· Bendera ya Mahakama juu SHIMIWI Iringa
·Elimu yakimbiwa na mashabiki wake
Na
Faustine Kapama -Mahakama, Iringa
Ukichezea moto utakuunguza.
Ndicho inachokifanya Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli kwenye
Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI)
mkoani hapa.
Katika mchezo huo
uliochezwa leo tarehe 30 Septemba, 2023 katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Ruaha, timu ya Mahakama
ilikutana na timu ngumu ya Maji ambayo imeungua vibaya baada ya kupokea kichapo
cha vikapu 28 kwa 16.
Mchezo huo uliochezwa kuanzia
saa 5:00 asubuhi ulianza kwa timu zote mbili kukamiana huku tupia tupia vikapu
ikawa bandika bandua. Kila timu inapotupia, timu nyingine nayo inatupia.
Ilikuwa timu ya Elimu
iliyoanza kutupia dakika za mwanzo za mchezo, lakini Mahakama Sports ikachomoa
baada ya muda mfupi. Kitendo cha Elimu kutangulia kutupia vikapu kiliwaamusha
wachezaji wa Mahakama na kuanza kulisakama lango la wapinzani wao.
Tupia tupia vikapu
iliendelea na hadi timu zote zinaenda mapumziko, Mahakama Sports ilikuwa mbele
kwa kutumbukiza vikapu 15 kwa 11. Kipindi cha pili kiliendelea kwa Mahakama
kuzidisha mashambulizi na kuzidi kuwakandamiza wapinzani wao.
Baada ya kugundua utoaji
wa dozi unazidi kuendelea, mashabiki wa timu ya Elimu walizima muziki na mavuvuzela
yao na kutokomea kusikojulikana na kuiacha timu yao ikiendelea kubamizwa na
Mahakama Sports. Hadi kipenga cha mwisho kinapulizwa, Mahakama Sports ikazoa
vikapu 28 kwa 16 walizoambulia Elimu.
Akizungumza baada ya
mchezo huo, Katibu wa Mahakama Sport Robert Tende amesema moto waliouwasha utaendelea
kuwaunguza wote wanaojitia kimbelembele kucheza nao kwenye mashindano hayo na hawatabaki
salama.
“Mjomba, huu sio moto wa
kifuu, ukichomeka kidole chako utaungua, tena vibaya mno. Timu yoyote
itakayoingiza timu uwanjani ikubali kuvumulia maumivu, hawatabaki salama, amini
nakwambia,” alisema.
Mwalimu wa timu Paul
Mathias amewashukuru vijana wake kwa kupambana na kuibuka na ushindi huo muhimu
dhidi ya timu hiyo ngumu. “Nawapongeza sana vijana wangu, kwa kweli
hawajaniangusha. Tulipoanzia ndipo tutakapomalizia, hakuna kupoa,” alisema.
Kwa
mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia
kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.
Katika mpira wa miguu,
timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji,
RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na
itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.
Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume,
timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma,
Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana
vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya
Uchaguzi (NEC).
Mahakama Sports inashiriki
katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira
wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.
Katika mashindano ya
SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa
makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.
Michezo ambayo Mahakama
Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa
kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa
kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume
walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni