wenyewe watamba kutembeza vichapo mwanzo mwisho

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) imewasili mkoani hapa leo tarehe 27 Septemba, 2023 kushiriki mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayotarajia kuanza kesho kutwa tarehe 29 Septemba, 2023.

Kuwasili kwa Timu hiyo inayoshiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli kumezua gumzo kwenye viunga na mitaa mjini hapa na kufanya baadhi ya maeneo kuzizima.

Kwenye baadhi ya mitaa kulionekana watu wakiwa kwenye vikundi wakijadili ushindani utakavyokuwa wakati wa mashindano na haikujulikana kama watu hao walikuwa wanatoka kwenye timu pinzani au ni wakazi wa mjini hapa.

"Zile bendera zilizotandazwa mbele ya mabasi kama za Mahakama vile. Sijui itakuwaje mwaka huu, maana jamaa wapo vizuri sana hawa kwenye kila mchezo, hasa Kamba.  Hawa ndiyo baba lao, wengine ni mchekea tu," alisikika jamaa mmoja ambaye hakufahamika jina lake akisema.

Akizungumza muda mchache baada ya kufika Iringa, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema wanamshukuru Mungu kwa kufika salama na wanamichezo wote wapo salama na wapo tayari kwa mashindano.

"Wachezaji wote wapo vizuri na tupo tayari kwa michezo ambayo ipo mbele yetu. Tumekuja kuendeleza pale tulipoishia mwaka jana, safari hii kama hakutakuwa na figisu figisu tutafanya maajabu,” alisema.

Naye Mwalimu wa Timu Spear Mbwembe amebainisha kuwa mara baada ya kuwasili wachezaji wote wataenda moja kwa moja kambini kujiwinda na mashindano yanayoanza tarehe 29 Septemba, 2023. "Hatuna muda wa kupoteza, tuna kazi moja tu iliyotuleta, ni ushindi," amesema.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Ndinga zilizobeba wanamichezo wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) zikiwa tayari kwa safari. 
Mwonekano kwa juu wa mji wa Iringa (juu na chini). 

Maandalizi ya safari yalianzia hapa (juu na chini). 

Safari imeanza (juu na chini). 

Safari imekolea sasa. 
Ndinga zinakunywa mafuta kabla ya kuendelea na safari. Picha chini Viongozi wa Mahakama Sports wakijadiliana mambo kadhaa. 

Safari inaendelea mdogo mdogo. 
Ndani ya Mbuga ya Mikumi sasa. 
Wanyama nao (juu na chini) hawakuwa nyuma kushuhudia Mahakama Sports ikichanja mbuga. 

Mlima Kitonga hiyo. 
Dereva wetu alikuwa makini kweli kweli. 
Iringa hiyooooo! 
Mitaani na kwenye vijiwe ilikuwa gumzo. 
Tumefika salama, Mungu ni mkubwa. 

Ilikuwa safari salama kabisa.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni