Jumatano, 20 Septemba 2023

JAJI MKUU AHIMIZA KAMATI ZA MAADILI KUTEKELEZA WAJIBU WAKE.

Na. Mayanga Malingila – Mahakama, Sumbawanga.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma hivi karibuni alimtembelea Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Makongoro Nyerere Ofisini kwake na kufanya naye mazungumzo na kumshukuru kwa kushiriki hafla ya uzinduzi wa Kikao cha kwanza cha Mahakama ya Rufani katika viwanja vya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga.

Akizungumza na Mkuu wa Mkoa huyo mara baada ya kukutana Mhe. Prof. Juma alisema kuwa, Mkuu wa mkoa na Wakuu wa Wilaya ni  wenyeviti wa Kamati za Maadili ya Maafisa wa Mahakama hivyo haina budi kusimamia nidhamu na mienendo ya Maafisa hao katika ngazi ya Mkoa na Wilaya. Kwa kufanya hivyo watakuwa wametimiza jukumu lao la kisheria la kusimamia maadili ya Wahe. Mahakimu katika maeneno hayo kupitia kamati hizo na kusisitiza haki itendeke kwa anaekiuka maadili.

“Nichukue fursa hii kukushukuru kwa kuja kushirikiana na Mahakamama katika uzinduzi wa Kikao cha Mahakama ya Rufani kwa dhumuni la kuanzisha Masjala Ndogo ya Mahakama ya Rufani ni kuhakikisha Mahakama inatekeleza Nguzo ya pili ya Mpango Mkakati wake ya Upatikanaji haki kwa wakati kwa lengo la kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi”, aliongeza Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma alisema faida za uanzishaji wa Masjali hiyo ni nyingi mathalani wananchi kutosafiri umbali mrefu kutafuta haki zao, kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri yao lakini pia kuhakikisha mashauri yanachukua muda mfupi kusikilizwa ili wananchi hao wapate muda wa kutosha kushiriki katika shughuli zao za kiuchumi na kijamii.

“Katiba inatoa nafasi ya Mihimili kushirikiana katika kutekeleza majukumu yao, kwa sababu Serikali inatuwezesha kwa kutuweka pamoja katika Mpango wa Maendeleo ya Nchi. Nia ya Mahakama ya Tanzania ni kuona ifikapo 2025 Mikoa yote isiyokuwa na huduma ya Mahakama kuu inapatikana ili wananchi wapate huduma hiyo kwa ukaribu zaidi bila kutumia gharama za ziada”, alisema Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma alisema kuwa, suala la Mahakama kutumia mfumo wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuimarisha mfumo wa utoaji haki kwa wananchi inalenga kurahisisha utoaji haki kwa wakati.

‘’Mhe. Mkuu wa Mkoa nikutoe shaka,kuwa Mahakama imejikita zaidi katika matumizi ya TEAHAMA ili kuboresha mfumo mzima wa utoaji haki kwa wananchi, nakuahidi Mahakama ya Rufani itaendelea kusikiliza mashauri kwa Kanda ya Sumbawanga na endapo kutakuwa na shauri la haraka Mahakama ya Rufani itasikiliza kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual court)”, alisema Prof. Juma.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Makongoro Nyerere aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuwa huru na kuelekeza nguvu kubwa katika kuwatumikia Wananchi wa Tanzania na kutoingiliwa na Serikali jambo ambalo linaifanya kuonekana ipo huru.

“Mahakama yetu ni huru ina heshima na nguvu, uhuru huo unatokana na kwamba Serikali haiingilii Mahakama katika kutekeleza amri zake na ndiyo maana kuna mabadiliko makubwa yamefanyika ndani ya Mahakama,ninakupongeza Jaji Mkuu kwa kusimamia mabadiliko hayo’’,alisema Mkuu huyo wa Mkoa.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (alieketi mbele), akiendelea na mazungumzo alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Ofisini kwake pamoja na ugeni wageni aliyoambatana nao.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Makongoro Nyerere (kushoto), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Amir Mruma (katikati) na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Bw.Emmanuel Munda (kulia) wakifuatilia maongezi ya Jaji Mkuu wa Tanzania (hayupo pichani).

Msajili wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Mhe.Sylvester Kainda (kulia), Naibu Msajili wa Mahakama Kuu kanda ya sumbawanga Mhe.Maira Kasonde (katikakti) na Naibu Msajili na Katibu wa Jaji Mkuu Mhe. Venance Mlingi (kushoto) wakifuatilia mazungumzo hayo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe.Prof Ibrahim Hamis Juma akielezea jambo wakati wa ziara hiyo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe.Prof Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe Makongoro Nyerere (kulia) mara baada ya kuwasili Ofisini kwake.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni