Ijumaa, 15 Septemba 2023

JAJI KIONGOZI ATETA NA MAJAJI WAPYA WA MAHAKAMA KUU

 

  •    Asisitiza Maadili na Uadilifu kama njia ya msingi wa kutekeleza jukumu la utoaji haki.

Na. Innocent Kansha – Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani amesisitiza maadili na uadilifu kwa Majaji Wapya wa Mahakama Kuu, kama njia kuu ya msingi ya kutekeleza jukumu mama la utoaji haki kwa wananchi.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika jana tarehe 14 Septemba, 2023 Mahakama Kuu jijini Dar es salaam kilichojumuisha Majaji wapya wa Mahakama Kuu mara baada ya kuapishwa, Mhe. Siyani alisema, majukumu ya Jaji wa Mahakama Kuu yatabadilisha baadhi ya mambo ya msingi waliyoyazoea na kwamba wameanza safari mpya ya utumishi ambayo awali hawakuwa nayo.

“Nafahamu kwamba baadhi yenu mmeingia kwenye utumishi wa umma kwa mara ya kwanza, lakini pia wapo baadhi yenu ambao mlikuwa watumishi wa umma na wengine mlikuwa Maafisa Mahakama kabla ya kupata uteuzi na kuapishwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu,” alisema Jaji Kiongozi.

Mhe. Siyani alikumbusha kuwa, jambo la muhimu ni kwamba Mahakama ni familia moja yenye mila na desturi moja, hivyo ni wajibu wenu kujifunza na kuzielewa kwa haraka mila na desturi zilizoainishwa katika Kanuni za Maadili za Maafisa Mahakama (The Code of Conduct and Ethics). Kwa hiyo, kila mmoja anapaswa kufahamu dira na dhima ya Mahakama, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali katika utendaji kazi.

“Mtapaswa kujifunza tamaduni mbalimbali ambazo hazijaandikwa na kuzitafsiri ili kuboresha mtizamo na kuleta tija katika utoaji haki, mtalazimika kuzingatia maadili yasiyo na mashaka ili kulinda heshima ya ofisi ya Jaji wa Mahakama Kuu. Ni muhimu kwa mfano kila Jaji kuheshimiana na mwenzake, ikiwa ni pamoja na kuheshimu ngazi za madaraka yenu”, alisisitiza Jaji Kiongozi.

Aidha, kwa upande wa utoaji haki, Jaji Kiongozi aliwakumbusha Majaji hao jukumu la msingi la Mahakama kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa ni kutenda  haki  kwa  wote  bila  ya  kujali  hali  ya  mtu  kijamii  au kiuchumi, kutochelewesha haki bila sababu ya kimsingi. Kutoa fidia ipasayo kwa watu wanaoathirika kutokana na makosa  ya  watu  wengine,  na  kwa  mujibu  wa  sheria  mahususi iliyotungwana Bunge na kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro.

“Tumieni weledi na umahiri wenu, kuhakisha haki haichelewi, haipotei kwa sababu za kiufundi, waathirika wanapata fidia inayostahili na pia kumaliza mashauri kwa kuhimiza usuluhishi kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa. Aidha ni vema kujifunza mazingira ya kijamii na kiuchumi ili iwasaidie katika kujibu matarajio halali ya wananchi wanaofika mbele yenu”, aliongeza Mhe. Siyani.

Jaji Kiongozi alisema, tafsiri za sheria zijielekeze katika ustawi wa jamii ya watanzania kiuchumi na kijamii. Hii ni kwa kuzingatia kama alivyowahi kusema Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Juma kwamba, “Wananchi kupitia Katiba wametupa sisi Majaji mamlaka ya utoaji haki lakini wananchi wamebaki na haki zao zote za msingi”

Jaji Siyani alieleza kuwa, ni vema Majaji hao wakafahamu wakati wote, kwamba kutotekeleza jukumu la utoaji haki kwa ufanisi, uaminifu na weledi wa kutosha, itaathiri siyo tu imani kwao bali kwa Mahakama na mfumo mzima wa utoaji haki, kwa kuwa maamuzi yao yatatumika kama rejea na Mahakama za chini hivyo kwa kujitahidi kutoa tafsiri sahihi inayoakisi uzito wa dhamana ambayo Mahakama imepewa.

Alikadhalika, Mhe. Siyani aliwahimiza Waheshimiwa Majaji kuwa, wao ni viongozi, na kwamba uongozi wao utajionyesha zaidi katika usimamiaji na uendeshaji wa mashauri. Aidha, kwa kuwa utoaji haki unahusisha pia wadau, onesheni mwelekeo wa utendaji utakaopaswa kuheshimiwa na wadau bila malalamiko.

“Mna wajibu wa kusaidiana na waheshimiwa Majaji na viongozi wengine mtakaowakuta kituoni kuwaongoza na kuwaelekeza waheshimiwa Mahakimu na watumishi wengine kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi mkubwa kwa faida ya mwananchi tunayemhudumia”, alisistiza Jaji Kiongozi.

Kwa upande wa usikilizwaji wa mashauri, Jaji Kiongozi akawaomba Majaji hao kwa msisitizo kutokubaliana na suala la mlundikano wa mashauri mahakamani, kwani mashauri yenye umri unaozidi miezi 24 Mahakamani yatahesabika kama mashauri yenye mlundikano.

“Kuna mambo mengi yanayosababisha mlundikano wa mashauri lakini kubwa zaidi ni maahirisho ya mashauri yasiyo kuwa na sababu za msingi. Maahirisho haya yamekuwa sababu ya malalamiko dhidi ya Mahakama. Suala muhimu ni kwa kila Jaji kuwa makini na shajara au diary yake. Hakikisha kila shauri lililo mbele yako linapangiwa muda wake maalumu ili kuepusha malalamiko yasiyokuwa ya lazima ya wadaawa kusubiri muda mrefu Mahakamani”, aliongeza Jaji Siyani.

Mhe, Siyani akawakumbusha Majaji hao kuendeleza jitihada za matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano alisema, kwa sasa Mahakama imejikita katika matumizi makubwa ya TEHAMA kwenye usimamizi na uendeshaji wa mashauri na shughuli nyingine za utawala. Mifumo ya kielektroniki ndiyo inayotumika katika usajili wa mashauri mahakamani, usimamizi na uhifadhi wa kumbukumbu mbalimbali za mashauri mahakamani kupitia mfumo wa JSDS II na usikilizaji wa mashauri kupitia Mahakama Mtandao (video conference).

Pia mfumo wa kuratibu taarifa za mawakili (e wakili), vilevile Mahakama inatarajia kuhamia kwenye  mfumo wa ki-elektroniki wa usimamizi wa mashauri (e Case Management System) ambao utatumika kusikiliza mashauri ikiwa ni hatua muhimu kuelekea Mahakama Mtandao.

“Niwafahamishe kuwa nanyi mtanufaika na mafunzo ya mfumo huo. Mfumo huu unakwenda sambamba na mfumo wa kurekodi na kutafsiri (Transcription and Translation System TTS). Aidha, mfumo wa ki-elektroniki wa utambuzi wa mahitaji ya Mahakama (court mapping) husaidia kupata taarifa za majengo ya Mahakama. Hivi sasa unajengwa mfumo wa kuratibu taarifa za madalali wa Mahakama”, alifafanua Mhe. Siyani.

Jaji Kiongozi akawahimiza Majaji hao kuwa watumiaji na vinara wa usimamizi wakuu wa mifumo hiyo ya TEHAMA. Lengo liwe kuhakikisha kwamba, mashauri yatakayokuja mbele yao yawe yamesajiliwa katika mfumo na taarifa zake ni sahihi, maamuzi watakayotoa yawekwe wazi kwa umma kupitia mtandao wa TanzLII.

Vilevile kwa kadri inavyowezekana kuwasaidia wadaawa na mashahidi wanapata nafuu ya gharama na muda kwa kusikilizwa mashauri yao kwa njia ya mtandao (video/audio Conferencing) bila kulazimika kusafiri kuja mahakamani, Kutumia ipasavyo fursa ya maktaba mtandao kujifunza kwa nia ya kuimarisha weledi katika kazi zao na kuhakikisha wanatoa mchango wao kuimarisha matumizi ya Mahakama  mtandao.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akizungumza na Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania (hawapo pichani) alipokutana nao na kufanya kikao cha pamoja ili kukumbusha baadhi ya mambo ya kiutendaji jana tarehe 14 Septemba, 2023 katika ukumbi wa Mahakama Kuu jijini Dar es salaam, wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Salma Maghimbi (kulia) na (kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Mhe. Latifa Mansoor.

 

Sehemu ya Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakinukuu baadhi ya mambo muhimu yaliyotokana na kikao hicho cha pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo pichani)


Sehemu ya Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakisikiliza na kinukuu baadhi ya mambo muhimu yaliyotokana na kikao hicho cha pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo pichani).


Sehemu ya Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakisikiliza na kinukuu baadhi ya mambo muhimu yaliyotokana na kikao hicho cha pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo pichani).



Sehemu ya Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakisikiliza na kinukuu baadhi ya mambo muhimu yaliyotokana na kikao hicho cha pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo pichani).


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania mara baada ya kuhitimisha kikao hicho, wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Salma Maghimbi (kulia) na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Mhe. Latifa Mansoor.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji Wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania na wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA) mara baada ya kuhitimisha kikao hicho, wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Salma Maghimbi (kulia) na (kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Mhe. Latifa Mansoor.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni