Jumanne, 12 Septemba 2023

TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA YAFUNGUA UKURASA WA USHIRIKIANO NA ZANZIBAR


Na Lydia Churi-Tume ya Utumishi wa Mahakama

Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania imefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baada ya kukukutana na Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama ya Zanzibar kwa lengo la kufahamiana na kubadilishana uzoefu wa kazi katika masuala ya utoaji haki.

Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel pamoja na watumishi wa Sekretariet hiyo wako katika ziara ya siku mbili visiwani humo itakayomalizika leo Septemba 12, mwaka 2023.

Akifungua Mkutano baina ya Tume hizo mbili jana Zanzibar, Prof. Ole Gabriel amewataka watumishi wa Sekretariet hizo zote mbili kujadiliana kwa kina kuhusu mambo manne ambayo ni muundo wa Tume hizo, nidhamu na maadili, matumizi ya Teknolojia katika utoaji haki na kuongeza imani ya wananchi kwa mhimili wa Mahakama.

Alisema ni muhimu wajumbe hao kujadili kuhusu muundo wa Tume kwa pande zote mbili za Muungano ili kuona mchango wake katika masuala ya utoaji haki.  Aliongeza kuwa japokuwa kuna tofauti ya muundo wa Tume kati ya Tanzania bara na Zanzibar lakini haki ni jambo linalogusa watu wote.

Katibu huyo wa Tume pia amewataka wajumbe wa Mkutano huo kujadiliana namna ya kushirikiana katika matumizi ya Teknolojia ya habari na mawasiliano kwenye  shughuli za utoaji. Alisema Mahakama ya Tanzania hivi sasa imepiga hatua kubwa kwenye matumizi hayo ambapo inayo mifumo mbalimbali ya kurahisisha kazi ya utoaji haki.

Aidha Prof. Ole Gabriel alitoa wito kwa watumishi wa Sekretaet zote mbili za Tume ya Utumishi wa Mahakama kuwa na nidhamu ya hali ya juu wanapotekeleza majukumu yao ili kujenga taswira chanya ya Mahakama kwa wadau wake.

”Nidhamu ni jambo la msingi na muhimu kwa watumishi wa Mahakama kwani bila nidhamu kwa watumishi wa Mhimili huo ni vigumu kwa wananchi kuwa na imani na Mahakama, pia inarahiusisha mnyororo wa utoaji haki”, alisema Katibu wa Tume.

Aliwataka watumishi hao wa Tume kulinda taswira nzuri ya Mhimili wa Mahakama iliyojengeka ili wananchi wawe na imani zaidi na mhimili huo ambapo alisema tathmini iliyofanyika hivi karibuni inaonesha kuwa kiwango cha imani ya wananchi kwa Mahakama kimeongezeka kutoka asilimia 65 mwaka 2015 na kufikia asilimia 88 mwaka huu wa 2023.

Kwa upande wake, Katibu wa Tume hiyo kwa upande wa Zanzibar ambaye pia ni Naibu Mrajis Mhe. Salim Hassan Bakari alisema Mkutano huo baina ya Tume hizo mbili ni utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi aambapo alizitaka taasisi za Serikali kwa pande zote mbili za Muungano kushirikiana katika kuwahudumia wananchi.

Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania imeundwa na Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Aidha, majukumu ya Tume yameelezwa kwenye katiba hiyo katika Ibara ya 113 (1) ikisomwa pamoja na kifungu cha 29 cha Sheria ya Uendeshaji wa Mahakama Na. 4 ya mwaka 2011. Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo cha kikatiba kilichopewa jukumu la kusimamia uendeshaji wa Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel (Katikati) akizungumza wakati akifungua Mkutano kati ya Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara na Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahkama Zanzibar leo Visiwani humo. Sekretaerti ya Tume imeanza ziara ya siku mbili Zanzibar yenye lengo la Kubadilishana uzoefu katika masuala ya utoaji haki. Kushoto ni Mrajis wa Mahakama Kuu Zanzibar Mhe. Valentina Katema na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama Kuu Zanzibar Bw. Kai Bashiru Mbarouk.  

Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara na ile ya Zanzibar wakati walipomtembelea ofisini kwake leo ikiwa ni sehemu ya ziara yao visiwani humo yenye lengo la kubadilishana uzoefu katika masuala ya utoaji haki kati ya Tume hizo mbili.

Viongozi wa Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahkama Zanzibar wakiwa kwenye Mkutano kati yao na Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara leo visiwani Zanzibar.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Sekretariet za Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara na ile ya Zanzibar leo visiwani humo.

Baadhi ya watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara pamoja na Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye Mkutano kati yao na Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahkama Zanzibar uliofanyika visiwani humo.

 

Naibu Makatibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara na Katibu wa Tume hiyo Zanzibar wakifuatilia jambo wakati wa Mkutano kati ya Tume hizo mbili. Kulia ni Naibu Katibu (Ajira na Uteuzi) Bibi Enziel Mtei na kushoto ni Naibu Katibu (Nidhamu na Maadili) Bi. Alesia Mbuya., Katikati ni Naibu Mrajis Mahkama Kuu Zanzibar ambaye pia ni Katibu wa Tume Mhe. Salum Hassan Bakari.

Baadhi ya watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania Bara pamoja na Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye Mkutano kati yao na Sekretariet ya Tume ya Utumishi wa Mahkama Zanzibar uliofanyika visiwani humo.

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni