Ijumaa, 22 Septemba 2023

KAMATI ZA MAADILI ZATAKIWA KUSIMAMIA SHERIA KANUNI NA MIONGOZO INAYOTOLEWA NA TUME

 Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mbeya

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dr. Francis Kasabubu amewataka wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama mkoani humo kusimamia Sheria, kanuni, na miongozo inayotolewa na Tume ya Utumishi wa Mahakama wanapotekeleza mashauri ya nidhamu kwa Maafisa Mahakama ngazi za mikoa na wilaya.

Akifungua Mafunzo ya siku tatu kwa wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama wa mikoa ya Mbeya na Songwe yenye lengo la kuzijengea uwezo kamati hizo, Dr. Kasabubu amesema endapo Sheria, kanuni na miongozo itazingatiwa ni wazi kuwa wajumbe hao watatekeleza kwa usahihi mashauri ya nidhamu kwa Maafisa Mahakama.

Mkuu huyo wa Mkoa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama Mkoa wa Songwe alisema mafunzo hayo yanayotolewa na Tume ya Utumishi wa Mahakama yatasaidia kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati za Maadili na kutatua changamoto zilizopo katika utekelezaji wa Sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya Utumishi wa Umma.

”Mafunzo haya ni moja ya misingi ya utekelezaji wa utawala bora wa Tume ya Utumishi wa Mahakama inayozingatia Sheria, kanuni, taratibu na miongozo katika usimamizi wa majukumu ya Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama” alisema.

Mkuu huyo wa Mkoa aliwakumbusha wajumbe wa Kamati za Maadili wajibu wao muhimu wa kuhakikisha kuwa haki za Maafisa Mahakama zinalindwa pale inapotokea wamekiuka utaratibu katika utekelezaji wa majukumu yao ya utoaji haki na si kuwakomoa.

Akizungumzia mafunzo hayo, Dr. Kasabubu alisema baadhi ya mada zitakazotolewa kwenye mafunzo hayo ni kuhusu historia ya Tume ya Utumishi wa Mahakama, uwasilishwaji wa malalamiko ya wananchi kwenye Kamati za Maadili na utaratibu wa kuyashughjulikia malalamiko hayo.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Mbeya Mhe. Dunstan Ndunguru amewataka wajumbe wa Kamati za Maadili kuyatumia mafunzo hayo kama chachu katika kushughulikia mashauri ya kinidhamu kwa Maafisa Mahakama.

”Naishukuru Tume ya Utumishi wa Mahakama na kuipongeza kwa  kuandaa mafunzo haya muhimu, naamini mafunzo haya yatakuwa ni  endelevu kwa kuwa wajumbe wake wamekuwa wakihama mara kwa mara vituo vyao vya kazi na wengine kuteuliwa wapya hususan wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya”, alisema.

Baada ya kukamilika kwa mapitio ya Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Namba 4 ya mwaka 2011 sura ya 237 ambazo ni kanuni za Uendeshaji wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama wa Mikoa na Wilaya za mwaka 2023, Tume imeanza kutoa mafunzo kwa wajumbe wa kamati za Maadili ili kuboresha utendaji kazi wa Kamati hizo.

Aidha, katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Tume imepanga kufanya mafunzo katika mikoa sita nchini ambayo ni Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe, Manyara na Arusha.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama ya mkoa huo Dr. Francis Kasabubu akifungua Mafunzo ya siku tatu yanayolenga kuimarisha utendaji kazi wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama yaliyoandaliwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama kwa wajumbe wa kamati hizo wa Mikoa ya Mbeya na Songwe pamoja na wilaya zake.

 

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Maafisa Mahakama mkoani humo Bw. Juma Homera (Katikati) akiwa katika Picha ya pamoja na Viongozi wengine wakati wa Mafunzo yanayolenga kuimarisha utendaji kazi wa    Kamati za Maadili yaliyoandaliwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama kwa Wajumbe wa Kamati hizo wa Mikoa ya Mbeya na Songwe na wilaya zake . Wa pili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dr. Francis Kasabubu na wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Lameck Mlacha, akifuattiwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu kanda ya Mbeya Mhe. Dunstan Ndunguru. Wa kwanza kulia ni Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Nidhamu na Maadili) Bi. Alesia Mbuya.

Wakuu wa wilaya za mkoa wa Mbeya ambao pia ni Wenyeviti wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama ngazi ya Wilaya wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dr. Francis Kasabubu baada ya kufungua  Mafunzo ya siku tatu yanayolenga kuimarisha Utendaji kazi wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama yaliyoandaliwa Tume kwa wajumbe wa kamati hizo wa Mikoa ya Mbeya na Songwe pamoja na wilaya zake. Wa pili kulia ni Jaji wa Mahakam ya Rufani Mhe. Lameck Mlacha na kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Mbeya Mhe. Dunstan Ndunguru. Kulia ni Naibu Katibu wa Tume(Ajira na Uteuzi) Bi. Enziel Mtei

Naibu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama (Nidhamu na Maadili) Bi. Alesia Mbuya akizungumza wakati wa Mafunzo yanayolenga kuimarisha Utendaji kazi wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama yaliyoandaliwa Tume kwa wajumbe wa kamati hizo wa Mikoa ya Mbeya na Songwe pamoja na wilaya zake.

Watumishi wa Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dr. Francis Kasabubu (Katikati) mara baada ya kufungua  Mafunzo ya siku tatu ya Kuimarisha utendaji kazi wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama yaliyoandaliwa Tume kwa wajumbe wa kamati hizo wa Mikoa ya Mbeya na Songwe pamoja na wilaya zake.



 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni