Alhamisi, 28 Septemba 2023

PAZIA LAFUNGULIWA MASHINDANO SHIMIWI IRINGA

· Mahakama Sports kumenyana na timu 14 kuwania 16 bora

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa

Ratiba ya makundi katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayoanza kufanyika mkoani hapa imeshawekwa hadharani, huku Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ikitarajia kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.

Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende amesema kuwa katika mpira wa miguu, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo.

Ameeleza pia kuwa timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kund G na itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu, huku kamba wanaume ikipangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma, Mawasiliano na Ardhi.

Timu ya kamba wanaume ya Mahakama imepangwa kundi A pia na itakabiliana vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya Uchaguzi (NEC).

Leo jioni tarehe 28 Septemba, 2023, Mahakama Sports imefanya mazoezi mepesi ili kujiandaa na mashindano hayo ambayo yanatarajiwa kuanza kesho tarehe 29 Septemba, 2023.

Mahakama Sports inayoshiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli iliwasili mkoani hapa jana tarehe 27 Septemba, 2023 na kuzua gumzo kwenye viunga na mitaa mbalimbali ya mji.

Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema vijana wote wapo salama na wapo tayari muda wowote kushiriki katika mashindano na ameahidi kuibuka na ushindi kwenye kila mchezo kutokana na ubora wa timu waliyonayo.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.


Timu ya Mahakama mpira wa miguu.
Timu ya Mahakama mpira wa netiboli.
Timu ya kamba wanawake.
Timu ya kamba wanaume.
Timu za kamba wanaume na wanawake (juu na chini) zikiwa kwenye mazoezi.


Timu ya netiboli ikijifua chini ya Mwalimu wao (juu na chini)


Timu ya mpira wa miguu (juu na chini) mambo safi.


Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede naye kumbe yumo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni