Jumanne, 26 Septemba 2023

JAJI NGWEMBE AKABIDHI UFAWIDHI MOROGORO KWA JAJI MANSOOR

Na Evelina Odemba – Mahakama Morogoro

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe amekabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi mpya, Mhe. Latifa Mansoor jana tarehe 25 Septemba, 2023 ikiwa ni baada ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani.

Mhe. Mansoor ambaye kabla ya kuja Morogoro alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Dar es Salaam ambapo akiwa huko alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) ngazi ya Tawi la Mahakama Kuu, Masjala Kuu.

Katika hafla ya makabidhiano, Majaji hao walipata wasaa wa kuzungumza na watumishi pamoja na wadau wa Mahakama, ambapo Mhe. Ngwembe alitumia nafasi hiyo kuagana na wanamorogoro, huku Mhe. Mansoor akatumia wasaa huo kujitambulisha na kuwatambua watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo.

Akitoa shukrani wakati wa kuagana na watumishi, Mhe. Ngwembe alisema kuwa ushirikiano alioupata toka Kanda ya Morogoro usiishe mara baada ya kuondoka kwake bali uendelee kwa Kiongozi huyo mpya na hata Viongozi wengine watakaoendelea kuja kwenye Kanda hiyo.

“Leo ni siku yangu ya pekee na adimu, nalazimika kuagana na watumishi niliokuwa nao tokea 2021, watumishi hawa wamenipa heshima kubwa sana, Viongozi hawawezi kufanya kazi peke yao isipokuwa kwa ushirikiano na umoja wetu,” alisema.

Naye Mhe. Mansoor alipokea kwa mikono miwili makaribisho aliyoyapata kwa watumishi wa Kanda hiyo, huku akisisitiza kuwa ofisi yake ipo wazi kwa yeyote mwenye mawazo ya kuboresha. Alisisitiza kuwa yeye ni mtu wa kazi na anavutiwa zaidi na wachapakazi.

“Nashukuru kwa uongozi wa Mahakama kwa kuona kuwa mimi naweza kuziba pengo la Mhe. Ngwembe, nimeona na nimeambiwa mafanikio ya Kanda ya Morogoro, sifa ya Morogoro kutoa elimu ni utamaduni mzuri nitaomba tuendelee nao,” alisema.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya watumishi, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Gabriel Malata alisema kuwa wataendelea kutoa ushirikiano kwa Kiongozi wao mpya ili aweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa.

Kauli hiyo iliungwa mkono Jaji mwingine wa Mahakama hiyo, Mhe. Messe Chaba ambaye aliongeza kuwa wapo tayari kuyapokea maelekezo toka kwa Kiongozi huyo na kuonesha ushirikiano.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Paul Ngwembe (kushoto) akimkabidhi taarifa ya Kanda Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor (kulia) wakati wa makabidhiano ya ofisi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor (kushoto) akipokea zawadi ya ua toka kwa aliyekuwa Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Messe Chaba (kulia) ikiwa ni ishara ya ukaribisho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa        Mansoor (aliyesimama) akizungumza na wanachama wa TAWJA Kanda ya Morogoro. Picha chini akipokea zawadi toka TAWJA.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Latifa Mansoor (kushoto) akimlisha keki Mtendaji wa Mahakama Kanda, Bw. Ahmed Ng’eni na kulia ni Naibu Msajili Mhe. Agustina Mbando.

Sehemu ya watumishi na wadau wa Mahakama (juu na chini) wakifuatilia hotuba ya Jaji Latifa Mansoor (hayupo pichani). 

Tukio la makabidhiano ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi toka kwa Mhe. Paul Ngwembe, aliyekaa mbele kwenda kwa Jaji Mfawidhi mpya wa Kanda ya Morogoro Mhe. Latifa Mansoor (wa pili kulia). Wengine ni Jaji Messe Chaba (wa tatu kushoto), Jaji Gabriel Malata (wa kwanza kulia), Naibu Msajili, Mhe. Augustina Mmbando (wa pili kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Ahmed Ng’eni (wa kwanza kushoto).

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni