Jumanne, 26 Septemba 2023

MAHAKAMA SPORTS YAKOLEZA MOTO

·Yafanya mazoezi ya kufa mtu

·Mwenyekiti asema ameridhika

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) inaendelea na mazoezi makali ya mwisho mwisho ili kujifua kuelekea mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayotarajia kuanza mwishoni wa mwezi huu wa Septemba, 2023 mkoani Iringa.

Akizungumza katika viwanja vya mazoezi vilivyoko Shule ya Sheria maeneo ya Mawasilisho jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema kwa sasa wapo tayari kwa ajili ya mashindano hayo kwani kiwango kinachoonyeshwa na vijana wake kwenye mazoezi kinaridhisha.

“Nimeridhika, kama mambo yataendelea kama hivi na kama hakutakuwa na majeruhi yeyote, tunaenda kwenye mashindano kuzoa kila kitu. Tuna timu nzuri kwenye kila mchezo na ari ya wachezaji kwenye maeneo yote ipo juu sana. Kwa kweli safari hii mambo ni mazuri sana,” alisema.

Alieleza kuwa tangu wanamichezo kutoka mikoani wawasili jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya mazoezi ya pamoja wamethihirisha Mahakama Sports itakuwa timu imara kwenye mashindano.

Dede amewahimiza wachezaji wote kuendelea kujituma kwenye mazoezi kwa dakika hizi za lala salama na kuzingatia maelekezo ya Mwalimu ili kukamilisha programu yake kabla ya kuelekea mkoani Iringa kesho tarehe 27 Septemba, 2023 kwenye mashindano hayo.

Michezo ambayo Mahakama Sports inatarajia kushiriki katika mashindano hayo ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha Wanaume na Wanawake pamoja na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Kocha wa Timu ya Netiboli ya Mahakama Sports Paul Mathias (mwenye kofia) akizungumza na vijana wake kwenye viwanja vya mazoezi. Anayefuatilia kwa karibu mwenye shati jeupe ni Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende.

Wachezaji wa Timu ya Netiboli wakiwa kwenye mazoezi.
Wachezi wa Timu ya Mpira wa Miguu wakijifua kisawa sawa, picha chini ni mchezaji wa Timu hiyo akimiliki mpira kwenye mtanange wa kirafiki na Timu ya Mawasiliano.

Timu ya Kamba (juu na chini) ikiwa kwenye mazoezi ya kufa mtu.



Mazoezi yamekolea..



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni