Na Hasani Haufi- Mahakama Kuu, Songea
Jaji
Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James
Karayemaha amekabidhiwa ofisi rasmi na mtangulizi wake, Mhe. Ephery Kisanya ambaye
amehamishiwa Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi Dar
es salaam.
Hafla
hiyo ya makabidhiano ilifanyika jana tarehe 24 Septemba, 2023 katika ukumbi wa
wazi wa Mahakama Kuu Songea na kushuhudiwa na wajumbe wa menejimenti wa Kanda
hiyo kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea na Mahakama za Wilaya Songea,
Mbinga, Nyasa, Namtumbo na Tunduru.
Akizungumza
wakati wa makabidhiano hayo, Mhe. Kisanya alianisha mafanikio yaliyopatikana,
ukiachilia mbali uwepo wa mashauri machache ya mlundikano ambayo hayatokani na
Mahakama moja kwa moja bali wadau wanaoshirikiana nao. Alisema kuwa mafanikio
hayo yamechagizwa na kujituma na ushirikiano kutoka kwa watumishi.
“Katika
kipindi cha miezi mitatu niliyoongoza hapa Songea tumeweza kufanya kazi kwa
pamoja na mmenipa ushirikiano mzuri na hakuna kilichoharibika. Namkabidhi Mhe.
Karayemaha Kituo kikiwa salama kwa sababu nyie ndiyo mliyesababisha kikawa
salama,” Mhe. Kisanya aliwaambia watumishi hao.
Kadhalika,
Jaji Kisanya aliwaasa kutumia muda vizuri wakiwa kazini na kutimiza majukumu yao
ya kila siku kwa weledi na uadilifu, Alisema kuwa ili Taasisi iweze kufikia
malengo yake inatemegemea uwajibikaji wa watumishi katika kila kada.
“Kila
mmoja wetu ana fursa au nafasi yake katika kuhakikisha kwamba ile shughuli ya
Mahakama ya utoaji haki kwa wananchi inafanyika bila kujali wewe ni dereva,
mlinzi, karani na hata mhasibu. Kila mmoja kwa nafasi yake anakuwa anashiriki,”
alisema.
Jaji
Kisanya aliwahimiza watumishi wote kumpa ushirikiano Jaji Mfawidhi mpya kama
waliyofanya kwakwe. “Ninapoondoka amekuja Jaji mpya, endelezeni ushirikiano mliokuwa
mnanipa na ikiwezekana uwe zaidi yangu kwani yeye ana vitu vyake na mtaviona,”
alisema Jaji Kisanya.
Kwa upande wake, Mhe. Karayemaha alimshukuru mtangalizi wake na kumweleza kuwa yote aliyoyaeleza atayatumia kama funguo za kufungulia milango ya Kanda ya Songea, kwani ameyaona mazuri mengi aliyoyafanya kwa muda mfupi.
Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha (kulia)
akipokea nyaraka mbalimbali za ofisi kutoka kwa mtangulizi wake, Mhe. Ephery
Kisanya.
Jaji
Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James
Karayemaha akizungumza na watumishi.
Sehemu
ya wajumbe wa menejimenti ya Mahakama Kanda ya Songea ikifuatilia zoezi la
kukabidhiana ofisi.
Hakimu
Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Songea akitoa neno la shukrani kwa niaba ya
watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea, Mhe. Lilian Rugarabamu.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni