Na. Paul Mushi- Mahakama, Moshi
Majaji
na Mahakimu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, wametakiwa kuzingatia
misingi ya uadilifu, usawa na kuheshimu utawala wa Sheria katika kutekeleza
jukumu lao la utoaji haki, ili kuendelea kukuza imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama.
Rai
hiyo imetolewa hivi karibuni na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda
ya Moshi, Mhe. Dkt. Lilian Mongela wakati akifungua mafunzo ya Majaji na
Mahakimu wa Kanda hiyo, yanayofanyika katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi
Moshi, yakiwa na lengo la kuwajengea uelewa wa umuhimu wa maadili kwa viongozi
wa umma na kujikumbusha mambo ambayo wanapaswa kuepuka katika utendaji wao wa
kazi.
Mhe.
Dkt. Mongela amesema, maendeleo ya nchi yoyote duniani yanategemea kwa kiasi
kikubwa uzingatiaji wa maadili katika kusimamia rasilimali za taifa na katika
utoaji wa huduma bora katika sekta ya umma na binafsi na kwamba uongozi wa umma
ndiyo chachu ya kuleta usawa, umoja, upendo, amani na kuheshimu utawala wa
sheria.
"Uongozi
wa umma ndiyo chachu ya kuleta usawa, umoja, upendo, Amani na mfano wa
kuheshimu utawala wa sheria, na katika muhimili wetu, sisi tukiwa watu tulioaminiwa kutoa haki kwa
jamii suala hili ndilo linapaswa kuwa kipaumbele chetu cha kila siku ili
kutokuondoa imani kwa wale wanaotutegemea kujipatia haki"amesema Mhe. Dkt.
Mongela.
Ameongeza
kuwa "Ni imani yangu kuwa, uelewa na ujuzi mtakaoupata kupitia mafunzo
haya utaimarisha waledi mlio nao na kuhakikisha jukumu la msingi la Mahakama la
utoaji haki linatekelezeka katika misingi ya uadilifu, na kukuza zaidi imani ya
wananchi kwenye Mahakama zetu"
Jaji
Mfawidhi huyo alisema, mafunzo hayo yatawasaidia kujikumbusha jukumu lenu la
msingi la utoaji haki na kuongeza uelewa wa pamoja juu ya mambo gani ambayo mnapaswa
kuyaepuka kama viongozi ili kulinda heshima ya muhimili wa Mahakama. Wakufunzi
wameandaa mambo mazuri ambayo yatasaidia kwenda kufanya mabadiliko katika
masuala yahusuyo maadili na hivyo kuwa kioo kwa wale mnaowahudumia katika
nafasi zenu.
Naye,
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Omari Kingwele
alisema, Mahakama ni miongoni mwa taasisi ambazo zimekuwa zikilalamikiwa
mafunzo hayo yatasaidia kujiimarisha na kujisafisha ili kuondoa malalamiko ya
wananchi ya mara kwa mara.
"Zikichambuliwa
taasisi ambazo zinalalamikiwa na watu Mahakama haikosekani miongoni mwa taasisi
10 zinazotajwa na hii inatokana na kwamba tunahudumia kundi kubwa la watu na
katika mfumo wetu wa maamuzi anayeshinda kashinda na anayeshindwa kashindwa,
hivyo tunahitaji sisi wenyewe kwanza kujisafisha ili kule kunyooshewa kidole
ibaki kwenye dhana na si uhalisia", aliongeza Naibu Msajili huyo.
Kwa
upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Moshi, Bw. Donald Makawia
alisema mafunzo hayo ni sehemu ya sera ya Mahakama ya kuwajenga watumishi uwezo
na kuwakumbusha majukumu yao ikiwa sambamba na suala la maadili wawapo kazini
hatua ambayo itawawezesha kuzingatia uadilifu na pindi wanapotekeleza majukumu
yao.
"Majaji
na Mahakimu, wao ndiyo watoa haki hivyo wanapaswa kuwa waadilifu, waaminifu katika
kazi yao ya kutoa haki mahakamani na kuzingatia miiko na kanuni zote za maadili
ya utumishi wa umma wanapofanya kazi zao za kila siku, kila mmoja atambue
uzingatiaji wa maadili ya utumishi na kujiepusha na vitendo vya rushwa ni
jukumu lao katika kuhakikisha wananchi wanapata haki", alisema Bw. Makawia
Hakimu
Mkazi wa Mahakama Wilaya ya Rombo, Mhe. Atupele Mwanjala ambaye ni mmoja wa
washiriki wa mafunzo hayo amesema yatawasaidia katika utendaji kazi wao wa kila
siku kwani kazi hiyo inahitaji maadili kwa kiasi kikubwa ili kutoa haki kwa
wananchi.
Mafunzo
hayo ambayo yanatolewa na wakufunzi kutoka taasisi ya kuzuia na kupambana na
Rushwa (Takukuru) na Tume ya maadili, yamejikita kwenye mada mbalimbali ikiwemo
Takukuru na majukumu yake, Mgongano wa Maslahi, baadhi ya makosa ya Rushwa
yanayoonekana na kutendeka mahakamani, ahadi ya uadilifu kwa viongozi wa umma
pamoja na athari za kutozingatia maadili kazini.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Dkt. Lilian Mongela (katikati walioketi) akiwa kwenye picha pamoja na washiriki wa mafunzo hayo kutoka Mahakama za Wilaya na Mwanzo, yaliyofanyika hivi karibuni Mahakama ya Hakimu Makazi mjini Moshi, wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Safina Simfukwe (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Adrian Kilimi (kulia).
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Dkt. Lilian Mongela akifungu rasmi mafunzo hayo katika ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini Moshi.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Safina Simfukwe (kushoto) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Adrian Kilimi (kulia) wakifuatilia mada katika mafunzo hayo.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo kutoka Mahakama za Wilaya na Mwanzo walioshiriki mafunzo yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano Mahakama ya Hakimu Makazi mjini Moshi.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi Mhe. Omari kingwele (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Moshi Bw. Donald makawia (kulia) wakifuatilia mafunzo hayo.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha- Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni