Jumanne, 19 Septemba 2023

JAJI EBRAHIM AFANYA ZIARA MKOANI LINDI

Na. Hilary Lorry – Mahakama Lindi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim hivi karibuni amefanya ziara ya kikazi mkoani Lindi na kukagua shughuli mbalimbali za kimahakama katika Wilaya tatu (3) zilizopo katika mkoa huo ambazo ni Liwale, Nachingwea na Ruangwa.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama katika Wilaya hizo kwa nyakati tofauti akiwa katika ziara ya ukaguzi wa shughuli za Mahakama Jaji Mfawidhi Mhe. Ebrahim aliwapongeza watumishi wa Mahakama za mkoa wa Lindi kwa kufanya kazi kwa uadilifu, weledi na ufanisi mkubwa katika kuwahudumia wananchi.

“Nafahamu kazi yetu ya utoaji haki kwa wananchi ni ngumu lakini nichukue fursa hii kuwapongeza Mahakimu wote wa Mkoa Lindi kwa jitihada kubwa za uondoshaji wa mashauri ya mlundikano na mikakati mizuri mliyojiwekea yenye lengo la kutozalisha mashauri ya muda mrefu (backlog cases)”, aliongeza Mhe. Ebrahim.

Mhe. Ebrahim alipata wasaa wa kufanya ukaguzi wa Mahakama zilizopo chini ya Kanda ya Mtwara na ukaguzi wa Mirandi ya ujenzi inayoendelea ikiwemo ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Liwale ambao upo katika hatua za mwisho kabla ya kukabidhiwa kwa ajili ya matumizi ya shughuli za kimahakama, na pia alitembelea eneo ambalo hivi karibuni linakusudiwa  kujengwa  Mahakama ya Wilaya ya Nachingwea.

‘’Tujitahidi kufanya kazi kwa bidii, maarifa, weledi na kwa ushirikiano hii itafanya Mahakama yetu ing’are na kuwa mfano bora wa kuingwa.Kila mmoja wetu awajibike kwa nafasi yake na tufanye kazi kama timu moja na siku zote tufanye kazi katika  ubora unaotakiwa”, alisisitiza  Jaji Mfawidhi huyo

 Kwa upande wa ushirikiano na wadau Mhe. Ebrahim alisema, ni jambo la msingi sana kiutendaji kushirikiana na wadau kwa karibu. “Natambua ushirikiano na ushirikishwaji mzuri uliopo kati ya Mahakama za Mkoa wa Lindi na wadau, mahusiano mema yanatija kubwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kwa wote”, aliongeza Mhe. Ibrahim.

Vilevile aliupongeza uongozi wa Mahakama Mkoa wa Lindi kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya ya utoaji elimu kupitia vyomba  vya Habari ikiwemo Radio Mashujaa FM, Mitandao ya kijamii, Club za Mahakama katika shule mbalimbali za sekondari na utoaji wa elimu kwenye mikusanyiko ya watu na kwa wateja wanaofika Mahakamani asubuhi kwa ajili ya kusikiliza mashauri yao.

Katika ziara hiyo Mhe Jaji Mfawidhi Kanda ya Mtwara aliongozana na viongozi mbalimbali waandamizi wa Kanda hiyo akiwepo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Fredrick Lukuna, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe. Consolata Peter Singano, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Bw.Richard Mbambe na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Qiup Mbeyela.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe.Rose Ebrahim akiongea na watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Liwale, Nachingwea na Ruangwa( Hawapo kwenye picha) alipofanya ziara ya ukaguzi wa shughuli za kimahakama mkoani Lindi.

Watumishi wa Mahakama ya wilaya ya Liwale,Ruangwa na Nachingwea wakimsikiliza kwa makini Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim (hayupo pichani).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ebrahim (Mwenye skafu) akiwa kwenye picha ya pamoja Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Liwale, Nachingwea na Ruangwa  alipofanya ziara katika Mkoa huo.


Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela akichangia mada.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ebrahim (wa kwanza kushoto) akikagua jengo la Mahakama ya Wilaya ya Liwale na kupewa maelezo ya kina kutoka kwa Mhandisi Mshauri wa Wakala wa Majengo Tanzania ( TBA)
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ebrahim (Mwenye Kilemba wa kwanza kulia) akipokea maelekezo wakati akikagua jengo la Mahakama ya Wilaya ya Liwale.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ebrahim akiandia neno la kumbukumbu katika ubao wa kumbukizi  Mahakama ya Wilaya ya Ruangwa.




Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ebrahim akipanda mti katika viwanja vya Mahakama ya Wilaya ya Ruangwa na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Ruangwa Mhe.Mariam Mchomba akishuhudia. 

Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni