·Kamba Wanaume yawang'oa pua Ras Kigoma
·Kamba Wanawake wakimbiwa
Na
Faustine Kapama-Mahakama, Iringa
Mashindano ya Shirikisho
la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika mkoani hapa yameanza
leo tarehe 29 Septemba, 2023, huku timu ya Mahakama (Mahakama Sports) ikiibuka
mshindi kwenye michezo yote miwili ya kamba.
Kamba Wanaume
imenyonyoana na timu ya Ras Kigoma, huku timu ya Wanawake ikizoa pointi zote mbili baada ya Waziri Mkuu Kazi kuingia mitini ili kukwepa kichapo cha mwizi wa
mayai.
Ilikuwa timu ya Kamba
Wanawake iliyoanza kuitwa uwanjani majira ya saa 12.45 asubuhi. Kabla ya mchezo
kuanza, waamuzi waliamua kuusimamisha ili kuisubiri timu kutoka Waziri Mkuu
Kazi. Baada ya kuita kwa mara kadhaa, timu ya Mahakama ikaamuriwa icheze peke
yake na kuzoa pointi zote mbili.
Baada ya kukamilika kwa
mchezo huo, timu za Kamba Wanaume ziliingia uwanjani, huku Mahakama Sports
ikipangwa na Ras Kigoma. Baada ya mchezo kuanza, Mahakama Sports haikuwa na huruma
na mtu, iliwakamua kisawasawa timu pinzani katika awamu ya kwanza.
Awamu ya pili ilipoanza,
Ras Kigoma walijaribu kuwaragai waamuzi kwa kuvuta kamba kabla ya filimbi
kupigwa. Hata hivyo, waamuzi walishtukia janja janja hiyo na kurejesha kamba
kwenye mstari.
Baada ya mwamuzi kupuliza
kipenga kuashiria kuanza kwa mchezo, timu ya Mahakama ilikuwa kama Nyati aliyejeruhiwa
na kuwaburuza vibaya Ras Kigoma, hivyo kuondoka na pointi zote mbili.
Mwenyekiti wa Mahakama
Sports Wilson Dede amewapongeza vijana wake kwa kuonyesha mchezo mzuri na
kupata ushindi huo mkubwa. Amesema kuwa huo ni mwanzo mzuri katika mashindano
hayo.
"Nawapongeza
wachezaji wote kwa ushindi huu ambao unaonyesha nia yetu iliyotuleta kwenye
mashindano haya. Tutaendelea kupambana kwenye michezo ijayo na safari hii
hakuna atakayechomoka salama, labda watukimbie," amesema.
Baadaye majira ya mchana
kutakuwepo na mechi nyingine ambapo timu ya Mahakama ya Netiboli ambayo ipo
kundi G inatarajia kupepetana na Ras Kilimanjaro.
Mchezo
wa mpira wa miguu wa kundi A kati ya Mahakama Sports na Kilimo uliokuwa uchezwe
leo majira ya asubuhi umeahirishwa hadi siku nyingine kufuatia Kilimo kufiwa
ghafla na Nyanda wao tegemezi.
Kwa
mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia
kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.
Katika mpira wa miguu,
timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji,
RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na
itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.
Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume,
timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma,
Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana
vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya
Uchaguzi (NEC).
Mahakama Sports inashiriki
katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira
wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.
Katika mashindano ya
SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa
makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.
Michezo ambayo Mahakama
Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa
kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa
kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume
walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni