Jumamosi, 23 Septemba 2023

MAHAKIMU MANYARA WASISITIZWA KUZINGATIA MIONGOZO, TARATIBU WANAPOTOA HAKI.

Christopher Msagati - Manyara

Mahakimu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara wameshiriki mafunzo ya siku moja ya kuwajengea uwezo wa namna bora ya kutekeleza na kuimarisha jukumu lao la utoaji haki kwa wote na kwa wakati, ikiwa ni sehemu ya mafunzo ya ndani ya Kanda hiyo.

Akizungumza katika mafunzo hayo yaliyofanyika jana tarehe 22 Septemba, 2023 mjini Babati mkoani Manyara, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza aliwakumbusha Mahakimu hao kuyatumia mafunzo hayo kama sehemu muhimu ya kusaidia kujenga uelewa wa pamoja wa miongozo na taratibu zinazosimamia jukumu lao la kila siku la utoaji haki kwa wananchi.

“Ni nafasi muafaka ya kuwekana sawa na kukumbushana yale ambayo tunayafanya kila siku katika majukumu yetu, na pale ambapo tunaonekana tunafanya kwa kiwango cha chini, mafunzo haya yatatusaidia kutuimarisha zaidi katika weledi na ufanisi wetu”, aliongeza Mhe. Kahyoza

Mafunzo hayo yaliwahusisha Mahakimu wote kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Manyara inajumuisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara pamoja na Mahakama zake za Wilaya ambazo ni Babati, Hanang, Mbulu, Kiteto na Simanjiro. Aidha, Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kutoka Wilaya hizo nao walishiriki mafunzo hayo.

Aidha, Mada mbalimbali ziliwasilishwa kwa umahiri mkubwa kutoka kwa wawezeshaji wa mafunzo hayo, ikiwa ni pamoja na Wajibu wa Mahakama katika Kupambana na Rushwa, Maadili ya Watumishi wa Mahakama, Taratibu za Uendeshaji wa Mshauri mbalimbali kama vile Uhujumu Uchumi, Ubakaji, Mirathi pamoja na Mshauri yanayosikilizwa katika Mahakama za Mwanzo. Vile vile Mahakimu hao, walijifunza namna bora ya uandaaji wa Bajeti pamoja na utekelezaji wake.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. Benard Mpepo aliwakumbusha Mahakimu hao juu ya utekelezaji wa maagizo ya Nyaraka mbalimbali zinazotolewa na Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi na Msajili Mkuu.

Imekuwa ni desturi kwa Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara kutoa elimu kwa watumishi wake mara kwa mara ili kuwaimarisha katika utendaji wa majukumu yao ya kila siku. Hii ni pamoja na kuwakumbusha kuhusu Maadili.

    Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akitoa mafunzo kuhusu taratibu mbalimbali za uendeshaji wa mashauri kwa Mahakimu (hawapo pichani) jana tarehe 22 Septemba, 2023 mjini Babati mkoani Manyara.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. Gladys Barthy akitoa mafunzo kwa Mahakimu wa Kanda hiyo.

     Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo akifafanua kuhusu Nyaraka mbalimbali zinazotoka kwa Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi na Msajili Mkuu.

Sehemu ya Mahakimu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara wakifuatilia kwa kina mafunzo hayo.

    Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Mahakimu walioshiriki mafunzo hayo. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. Gladys Barthy (wa pili kushoto),  Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mhe. Bernard Mpepo (wa kwanza kushoto) na wa pili kulia ni Afisa kutoka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Manyara Bw. Sadiki Nombo.

(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


H





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni