Jumatatu, 25 Septemba 2023

WATUMISHI MAHAKAMA DODOMA WAPATIWA ELIMU YA UWEKEZAJI DHAMANA ZA SERIKALI

Na Stanslaus Makendi – Mahakama Kuu Dodoma

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma hivi karibuni walipatiwa elimu ya uwekezaji kwenye dhamana za Serikali ili kuwajengea uelewa namna wanavyoweza kunufaika na uwekezaji huo.

Elimu hiyo ilitolewa na mwezeshaji kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dar es Salaam, Bw. Fidelis Mkatte ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa ndani wa utoaji wa elimu kwa watumishi unaoratibiwa na Kamati ya Elimu ya Mkoa.

Katika mafunzo hayo, mwezeshaji aliwaasa washiriki wa mafunzo hayo kuanza kuwekeza fedha zao katika masoko ya fedha ili waweze kunufaika na huduma mbalimbali zinazopatikana.

Alisisitiza kuwa uwekezaji huo ni fursa kwa wananchi wote na huiwezesha Serikali kupata fedha za kuendesha miradi mbalimbali ya maendeleo nchini, kugharamikia upungufu katika bajeti na faida nyingine lukuki.

Bw. Mkatte alieleza kuwa uwekezaji huo ni salama kwani Serikali haitarajiwi kukiuka mategemeo ya wadai wake wakati wa malipo unapofika na siyo rahisi kufilisika kama ilivyo Taasisi nyingine za kifedha na uwekezaj.

“Dhamana za Serikali zinatumika kama dhamana ya mikopo katika Taasisi za kifedha, zinaweza kuhamishika au kuuzwa na mwekezaji kabla ya muda wake wa kuiva iwapo atakutana na hali inayomlazimu kufikia uamuzi huo,” alisema.

Alibainisha kuwa BoT, kwa niaba ya Serikali zote mbili yaani Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, huuza dhamana za Serikali ikiwa ni njia ya kukopa fedha kutoka kwa Taasisi mbalimbali na mwananchi mmoja mmoja.

Bw. Mkatte alisema dhamana za Serikali za muda mrefu ambazo huiva katika muda unaozidi mwaka mmoja huuzwa kwenye soko la awali kwa njia ya ushindani kupitia minada na baadaye kwenye soko la upili.

“Mtu yeyote au kikundi kilichosajiliwa kinaweza kuwekeza katika dhamana za Serikali kwani kiwango cha chini cha kuwekeza kwenye dhamana hizo za muda mrefu ni rafiki kwa kuwa uwekezaji huo huanzia kiwango cha shilingi milioni moja,” alisema.

Alieleza kuwa utaratibu wa ununuzi na uuzaji wa dhamana hizo hutolewa kupitia kwenye magazeti na pia taarifa zaidi hupatikana kwenye tovuti ya Benki Kuu ya Tanzania inayoonyesha itakavyotolewa na tarehe ya mnada.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, akizungumza wakati wa zoezi hilo alisema mafunzo hayo yamekuwa yenye manufaa kwetu.

“Natamani elimu hii tungeipata mapema zaidi. Hata hivyo, bado hatujachelewa sana, ni wakati wa kujitafakari na kufanya maamuzi. Wapo watu tunaowafahamu ambao wamenufaika na uwekezaji katika dhamana za Serikali,” alisema.

Mhe. Dkt. Masabo aliwashukuru wajumbe wa Kamati ya Elimu inayoongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Adam Mambi kwa kushirikiana na Mtendaji wa Mahakama Kanda, Bw. Sumera Manoti, kwa uratibu mzuri wa masuala ya utoaji wa elimu kwa umma na watumishi.

Sambamba na hilo, Jaji Mfawidhi aliushukuru uongozi wa BOT kwa kukubali ombi la kupatiwa mwezeshaji kwa ajili ya kutoa mafunzo hayo kwa watumishi.

Sanjari na zoezi hilo, watumishi wa Kituo hicho walipatiwa pia elimu kuhusu mafao ya hitimisho la ajira na mafao mengine yanayotolewa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (PSSSF).

Watumishi hao mwezi ujao wa Oktoba watapatiwa elimu ya mabadiliko ya kifikra, masuala ya saikolojia na afya ya akili ili kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao na kumudu maisha yao nje ya kazi.

Mwezeshaji wa mafunzo ya uwekezaji katika dhamana za Serikali kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Bw. Fidelis Mkatte, akifafanua jambo wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma hivi karibuni.
Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma walioshiriki mafunzo hayo, kuanzia kushoto ni Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt. Juliana Masabo, Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, Mhe. Dkt. Adam Mambi na Mhe. Suleiman Hassan wakifuatilia kwa umakini mafunzo hayo.

Sehemu ya watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma (juu na chini) wakifuatilia mafunzo hayo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu Mkoa wa Dodoma, Mhe. Dkt. Adam Mambi akiteta jambo na Mhe. Jaji Suleiman Hassan wakati wa mafunzo hayo.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Silivia Lushasi akiuliza swali kwa mwezeshaji (hayupo pichani) mara baada ya kuwasilishwa kwa mada ya uwekezaji katika dhamana za Serikali.
Sehemu ya wahudhuriaji wakifuatilia kwa umakini mada zilizowasilishwa katika mafunzo hayo.
Mwezeshaji wa mafunzo ya uwekezaji katika dhamana za Serikali, Bw. Mkatte kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BOT) akihitimisha uwasilishaji wa mada mbalimbali katika mafunzo hayo na kuwaasa watumishi hao kuchangamkia fursa hiyo ya uwekezaji.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo (wa kwanza kushoto) akimsikiliza mwezeshaji (hayupo pichani) wakati akishukuru kwa niaba ya Benki Kuu ya Tanzania kufuatia salam za pongezi na shukrani zilizotolewa na Kiongozi huyo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni