· Tume ya Utumishi wameyataka wenyewe
Na
Faustine Kapama -Mahakama, Iringa
Timu ya Mahakama ya
Tanzania (Mahakama Sports) leo tarehe 30 Septemba, 2023 imeendelea kutoa dozi
baada ya kuzoa pointi mbili katika kila timu kwenye mchezo wa Kamba Wanaume na
Kamba Wanawake.
Katika michezo hiyo
iliyofanyika katika uwanja wa Mkwawa mjini hapa, Kamba Wanaume walikutana na
Mawasiliano, huku Kamba Wanawake wakikabana koo na Tume ya Utumishi na
kufanikiwa kuzilambisha nyasi timu hizo.
Ulikuwa mchezo wa Kamba
Wanawake ulioanza ambapo timu ya Tume ya Utumishi nusra iondolewe kwenye
mashindano baada ya kuingia uwanjani kwa kusitasita wakihofia kichapo.
Mwamuzi alipouita mchezo
huo, Tume ya Utumishi walijitokeza haraka haraka, lakini walipoziona ‘Tembo za
Mahakama’ wakatokomea, wakidai haikuwa mechi yao.
Baada ya kujiridhisha,
huku timu ya Mahakama ikiwa inasubiri mpinzani uwanjani, waamuzi waliwaita tena
Tume ya Utumishi lakini wakahofia kuingia. Walipoitwa kwa mara ya tatu ndipo
wakaibuka kutoka mafichoni kukabiliana na miamba ya Mahakama.
Mchezo huo ulipoanza,
Mahakama hawakuwa na huruma na mtu, wakawachakaza vibaya wapinzani wao kwenye
mivuto yote miwili, hivyo kuzoa pointi zote mbili.
Baadaye, mchezo wa Kamba
Wanaume ulifuata kwa Mahakama kutifuana na Mawasiliano. Kipigo kikaendelea
kutembea ambapo Mawasiliano walikiona cha mtema kuni baada ya kuchakazwa vibaya
kwenye mivuto yote miwili.
Kufuatia ushindi huo,
timu za Mahakama zinaendelea kupeperusha vyema bendera ya Mahakama, huku
Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede akiwapongeza vijana wake kwa
kuendeleza kile wanachokitaka.
"Kazi inaendelea,
kwani bado hatujamaliza. Niwakumbushe tu wapinzani wetu kuwa vipigo kama hivi
vinaendelea na yoyote tutakayekutana naye ajiandae kisaikolojia kupokea
kipigo," amesema.
Kwa
mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia
kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.
Katika mpira wa miguu,
timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji,
RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na
itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.
Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume,
timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma,
Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana
vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya
Uchaguzi (NEC).
Mahakama Sports inashiriki
katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira
wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.
Katika mashindano ya
SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa
makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.
Michezo ambayo Mahakama
Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa
kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa
kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume
walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni