Na Faustine Kapama-Mahakama
Mahakama ya Tanzania itakuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jukwaa la Majaji Wakuu wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika utakaofanyika jijini Arusha kuanzia tarehe 23 hadi 27 Oktoba, 2023.
Hayo yamebainishwa
leo tarehe 1 Septemba, 2023 na Mwenyekiti
wa Kamati ya Maandalizi ya Mkutano huo, Mhe, Ignas Kitusi alipokuwa anaongea na
Wahariri na Waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari katika Kituo Jumuishi
cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam.
“Mkutano wa Jukwaa
la Majaji Wakuu wa Nchi za Mashariki na Kusini
mwa Afrika (SEACJF) utafunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.
Dkt. Samia Suluhu Hassan,” Mhe Kitusi, ambaye
pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania amesema.
Amesema Mkutano huo utahudhuriwa na Majaji Wakuu
16 kutoka Angola, Botswana, Eswatin, Kenya, Lesotho, Malawi, Mauritius,
Msumbiji, Namibia, Seychelles, Afrika Kusini, Tanzania Bara, Tanzania Visiwani
(Zanzibar), Uganda, Zambia na Zimbamwe.
Mwenyekiti huyo
amebainisha kuwa Jukwaa hilo ni sehemu muhimu ya kukuza ushirikiano,
kubadilishana maarifa na maendeleo ya mifumo ya Mahakama ndani ya eneo la
Kusini mwa Afrika.
“Jukwaa hili pia ni
sehemu ya kujadiliana juu ya changamoto zinazowakabili katika mfumo wa utoaji
haki na kubadilishana mbinu bora na kushughulikia changamoto zinazokabili
Mahakama katika Nchi zetu,” amesema.
Mhe. Kitusi
amesema kuwa Kauli mbiu ya Mkutano huo ni “Wajibu wa Mahakama za Kitaifa katika Utatuzi wa Migogoro kwenye Eneo Huru
la Biashara la Afrika (AFCFTA): Matumizi ya teknolojia ya kisasa ili kuongeza ufanisi
katika utoaji wa haki.”
Amesema kuwa
kulingana na kaulimbiu hiyo kusisitiza biashara huria, wakati Mkutano huo kutakuwepo
na matukio muhimu ambayo yatakuwa yakiendelea, ikiwemo mijadala na mawasilisho
kutoka kwa wanasheria na wanazuoni kutoka maeneo mbalimbali ya Nchi za SADC.
“Kutakuwepo pia na
maonesho ya wadau mbalimbali wa Mahakama yatakayokuwa yakiendelea katika
Viwanja vya Hoteli ya Mount Meru kuanzia tarehe ya ufunguzi tarehe 23 Oktoba hadi
ufungaji wa Mkutano tarehe 27 Oktoba, 2023,” amesema.
Wadau hao wanaotegemewa
ni Wizara ya Fedha, Wizara ya Biashara, Wizara ya Maliasili na Utalii, Mamlaka
ya Mapato Tanzania (TRA), Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) na Mamlaka ya
Hifadhi ya Ngorongoro.
Kutakuwepo pia na Bodi
ya Utalii (TTB), Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Mzumbe, Mamlaka
ya Bandari Tanzania (TPA), Mabenki, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, Kampuni ya
Ndege ya Tanzania (ATCL), Shirika la Maendeleo la Taifa (TPDC) na wengine.
“Lengo la
kuwaalika wadau hawa ni kuwaonyesha wageni wetu huduma mbalimbali zinazotolewa
nchini na kuungana na Serikali kutangaza vivutio nchini ikiwemo kuunga mkono
Filamu ya ‘Royal Tour,” Mhe. Kitusi amesema.
Amesema kuwa jukwaa
hilo la Majaji Wakuu limekuwa likikutana kila mwaka katika moja ya Nchi
mwanachama kwa lengo la kuelimishana na kubadilishana uzoefu wa utatuzi wa
changamoto mbalimbali ili kuboresha huduma ya utoaji wa haki kwa wananchi.
Mkutano huo wa
Wahariri na Waandishi wa habari umehudhuriwa pia na Jaji Mfawidhi wa Kituo
Jumuishi cha Utoaji Haki Masuala ya Familia, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, Naibu
Msajili wa Mahakama hiyo, Mhe. Martha Mpaze, Mwenyekiti
wa Kamati Ndogo ya Elimu na Habari, Bw. Machumu Essaba
na sehemu ya wajumbe wa Kamati ya maandalizi ya Mkutano huo.
Katika kutambua na
kukuza jukumu muhimu la Mahakama ndani ya Kanda, Majaji Wakuu wa Mashariki na Kusini
mwa Afrika waliamua kuanzisha Jukwaa mwaka 2003 ili, pamoja na mambo mengine, kuzingatia
Utawala wa Sheria, Demokrasia, Uhuru wa Mahakama na kukuza mawasiliano ya
pamoja.
Maono au mtazamo
wa Jukwaa hilo ni kuwa na Mahakama iliyobadilika, iliyo huru, iliyounganishwa
na yenye umoja ambayo inakuza utawala wa sheria, haki, demokrasia na utawala
bora ili kuhakikisha ustawi, usawa, amani na usalama wa raia wote.
Kanuni zinazoongoza utendaji kazi na uendeshaji wa umoja huo ni kukuza utawala wa sheria, utoaji wa haki bora inayopatikana kwa wote, utawala bora na maadili ya pamoja, uwazi, uhuru, kutopendelea, uadilifu na uwajibikaji, kukuza utamaduni wa haki za binadamu, uhuru, uvumilivu na kuishi pamoja kwa amani.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni