Ijumaa, 1 Septemba 2023

MAHAKAMA KANDA YA MTWARA KUANZISHA KAMATI ZA ELIMU YA SHERIA

Na Hilari Herman-Mahakama, Lindi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim hivi karibuni aliongoza kikao maalumu alichokiitisha kujadili namna watakavyofanikisha kuunda kamati za utoaji elimu katika ngazi zote za Mahakama katika Kanda hiyo.

Kikao hicho kilifanyika katika Ukumbi wa Mahakama Kuu Mtwara na kuhudhuriwa na wadau wa haki jinai na Viongozi wa Kanda hiyo, huku Mahakimu wengine wakishiriki kwa njia ya Mtandao (video Conference).

Akizungumza kwenye kikao hicho, Mhe. Ebrahim alisema hiyo ni ishara ya uzinduzi wa kamati za utoaji elimu kwa Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi na Mahakama zote za Wilaya na Mwanzo zilizopo katika Kanda hiyo ili kurahisisha zoezi la utoaji elimu kwa wananchi kwa kugusa nyanja zote.

Jaji Mfawidhi alieleza kuwa moja ya malengo ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania ni kurudisha imani ya wananchi kwa Mahakama, hivyo alisisitiza jukumu hilo haliwezi kufanywa na Mahakama pekee, bali kwa kushirikiana na wadau wote wa haki katika majukwaa mbalimbali ya utoaji elimu.

“Najua kila taasisi ina namna ya kuwafikia wananchi, lakini uongozi wa Mahakama Kanda ya Mtwara umeona kuwashirikisha ninyi wadau kwani tunaowajibu wa kuwafikia wananchi kwa umoja wetu ili kuweza kushughulikia matatizo na kero zao tukiwa kama timu moja yenye kutaka kusongeza mbele gurudumu la utoaji haki kwa wakati,” alisema Mhe. Ebrahim.

Wadau walifurahishwa na juhudi kubwa zinazofanywa na Mahakama ya Tanzania na kuahidi kutoa ushirikiano katika zoezi zima la utoaji elimu kwa jamii ili kupunguza kero na malalamiko kutoka kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim akitoa neno la ufunguzi wa kikao hicho.
Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Fredrick Lukuna akiwakaribisha wadau, Mahakimu na viongozi wengine kwenye kikao (hawapo kwenye picha).
Kamati ya utoaji elimu inayohusisha wadau, Mahakimu na Viongozi wengine wa Mahakama Kanda ya Mtwara (juu na chini)wakifuatilia kwa makini mada zinazowasilishwa.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi, Mhe. Consolata Singano akichangia mada kwa njia ya Mtandao (video conference).

Wadau, Mahakimu na Viongozi mbalimbali wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim (aliyekaa katikati), kushoto kwake ni Naibu Msajili, Mhe. Fredrick Lukuna na Kulia kwakwe ni Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Mtwara, Bw. Richard Mbambe.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni